Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Biblia

Yesu Alizaliwa Wakati Gani?

Yesu Alizaliwa Wakati Gani?

“TAREHE hususa ambayo Kristo alizaliwa haijulikani,” inasema Encyclopedia of Early Christianity. Hata hivyo, mamilioni ya watu wanaodai kuwa Wakristo ulimwenguni pote husherehekea kuzaliwa kwa Yesu Desemba (Mwezi wa 12) 25. Lakini tarehe hiyo haionekani mahali popote katika Biblia. Je, kweli Yesu alizaliwa Desemba?

Ingawa Biblia haitupi tarehe hususa ya kuzaliwa kwa Yesu, inatoa uthibitisho wa kwamba hakuzaliwa Desemba. Mbali na Biblia kuna uthibitisho mwingine unaoweza kutusaidia kujua kwa nini Desemba 25 ilichukuliwa kuwa tarehe ya kusherehekea kuzaliwa kwake.

Kwa Nini Hakuzaliwa Desemba?

Yesu alizaliwa katika jiji la Bethlehemu huko Yudea. Injili ya Luka inaripoti hivi: “Katika nchi hiyo kulikuwako pia wachungaji wakiishi nje, wakichunga makundi yao usiku.” (Luka 2:4-8) Hilo lilikuwa jambo la kawaida. “Kwa miezi mingi mifugo ilikuwa katika maeneo yaliyo wazi,” kinasema kitabu Daily Life in the Time of Jesus. Lakini je, wachungaji wangekuwa nje na mifugo yao katika usiku wenye baridi wa Desemba? Kitabu hicho kinasema: “Katika majira ya baridi kali walikuwa ndani ya nyumba; na hilo peke yake linafanya tarehe ya Krismasi, katika majira ya baridi kali, kuwa si sahihi kwa sababu Injili inasema wachungaji walikuwa mashambani.”

Mkataa huo unapatana na habari nyingine katika Injili ya Luka: “Katika siku hizo Kaisari Augusto alitoa amri kwamba dunia yote inayokaliwa iandikishwe; (uandikisho huu wa kwanza ulitendeka wakati Kirenio alipokuwa gavana wa Siria;) na watu wote wakaanza kusafiri kwenda kuandikishwa, kila mmoja kwenye jiji lake mwenyewe.”—Luka 2:1-3.

Huenda Augusto aliamuru uandikisho huo ili atumie habari hiyo kuhusiana na kutoza ushuru na kuandikisha watu jeshini. Ili atii amri hiyo, Maria, aliandamana na mume wake, Yosefu, katika safari ya [kilomita 150] hivi kutoka Nazareti kwenda Bethlehemu ingawa alikuwa karibu kuzaa. Sasa hebu fikiria kuhusu jambo hilo. Je, inapatana na akili kwamba Augusto, mtawala ambaye hakujihusisha sana na serikali za wilaya, angewaamuru watu ambao walikuwa tayari kuzusha ghasia dhidi ya utawala wa Waroma wafunge safari hiyo ndefu katika majira ya baridi kali?

Ni muhimu kujua kwamba wanahistoria na wasomi wengi wa Biblia wanapinga kwamba Yesu alizaliwa Desemba 25. Bila shaka, utapata habari hiyo katika ensaiklopedia mbalimbali. Our Sunday Visitor’s Catholic Encyclopedia inasema: “Watu wengi wanakubaliana kwamba Yesu hakuzaliwa Desemba 25.”

Biblia inatoa uthibitisho wa kwamba Yesu hakuzaliwa Desemba

Kwa Nini Walichagua Desemba 25?

Mamia ya miaka baada ya kifo cha Yesu, Desemba 25 ilichaguliwa kuwa tarehe ya kuzaliwa kwake. Kwa nini? Wanahistoria wengi wanaamini kwamba wakati ambao sasa Krismasi husherehekewa ulikuwa wakati wa sherehe za kipagani.

Kwa mfano, Encyclopædia Britannica inasema: “Ufafanuzi mmoja ulioenea wa chanzo cha tarehe hii ni kwamba sikukuu ya dies solis invicti nati (‘siku ya kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa’) iliyosherehekewa Desemba 25, ilifanywa kuwa ya Kikristo. Hiyo ilikuwa sikukuu maarufu ya Milki ya Roma iliyosherehekewa wakati jua linapochomoza katika majira ya baridi kali kama ishara ya mwisho wa majira hayo na mwanzo wa majira ya kupukutika na kiangazi.”

Kitabu The Encyclopedia Americana kinatuambia hivi: “Sababu ya kutenga Desemba 25 kuwa Krismasi haijulikani, lakini inaaminiwa kwamba siku hiyo ilichaguliwa ili ilingane na sherehe ya kipagani iliyofanyika jua lilipochomoza katika majira ya baridi kali, wakati mchana ulianza kuwa mrefu, ili kusherehekea ‘kuzaliwa tena kwa jua.’ . . . Satanalia ya Kiroma (sherehe ya Saturn, mungu wa kilimo, na nguvu mpya za jua), pia ilifanyika wakati huo.” Kwa kawaida, sherehe hizo zilitia ndani mwenendo mpotovu kingono ambapo watu walisherehekea bila kujizuia na kwa kelele nyingi sana. Tabia hizohizo huonekana katika sherehe nyingi za Krismasi leo.

Jinsi ya Kumheshimu Kristo

Watu fulani wanahisi kwamba hata ingawa hatujui tarehe hususa, ni lazima Wakristo washerehekee kuzaliwa kwa Yesu. Kwa maoni yao, sherehe hiyo inapofanywa kwa njia inayofaa ni njia nzuri ya kumheshimu Kristo.

Kwa kweli, kuzaliwa kwa Yesu ni tukio muhimu katika Biblia. Biblia inasema kwamba Yesu alipozaliwa, umati wa malaika ulitokea ghafula na kumsifu Mungu kwa shangwe wakisema: “Utukufu katika vilele vilivyo juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.” (Luka 2:13, 14) Hata hivyo, ni muhimu kutambua kwamba hakuna mahali popote katika Biblia ambapo inasemekana kwamba siku ya kuzaliwa kwa Yesu inapaswa kusherehekewa. Kinyume na hilo, kuna amri hususa ya kuadhimisha kifo chake. Mashahidi wa Yehova hufanya hivyo mara moja kwa mwaka. (Luka 22:19) Hiyo ni njia moja ya kumheshimu Yesu.

Usiku wake wa mwisho akiwa mwanadamu, Yesu alisema: “Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru ninyi.” (Yohana 15:14) Pia alisema: “Ikiwa mnanipenda, mtazishika amri zangu.” (Yohana 14:15) Ni wazi kwamba hakuna njia bora zaidi ya kumheshimu Yesu Kristo kuliko kujifunza na kufuata mafundisho yake.