Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nguvu za Udanganyifu za Matangazo ya Biashara

Nguvu za Udanganyifu za Matangazo ya Biashara

Nguvu za Udanganyifu za Matangazo ya Biashara

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI POLAND

Tomek anatazama televisheni kwa makini. Anasikiliza kwa makini tangazo la biashara linapowahimiza hivi wasikilizaji: “Mtoto wako akivalia vazi hili, atakuwa mwenye nguvu, umbo zuri, na rafiki zake watamsifu. Unapaswa kulinunua!” Tomek anakimbia kumwelekea baba yake akiimba wimbo aliosikia katika tangazo hilo. “Baba, utaninunulia vazi hilo?” anauliza.

▪ Kwa nini watoto wanataka vitu wanavyoona vikitangazwa? “Kwa sababu rafiki zao wana vitu hivyo, nao pia wanataka kuwa navyo. Wanataka kuwa sawa na wenzao,” anaeleza mwalimu mmoja aliyenukuliwa katika gazeti Rewia nchini Poland. Watoto wanaposihi, kulia, na kununa, wazazi fulani hukubali na kuwanunulia vitu wanavyotaka.

Ni nini kinachofanya matangazo yanayolenga watoto yawe yenye udanganyifu sana? Matangazo hayo “hayakazii bei, ubora, au faida za bidhaa hiyo,” anaeleza mwanasaikolojia Jolanta Wąs. Tangazo hilo limebuniwa “ili kuchochea hisia.” Wąs anasema hivi: “Watoto wadogo hawachanganui hadithi inayosimuliwa katika tangazo. . . . Hawalinganishi habari inayotolewa na mambo halisi wanayojua.” Na hata wakijaribu kufanya hivyo, uelewaji wao ni mdogo sana hivi kwamba hawawezi kuchunguza bidhaa hiyo kwa usahihi.

Unaweza kumlinda mtoto wako asidanganywe na matangazo ya biashara kwa njia gani? Kwanza, “unahitaji kutumia wakati kumweleza mtoto wako kwamba thamani ya mtu haipimwi kwa aina ya viatu [au nguo] anavyovaa,” linasema Rewia. Mfundishe mtoto wako kwamba anaweza kuwa na furaha bila kuwa na vifaa vya kuchezea vya karibuni zaidi. Pili, wazazi wenyewe wanapaswa kujua jinsi matangazo ya biashara yanavyoweza kuwaathiri watoto wao. Jambo muhimu ni kwamba hatupaswi “kuruhusu matangazo ya biashara yatuamulie kinachomfaa mtoto wetu,” anapendekeza Wąs.

Mwishowe, wazazi wote wanaweza kunufaishwa na shauri la Biblia. Mtume Yohana aliandika: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.”—1 Yohana 2:15, 16.

Je, hukubali kwamba matangazo mengi ya biashara yanavutia “tamaa ya macho” na kuwachochea wadogo kwa wakubwa watake “kujionyesha mali [yao] maishani”? Kwa kupendeza, mtume Yohana aliendelea kutoa shauri lake hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17.

Wazazi ambao kwa ukawaida wanatumia wakati mwingi wakizungumza na watoto wao mambo yenye kujenga wanaweza kukazia kanuni za kimungu na viwango vinavyofaa ndani yao. (Kumbukumbu la Torati 6:5-7) Kisha watoto hawatadanganywa kwa urahisi na matangazo ya biashara yenye udanganyifu ya ulimwengu huu ambayo yamekusudiwa kuwafanya wawashinikize wazazi wao wawanunulie vitu.