Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Tupo Hapa

Sababu Tupo Hapa

Sababu Tupo Hapa

BIBLIA inaonyesha kwamba Muumba wetu, Yehova Mungu, hatendi bila kusudi. Kwa mfano, fikiria uumbaji wake wa mzunguko wa maji unaoendeleza uhai duniani. Biblia inaufafanua hivi kwa usahihi: “Mito yote hutiririkia baharini, lakini bahari kamwe haijai; huko ambako mito hutiririkia ndiko huko inakotoka tena.”—Mhubiri 1:7, Biblia Habari Njema.

Biblia inalinganisha kutegemeka kwa ahadi za Mungu na mzunguko ambao umefafanuliwa. Kama tunavyojua leo, nguvu za jua hufanya maji yavukizwe kutoka katika bahari na maziwa, na baadaye yanarudi duniani kama mvua. Yehova anaelekeza fikira kwenye mzunguko huo na kueleza: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:10, 11.

Maji safi hurudi duniani kutoka kwenye mawingu ili kuendeleza uhai duniani. Vivyo hivyo, ‘neno linalotoka katika kinywa cha Mungu’ linaweza kuendeleza maisha yetu ya kiroho. Ni kama Yesu Kristo alivyoeleza: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.”—Mathayo 4:4.

Kula chakula cha kiroho kinachotoka kwa Mungu hutuwezesha kupatanisha maisha yetu na kusudi lake. Lakini, kabla ya kufanya hivyo, tunahitaji kuelewa kusudi la Mungu ni nini. Kwa mfano, kwa nini Mungu aliumba dunia? Na kusudi lake kwa dunia linatuhusu jinsi gani? Acheni tuone.

Kusudi la Mungu kwa Dunia

Kwa sababu Mungu anataka wanadamu wawe na maisha bora, alimweka mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, katika Edeni, bustani iliyokuwa paradiso. Kisha akawaagiza wazae, akiwaambia: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.”—Mwanzo 1:26-28; 2:8, 9, 15.

Tunaweza kukata kauli gani kutokana na maagizo hayo? Je, si wazi kwamba Mungu alitaka dunia yote igeuzwe kuwa paradiso kwa ajili ya wanadamu? Neno lake linasema: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.”Zaburi 115:16.

Hata hivyo, ili wanadamu wapate utimizo wa kusudi la Mungu la kuishi duniani milele kwa furaha, wangehitaji kumheshimu Yehova kwa kumtii. Lakini je, Adamu alifanya hivyo? La, alifanya dhambi kwa kutomtii Mungu. Hilo lilikuwa na matokeo gani? Wazao wote wa Adamu, kutia ndani sisi sote leo, tumerithi dhambi na kifo, kama vile Biblia inavyosema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Kwa sababu hiyo, wanadamu wote wanakufa na dunia haijageuzwa kuwa paradiso. Basi, je, inawezekana kwamba kusudi la Mungu kwa dunia limebadilika?

La, kwa sababu Mungu alisema: “Neno langu linalotoka katika kinywa changu . . . halitarudi kwangu bila matokeo” bali “litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” Isitoshe, Mungu aliahidi: “Kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya.” (Isaya 45:18; 46:10; 55:11) Na ni mapenzi ya Mungu, naam, ni kusudi lake, kwamba dunia yote iwe paradiso iliyojaa wanadamu wanaomtumikia milele kwa furaha, kama alivyokusudia mwanzoni.—Zaburi 37:29; Isaya 35:5, 6; 65:21-24; Ufunuo 21:3, 4.

Kusudi la Mungu Litatimia Jinsi Gani?

Yehova alionyesha hekima na upendo wake usio na kifani kwa kufanya maandalizi ili wanadamu wawekwe huru kutoka kwa dhambi waliyorithi na matokeo yake ambayo ni kutokamilika na kifo. Alifanya hivyo kwa kufanya mwana azaliwe ambaye hangerithi dhambi ambayo wote wamerithi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Uandalizi huo unaitwa fidia ambayo ilitolewa ili wanadamu wanaostahili wapate uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Waefeso 1:7; 1 Timotheo 2:5, 6) Fidia ilitolewa jinsi gani?

Malaika wa Yehova, Gabrieli, alimwambia mwanamke bikira aliyeitwa Maria kwamba angezaa mtoto kimuujiza, akamfafanulia jinsi angemzaa mtoto huyo hata ingawa ‘hakuwa akilala na mwanamume.’ Muujiza ambao Mungu alifanya ulikuwa kuhamisha uhai wa Mwana wake mzaliwa wa kwanza kutoka mbinguni hadi katika yai lililo katika tumbo la uzazi la Maria. Hivyo, akachukua mimba kupitia utendaji wa roho takatifu ya Mungu.—Luka 1:26-35.

Yesu alizaliwa miezi tisa hivi baadaye akiwa mwanadamu mkamilifu, kama tu mwanadamu wa kwanza, Adamu. Baada ya kuwa mtu mzima, alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu katika kifo cha kidhabihu. Kwa kufanya hivyo, Yesu alikuwa ‘Adamu wa pili’ na hivyo akaweka msingi kwa ajili ya wote ambao ni waaminifu kwa Mungu waweze kukombolewa kutoka kwa dhambi na kifo.—1 Wakorintho 15:45, 47.

Kwa kweli tunapaswa kuchochewa na upendo mwingi ambao Mungu ametuonyesha! Biblia inasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Swali ni, Tutaonyesha jinsi gani kwamba tunathamini upendo wa Mungu? Je, hatupaswi kuthamini zawadi yake? Fikiria mifano ya watu ambao wameonyesha uthamini wao.

Furahia Maisha Yenye Kusudi

Denise, aliyetajwa katika makala inayotangulia, aliona kwamba kuheshimu Mungu kwa kufuata sheria na maagizo yake kulifanya maisha yake yawe na kusudi. Anasema hivi: “Nilijifunza kutoka kwa Biblia kwamba licha ya kuwa na kusudi kwa ajili ya wanadamu litakalotimizwa wakati ujao, Mungu anataka waabudu wake wafanye kazi fulani hususa. Siwezi kuwazia maisha yenye kuridhisha kuliko kutumia uhuru wa kuchagua ambao amenipa ili nimtukuze kwa kuishi kulingana na kusudi lake.”

Tunaweza kufanya hivyo kwa kujifunza mapenzi ya Mungu na kuyafanya. Ni kweli, hatujapata manufaa kamili za dhabihu ya fidia ambayo itatuwezesha tufurahie ukamilifu wa kibinadamu katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. Lakini kwa sasa, ni muhimu tutosheleze tamaa yetu ya kiroho ambayo Mungu ameweka ndani ya kila mmoja wetu.

Njaa ya kiroho ya Dave, aliyetajwa katika makala ya kwanza, ilitoshelezwa. Alipata majibu ya maswali yake kuhusu kusudi la uhai. “Nikitazama nyuma,” anasema, “ninaona kwamba maisha yangu kabla ya kujifunza kusudi la Mungu yalikuwa yamejaa jitihada zisizo na mafanikio. Wakati huo sikujua kwamba kukosa uradhi kulitokana na uhitaji wangu mwingi wa kiroho. Sasa sijihisi hivyo tena. Ninaelewa kwa nini nipo hapa na ninachopaswa kufanya maishani.”

Naam, tofauti na mawazo ya wanadamu wasio wakamilifu, maoni ya Mungu kuhusu kusudi la uhai kama yalivyoandikwa katika Biblia yanaridhisha kwelikweli. Tupo hapa kwa sababu ya kusudi la Yehova la kutuumba, yaani, tulitukuze jina lake, tuwe na uhusiano mzuri naye, na hivyo tutosheleze uhitaji wetu wa kiroho. Leo na kwa umilele wote, tunaweza kufurahia kutimizwa kwa maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—Zaburi 144:15.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

TATIZO LA KUTESEKA

Kuteseka kumesemwa kuwa ndilo tatizo kubwa zaidi linalofanya tusielewe kwa nini tupo hapa. Viktor Frankl alisema: “Ikiwa kuna kusudi la uhai, basi lazima kuwe na sababu inayotufanya tuteseke. Kuteseka ni sehemu ya maisha isiyoweza kuondolewa, kama tu majaliwa na kifo visivyoweza kuondolewa.”

Biblia inaeleza sababu inayotufanya tuteseke na kufa. Hatupaswi kumlaumu Mungu. Badala yake, tunapatwa na hali hizo kwa sababu ya uamuzi mbaya ambao wenzi wawili wa kwanza walifanya kwa kutomtegemea Muumba wao. Wazao wao wote wamerithi mwelekeo huo wa kufanya dhambi na ndiyo sababu wanadamu wanateseka.

Ingawa kuelewa kwa nini tupo hapa hakusuluhishi matatizo yote tunayokabili maishani, kunatupa msingi wa kukabiliana nayo. Pia, tunapata tumaini kwa ajili ya wakati ujao, wakati ambapo Mungu ataondoa kuteseka na kifo milele.

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 7]

Biblia inalinganisha kutegemeka kwa ahadi za Mungu na mzunguko wa maji wenye kustaajabisha

[Mchoro]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mvua

Uvukizaji

Uvukizaji

Maziwa, Mto

Bahari

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba hatimaye dunia itakuwa paradiso iliyojaa watu wenye furaha na afya?

[Picha katika ukurasa wa 9]

‘Siwezi kuwazia maisha yenye kuridhisha kuliko kutumia uhuru wangu wa kuchagua kumtumikia Mungu.’—Denise