Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Kupata Wapi Mwongozo Unaofaa?

Tunaweza Kupata Wapi Mwongozo Unaofaa?

Tunaweza Kupata Wapi Mwongozo Unaofaa?

NI NANI anayeweza kutuonyesha jinsi ya kupata mafanikio ya kweli, si mafanikio katika mambo ya kimwili bali mafanikio halisi? Kama ilivyotajwa katika makala inayotangulia, mafanikio ya kweli yanapaswa kuhusianishwa na kanuni za maadili zinazofaa na kusudi muhimu maishani, na hayo ni mambo ambayo hayategemei umaarufu, mali, au uwezo.

Tunaweza kupata wapi kanuni zinazofaa na majibu ya maswali kuhusu kusudi la maisha? Je, ni kwa kujichunguza tu? Kwa kweli, tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, tunapatwa na tamaa mbaya zinazoweza kutuongoza kutenda maovu. (Mwanzo 8:21) Hivyo, mamilioni ya watu wanaendelea kufuatia mambo yasiyo na thamani ambayo Biblia inafafanua kuwa “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani.” (1 Yohana 2:16) Hiyo si njia ya kupata mafanikio halisi bali hayo ni mawazo tu yasiyo ya kweli yanayowafanya watu wakose kuona mambo kihalisi na wakose furaha. Hivyo, inafaa kwamba watu wengi humtegemea Muumba ajibu maswali muhimu zaidi maishani. *

Je, Tumtegemee Mungu?

Kwa nini inafaa kumtegemea Muumba wetu? Anajua kwa nini alituumba na hivyo, anajua tunapaswa kuwa na kusudi gani maishani. Pia anajua jinsi alivyotuumba, kimwili, kiakili, na kihisia. Kwa hiyo, Mungu anajua kanuni bora zaidi ambazo wanadamu wanapaswa kufuata. Isitoshe, Mungu ndiye mfano bora zaidi wa upendo, na hivyo anataka tuwe na furaha na tufanikiwe kikweli. (1 Yohana 4:8) Tunaweza kupata wapi mwongozo wake wenye upendo? Ni katika Biblia Takatifu ambayo Mungu alitupa kwa kutumia waandikaji 40. * (2 Timotheo 3:16, 17) Hata hivyo, je, tunaweza kuamini kabisa mwongozo unaopatikana katika kitabu hicho?

“Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake,” au matokeo yake, akasema Yesu Kristo, mwakilishi mkuu wa Mungu. (Mathayo 11:19; Yohana 7:29) Hekima kutoka kwa Mungu hutuongoza kwenye mafanikio na furaha ya kudumu, yaani, “njia yote ya yaliyo mema.” Kwa upande mwingine, hekima ya kibinadamu ambayo inampuuza Mungu haileti mafanikio wala furaha.—Methali 2:8, 9; Yeremia 8:9.

Fikiria miaka ya 1960 kulipokuwa na ile enzi ya maisha ya kihuni. Wakikataa viwango na mamlaka ya vizazi vya zamani, wengi walioishi maisha ya kihuni, walionyesha kwamba kutumia dawa za kulevya, kuishi kwa ajili ya sasa, na uhuru wa kingono ni mambo yanayofaa. Lakini je, hiyo ndiyo iliyokuwa njia inayofaa ya maisha? Je, iliwapa watu kusudi la kweli maishani na viwango wa maadili vilivyotokeza amani ya kweli ya moyoni na furaha ya kudumu? Historia inaonyesha kwamba njia hiyo ya maisha haikuboresha maisha bali ilichangia kuzorota kwa maadili katika jamii ya wanadamu.—2 Timotheo 3:1-5.

Tofauti na falsafa za wanadamu, sikuzote hekima ya Biblia imekuwa na matokeo mazuri. (Isaya 40:8) Unaposoma makala inayofuata, huenda utaona kwa nini hekima ya Biblia imekuwa na matokeo mazuri, kwa kuwa makala hiyo inazungumzia kanuni sita za Biblia ambazo zimewasaidia mamilioni ya watu kutoka karibu nchi zote kuwa na furaha na mafanikio ya kweli, haidhuru wana hali gani ya kiuchumi au ya kijamii.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona toleo la pekee la Novemba (Mwezi wa 11) 2007 la gazeti hili ambalo linazungumzia kichwa “Je, Unaweza Kuitegemea Biblia?” Makala katika toleo hilo zinatoa uthibitisho wa kihistoria, kisayansi, wa vitu vya kale, na uthibitisho mwingine unaoonyesha kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

 IMANI ZINAZOPUNGUZA THAMANI YA MAFANIKIO

Watu wengi wanaamini kwamba hakuna Mungu na kwamba uhai ulitokana na mageuzi. Ikiwa maoni hayo yangekuwa kweli, basi uhai ungekuwa umetokezwa tu kupitia aksidenti za kikemikali na za kibiolojia, na jitihada zetu za kupata kusudi na kanuni zinazotumika ulimwenguni pote hazingekuwa na maana.

Wengine wanaamini kwamba Mungu alituumba kisha akatuacha. Ikiwa hilo ni kweli, basi sisi ni mayatima kiroho na hatuna kusudi la kweli na viwango vinavyofaa. Hebu fikiria: Mungu alimpa kila mnyama hekima ya kisilika ili kutimiza sehemu yake duniani. Kwa sababu hiyo, hekima nyingi ya Mungu inaonekana katika ulimwengu unaotuzunguka. Je, Muumba huyohuyo angetuumba kisha atuache bila mwongozo wowote? La hasha!—Waroma 1:19, 20.

Kwa kufanya jitihada zetu za kutafuta kusudi na kanuni zinazotumiwa ulimwenguni pote kuwa za bure, falsafa za watu wasioamini kwamba kuna Mungu zinapunguza thamani ya mafanikio.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Hekima inayopatikana katika Biblia inathibitishwa kuwa inafaa kwa matokeo yake mazuri