Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tupo Hapa?

Kwa Nini Tupo Hapa?

Kwa Nini Tupo Hapa?

Ni nini kusudi la uhai?

MARA nyingi watu wamejiuliza maswali yaliyo hapo juu. Pia wao hujiuliza: Je, kuna kusudi lingine isipokuwa kuishi kwa miaka 70 au 80 kisha tufe?—Zaburi 90:9, 10.

Huenda tukajiuliza maswali kama hayo hasa tunapotambua kwamba maisha yetu ni mafupi sana. Bila shaka, si lazima tuwe tunakabili hatari maishani ili kujiuliza kwa nini tupo hapa. Kukata tamaa pia kunaweza kutufanya tujiulize swali hilo. Na watu wengine hujiuliza swali hilo wanapotafakari juu ya maisha yao.

Dave alikuwa na kazi yenye mshahara mnono, nyumba nzuri, na alifurahia kuwa pamoja na marafiki wake. Anasema hivi: “Usiku mmoja nilikuwa nikirudi nyumbani kutoka kwenye sherehe nilipojiuliza swali hili, ‘Je, hili ndilo kusudi la uhai?—Je, nitaishi kwa muda mfupi tu kisha nife? Au je, kuna kusudi lingine?’ Jambo lililonisumbua ni kugundua sikuwa na kusudi maishani wakati huo.”

Katika kitabu chake Man’s Search for Meaning, Viktor Frankl alisema kwamba baada ya kuachiliwa kutoka katika kambi za mateso, baadhi ya waokokaji wenzake wa yale Maangamizi Makubwa waliuliza swali kama hilo. Waliporudi nyumbani, baadhi yao walikuta kwamba wapendwa wao walikuwa wameangamia. Frankl aliandika hivi: “Ole wake yule ambaye siku ya kuachiliwa, alikuta maisha yakiwa tofauti sana kuliko alivyotarajia!”

Watu Wanaouliza Swali Hilo

Swali kuhusiana na kusudi la uhai limeulizwa na watu katika vizazi vyote. Biblia inatuambia kuhusu watu waliotaka kujua maisha yana kusudi gani. Ayubu aliuliza hivi baada ya kupoteza mali na watoto wake na alipougua ugonjwa mbaya: “Kwa nini sikufa tokea tumbo la uzazi? Kwa nini sikutoka tumboni kisha nikate pumzi?”—Ayubu 3:11.

Nabii Eliya alihisi vivyo hivyo. Huku akihisi kwamba yeye ndiye mwabudu pekee wa Mungu, alilalamika hivi: “Inatosha! Sasa, Ee Yehova, iondoe nafsi yangu.” (1 Wafalme 19:4) Watu wengi sana wamehisi hivyo. Kwa kweli, Biblia inamfafanua Eliya kuwa “mtu mwenye hisia kama zetu.”—Yakobo 5:17.

Safari Yenye Mafanikio Maishani

Maisha hulinganishwa na safari. Kama vile unavyoweza kuanza safari bila kufikiria utafika wapi, unaweza kuishi bila kutambua kusudi halisi la maisha. Ukifanya hivyo, utakuwa kama watu ambao mwandishi anayejulikana Stephen R. Covey anasema wanatafuta kusudi kwa kufanya maisha yawe yenye shughuli nyingi sana. Aliandika kuhusu wale ambao “wanapata mafanikio yasiyo na maana, mafanikio ambayo wamepata kwa kupoteza vitu ambavyo ghafula wanatambua vilikuwa vya muhimu zaidi kwao.”

Je, hukubali kwamba kuongeza mwendo katika safari ni bure ikiwa hatuelekei upande unaofaa? Vivyo hivyo, kutafuta kusudi maishani kwa kuwa na shughuli nyingi hakutaleta uradhi wa kweli.

Tamaa ya kujua kwa nini tupo hapa ni kawaida kwa watu wa utamaduni na umri mbalimbali. Inatokana na uhitaji muhimu ambao sote tunao, uhitaji wa kiroho ambao hauwezi kutoshelezwa hata baada ya mahitaji yetu ya kimwili kutimizwa. Hebu ona jinsi wengine wamejaribu kutosheleza uhitaji huo wanapotafuta kusudi la maisha.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Kutafuta kusudi maishani kwa kuwa na shughuli nyingi hakutaleta uradhi wa kweli

[Picha katika ukurasa wa 3]

Ayubu aliuliza kwa nini alizaliwa

[Picha katika ukurasa wa 4]

Eliya alikuwa na “hisia kama zetu”