Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ni Vigumu Kufanikiwa?

Kwa Nini Ni Vigumu Kufanikiwa?

Kwa Nini Ni Vigumu Kufanikiwa?

Msichana huyu alikuwa mwimbaji maarufu alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi na alikuwa tajiri sana. Ni watu wachache sana ambao hufaulu kuwa maarufu na matajiri kadiri hiyo wakiwa na umri mchanga hivyo. Lakini mambo yakaanza kumwendea mrama. Baada ya kutalikiwa mara mbili, alihitaji kulazwa katika vituo vya kuwatibu waraibu wa vileo na dawa za kulevya. Kila kitu maishani mwake kikaanza kwenda kombo.

INASIKITISHA kwamba watu wengi sana hujipata katika hali kama ya msichana huyo. Mara nyingi vyombo vya habari husimulia mambo yenye kuhuzunisha kuhusu watu maarufu. Hata wafanyabiashara ambao huonekana wamefanikiwa sana wanapatwa na matatizo maishani. Gazeti moja lilisema hivi kuhusu wafanyabiashara waliofanikiwa sana: “Jitihada za kupata faida kubwa zinaharibu kazi, zinatenganisha familia, na kufanya watu watumie dawa za kulevya . . . Pesa za ziada ambazo wafanyakazi katika soko la hisa la Marekani hupata kwa sababu ya kazi nzuri huwafanya wafanyabiashara fulani wajihisi salama kabisa, wengine hupatwa na matatizo ya kihisia kwa sababu ya mkazo wa kufanya kazi kwa bidii, na wengine hushuka moyo kabisa.

Je, matatizo kama hayo husababishwa na jitihada zisizofaa za kupata furaha na mafanikio? Ni kweli kwamba tunahitaji kiasi fulani cha pesa maishani. Lakini, je, kujikusanyia mali ndiko kunaleta mafanikio maishani? Uchunguzi unaonyesha mambo tofauti. Kwa mfano, uchunguzi nchini China unaonyesha kwamba katika kipindi fulani hivi karibuni wakati mapato ya wastani yaliongezeka kwa asilimia 250, kwa ujumla watu hawakuridhika sana na maisha yao.

Hivyo, mafanikio halisi yanapimwa na kitu muhimu zaidi kuliko kazi ya kimwili au thamani ya nyumba, gari, au saa ambayo mtu anamiliki. Je, si jambo linalopatana na akili kupima mafanikio kwa jinsi mtu alivyo, kutia ndani kanuni anazofuata na kusudi lake maishani? Kwa mfano, mtu anaweza kuwa na akili na uwezo mwingi, lakini asiwe na maadili mazuri, upendo, na marafiki wa kweli. Mwingine anaweza kuwa maarufu na mwenye pesa lakini akitazama nyuma maishani anajiuliza, ‘Kulikuwa na faida gani kupata vitu hivyo vyote? Maisha yangu yana kusudi gani?’

Basi, inapatana na akili kusema kwamba maisha ya watu waliofanikiwa kikweli yanategemea mambo muhimu zaidi kutia ndani kuongozwa na kanuni zinazofaa. Kwa sababu hiyo, wanakuwa na amani ya moyoni, wanajiheshimu, na kuwaheshimu wengine. Pia, wanakuwa na kusudi lenye maana na linaloridhisha maishani ambalo linahusisha kutanguliza mambo mengine badala ya mapendezi yao wenyewe. Huenda wengine wakajiuliza, ‘Ni kanuni gani hizo na ni kusudi gani hilo?’ Je, sisi wenyewe tunaweza kupata majibu ya maswali kama hayo, au tunapaswa kutafuta majibu mahali pengine? Makala zinazofuata zitazungumzia mambo hayo.

[Sanduku katika ukurasa wa 3]

MAONI YALIYOPOTOKA KUHUSU MAFANIKIO

Kulingana na watafiti wa kitiba, idadi inayoongezeka ya wachezaji wenye umri mchanga wanatumia dawa hatari za kuongeza nguvu mwilini ili washinde. Kichapo Education Update kilicho kwenye Intaneti kinasema: “Katika uchunguzi uliofanywa hivi karibuni wanafunzi wa chuo waliulizwa hivi: ‘Ukijua kwamba utashinda ama kuingizwa katika timu kwa sababu ya kutumia steroidi, lakini uwe mgonjwa baada ya miaka mitano, je, bado ungezitumia?’ Karibu wote walisema wangezitumia. Walipoulizwa ikiwa wangezitumia ‘lakini wafe baada ya miaka mitano,’ asilimia 65 walisema wangezitumia.”