Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulipata Kile Ambacho Tulikuwa Tukitafuta

Tulipata Kile Ambacho Tulikuwa Tukitafuta

Tulipata Kile Ambacho Tulikuwa Tukitafuta

Limesimuliwa na Bert Tallman

Ninakumbuka vizuri sana maisha yangu nikiwa kijana katika eneo lililotengewa Wenyeji wa Asili wa Amerika. Jamii yetu inaitwa Blood nayo ni sehemu ya kabila kubwa la Blackfoot huko Alberta, Kanada. Tuliishi karibu na Milima ya Rocky ya Kanada na ziwa maridadi linaloitwa Louise.

FAMILIA yetu ina wavulana saba na wasichana wawili. Sisi watoto tulipenda sana kwenda kwa nyanya yetu. Alifanya kazi kwa bidii na alitufundisha utamaduni wa mababu wa kabila la Blackfoot. Tulijifunza jinsi ya kukusanya beri za mwituni, kutayarisha vyakula vya kienyeji, na kulima. Mara nyingi nilienda kuwinda na kuvua pamoja na babu na baba yangu. Tuliwinda kulungu, mbawala, na kongoni ili tupate chakula na ngozi. Wazazi wetu walifanya kazi kwa bidii na walijaribu sana kutuandalia makao mazuri. Maisha yangu katika eneo hilo yalikuwa yenye kufurahisha.

Hata hivyo, mnamo 1963 mambo yalibadilika nyanya yangu alipokufa. Nikiwa na umri wa miaka mitano, jambo hilo lilifanya nichanganyikiwe. Hakuna jambo lolote nililosikia lililonifariji. Hata nilipokuwa na umri mdogo hivyo, nilijiuliza, ‘Ikiwa kuna Muumba, yuko wapi? Kwa nini watu wanakufa?’ Nyakati nyingine ningeanza kulia kwa sababu ya kukata tamaa. Wazazi wangu waliponiuliza ni kwa nini ninalia, niliwaambia kwamba nina maumivu.

Uhusiano na Wazungu

Kabla ya nyanya yangu kufa, hatukukutana sana na wazungu. Wakati wowote tulipowaona, nilisikia watu wakisema mambo kama: “Huyu ni mzungu mwingine mwovu, mwenye pupa, asiye na hisia zozote. Hawa si watu wazuri.” Nilionywa kwamba kuna wazungu wachache sana wazuri na hawawezi kuaminiwa. Ingawa nilitaka sana kuwafahamu, nilijihadhari sana kwa sababu mara nyingi wazungu katika eneo letu walitudhihaki na kutuambia mambo yasiyofaa.

Muda mfupi baada ya nyanya yangu kufa, wazazi wangu walianza kutumia kileo vibaya, na hilo lilifanya maisha yangu wakati huo yawe yenye kusikitisha sana. Nilipokuwa na umri wa miaka minane, wahubiri wawili wa dini ya Mormon walianza kuja nyumbani kwetu. Walionekana kama watu wazuri. Wazazi wangu walikubali pendekezo lao la kunihusisha katika mradi fulani wa dini yao. Nilielewa kwamba mradi huo ulikusudiwa kuwafunza watoto wa wenyeji utamaduni mwingine kwa kuwafanya waishi na familia ya wazungu. Ni wazi kwamba kwa sababu ya hali zao, wazazi wangu walifikiri kwamba ni bora kwangu kuishi na familia nyingine. Nilishtuka na kuvunjika moyo kwa kuwa nilikuwa nimewasikia wazazi wangu wakisema kwamba wazungu hawawezi kuaminiwa. Sikutaka kwenda na nilijaribu kukataa. Mwishowe, nilikubali wazazi wangu waliponihakikishia kwamba kaka yangu angeenda pamoja nami.

Hata hivyo, tulipofika huko Vancouver, British Columbia, mimi na ndugu yangu tulitenganishwa nami nikapelekwa kilomita 100 hivi kutoka huko! Nilihuzunika sana. Ingawa familia niliyoishi nayo ilikuwa ya watu wazuri, nilishuka moyo na kuogopa sana. Nilirudi nyumbani miezi kumi hivi baadaye.

Narudi Nyumbani kwa Wazazi

Nilifurahi kurudi nyumbani, hata ingawa hali hazikuwa zimebadilika sana. Nilipokuwa na umri wa miaka 12 hivi, wazazi wangu waliacha kutumia kileo. Hilo liliboresha hali, lakini tayari nilikuwa ninaishi maisha yasiyofaa kwani nilikuwa nimeanza kutumia dawa za kulevya na kileo. Wazazi wangu walinitia moyo nifuatilie mambo mengine kama vile kujihusisha katika mashindano ya kupanda fahali na farasi wa mwituni, jambo nililofurahia sana. Mtu mwoga hangeweza kushiriki mashindano hayo. Nilijifunza kupanda fahali wa mwituni anayeruka-ruka kwa kishindo kwa muda wa zaidi ya sekunde nane bila kuangushwa, huku nikishikilia kamba iliyofungiliwa tumboni mwa fahali huyo kwa mkono mmoja tu.

Nilipokuwa kijana, wazee wa kabila letu walinifundisha kuhusu dini ya Wenyeji wa Asili wa Amerika. Nilipendezwa sana nayo kwani sikuheshimu dini zilizosemekana kuwa za wazungu. Niliamua kwamba utamaduni wa Blackfoot ulichochea fadhili na haki ambazo hazipatikani katika dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo. Nilifurahia kuwa kati ya Wenyeji wa Asili wa Amerika, nikifurahia ucheshi na uhusiano wa karibu kati ya familia na marafiki.

Karibu na wakati huo, nilijifunza jinsi Wenyeji wa Asili wa Amerika walivyotendewa isivyo haki kwa karne nyingi. Niliambiwa kwamba wazungu walikuwa wamesambaza ugonjwa na kuua chanzo chetu cha kikuu cha chakula, yaani, nyati. Kwa kweli, inaripotiwa kwamba Kanali R. I. Dodge wa jeshi la Marekani alisikiwa akisema: “Mwueni kila nyati mnayeweza. Mkimwua nyati mmoja, mnamwua mwenyeji mmoja.” Niligundua kwamba mtazamo huo uliwakatisha tamaa wenyeji wa kabila la Blackfoot na kuwafanya wajihisi hawajiwezi.

Isitoshe, viongozi fulani wa serikali pamoja na viongozi wa kidini walikuwa wamejitahidi kubadili utamaduni wa Wenyeji wa Asili wa Amerika na kuwageuza kwa sababu waliwaona kuwa washamba. Waliamini kwamba utamaduni, mafundisho, tabia, lugha, na mambo mengine ya Wenyeji wa Asili wa Amerika yalipaswa kubadilishwa ili waishi kama wazungu. Nchini Kanada, watoto wa wenyeji walitendewa vibaya katika shule za kidini. Ili kukabiliana na hali hiyo, wengine walijiua, au wakajihusisha na dawa za kulevya, au jeuri, na hayo ni matatizo yanayoendelea hadi leo katika maeneo yaliyotengewa wenyeji hao.

Ili kuepuka matatizo hayo, baadhi ya Wenyeji waliamua kuacha utamaduni wa Blackfoot. Waliamua kuzungumza na watoto wao Kiingereza badala ya lugha ya Blackfoot na walijaribu kuiga baadhi ya tabia za wazungu. Hata hivyo, badala ya kupendwa wengi walidhihakiwa, si tu na wazungu fulani, bali pia na Wenyeji wenzao ambao walisema kwamba walionekana kama wenyeji lakini walitenda kama wazungu.

Ilisikitisha kuwaona Wenyeji wakiteseka katika njia nyingi sana. Nilitamani kuona watu katika eneo letu na wengine kotekote nchini Kanada na Marekani wakiishi chini ya hali bora zaidi.

Nilitamani Kupata Majibu

Nilipokuwa kijana wa umri wa zaidi ya miaka 15 nilihisi kwamba singewahi kukubaliwa na nilihisi sifai. Kwa sababu hiyo nilianza kuwa na chuki. Hata nilianza kuwachukia wazungu. Lakini wazazi na shangazi yangu walinionya kuhusu kufungia hisia zisizofaa za chuki na kulipiza kisasi; badala yake walinitia moyo nisamehe na kuonyesha upendo na niwapuuze watu waliokuwa na ubaguzi. Baadaye niligundua kwamba shauri hilo linapatana na kanuni za Biblia. Isitoshe, nilitamani kupata majibu ya maswali yaliyokuwa yamenisumbua tangu utotoni. Pia nilianza kujiuliza kwa nini tuko duniani na kwa nini kuna ukosefu wa haki. Sikuelewa kwa nini wanadamu wanaishi kwa muda mfupi tu na kisha kufa. Nilichanganyikiwa kabisa.

Kila mara Mashahidi wa Yehova walipotutembelea, nilitumwa niongee nao. Niliwaheshimu kwa sababu hawakuwa na ubaguzi. Ingawa sikujua jinsi ya kupanga maswali yangu kwa njia inayofaa, nilifurahia kuzungumza nao. Ninakumbuka siku moja tulipotembelewa na John Brewster na Harry Callihoo, ambaye ni Shahidi wa kabila la Blackfoot. Tulizungumza kwa muda mrefu huku tukitembea uwandani. Walinipa kitabu, lakini kilipotea baada ya mimi kusoma nusu yake.

Kushiriki Mashindano ya Fahali

Niliwaomba wazee katika eneo letu mawaidha. Ingawa nilithamini mashauri yao yenye hekima, sikuwahi kupata majibu yenye kuridhisha kwa maswali kuhusu maisha. Nilipokuwa na umri wa miaka 16 hivi, nilitoka nyumbani na nilishiriki kabisa katika mashindano ya fahali. Sherehe zilizofanywa baada ya mashindano kwa kawaida zilihusisha kunywa kileo kupita kiasi na kutumia dawa za kulevya. Dhamiri yangu ilinisumbua kwa sababu nilijua kwamba hayo yalikuwa matendo mabaya na nilihisi kwamba Mungu hakukubali njia yangu ya maisha. Mara nyingi, nilimwomba Muumba msaada wa kufanya yaliyo sawa na kupata majibu ya maswali ambayo bado yalinisumbua.

Mnamo 1978, nilipokuwa Calgary, nilikutana na mwanamke Mwenyeji wa Asili wa Amerika ambaye anaitwa Rose. Wazazi wake walitoka makabila mawili tofauti; mmoja kabila la Blackfoot na mwingine kabila la Cree. Tulikuwa na mapendezi yaleyale na ningeweza kuwasiliana naye waziwazi. Tulipendana na tukaoana mnamo 1979. Tulipata binti anayeitwa Carma na mwana anayeitwa Jared. Rose amekuwa mke mshikamanifu na amenitegemeza, na pia amekuwa mama mzuri. Siku moja tulipokuwa tukimtembelea kaka yangu, nilipata kitabu chenye kichwa Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. * Mambo niliyosoma yalinipendeza na yalipatana na akili. Lakini nilipoanza tu kuhisi kwamba ninaelewa ujumbe wa Biblia, nikafikia sehemu ya kitabu ambapo kurasa zilikuwa zimeraruliwa. Mimi na Rose tulijitahidi sana kutafuta kurasa hizo, lakini hatukufaulu. Hata hivyo, niliendelea kusali ili nipate msaada.

Namtembelea Kasisi

Mnamo 1984, Rose alizaa mtoto wetu wa tatu, binti yetu mrembo sana anayeitwa Kayla. Hata hivyo, Kayla alikufa miezi miwili tu baadaye kutokana na tatizo fulani la moyo. Tulihuzunika sana, na sikujua jinsi ya kumfariji Rose. Alinisadikisha twende kumwona kasisi Mkatoliki katika eneo letu ili tufarijiwe na kupata majibu ya maswali yetu.

Tulimwuliza sababu iliyofanya binti yetu mdogo afe na mahali alipokuwa ameenda. Alituambia kwamba Mungu alimchukua Kayla kwa sababu alihitaji malaika mwingine. Nilijiambia, ‘Kwa nini Mungu anahitaji kuchukua binti yetu awe malaika ikiwa yeye ndiye Muumba Mweza-Yote? Mtoto mdogo asiye na uwezo anaweza kumsaidia jinsi gani?’ Kasisi huyo hakufungua Biblia hata mara moja. Tuliondoka tukihisi hatujiwezi.

Sala Ilitutegemeza

Jumatatu (Siku ya 1) moja asubuhi mwishoni mwa Novemba (Mwezi wa 11) 1984, nilisali kwa muda mrefu, nikimsihi Mungu anisaidie niwe mtu mzuri zaidi, nielewe mambo yaliyokuwa yakitukia, na kuelewa kusudi la uhai. Asubuhi hiyohiyo Mashahidi wa Yehova wawili, Diana Bellemy na Karen Scott, walibisha mlango wetu. Walikuwa wanyoofu na wenye fadhili na walikuwa na hamu ya kunieleza ujumbe waliokuwa nao. Nilisikiliza, wakanipa Biblia na kitabu chenye kichwa Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya, * na nikakubali Diana arudi akiwa na mume wake Darryl, baadaye juma hilo.

Walipoondoka ndipo nilipotambua kwamba ziara yao ilikuwa jibu kwa sala niliyotoa. Nilisisimuka sana hivi kwamba nilitembea-tembea ndani ya nyumba nikisubiri Rose arudi kutoka kazini ili nimweleze yaliyotokea. Nilishangaa Rose aliponiambia kwamba alikuwa amesali usiku uliotangulia na kumwomba Mungu amsaidie kupata dini ya kweli. Ijumaa (Siku ya 5) hiyo, tulianza kujifunza Biblia. Baadaye tuligundua kwamba siku ambayo Karen na Diana walitutembelea, hawakupata nyumba walizokuwa wameelekezwa kuhubiri. Hata hivyo, walipoona nyumba yetu, walichochewa kututembelea.

Hatimaye Maswali Yangu Yajibiwa!

Watu katika familia yetu na marafiki walishangaa na walitupinga tulipoanza kujifunza Biblia. Kisha wakatushinikiza kwa kutuambia tulikuwa tukipoteza maisha yetu na hatukuwa tukitumia vipawa na uwezo wetu kikamili. Lakini tuliazimia kwamba hatutampa kisogo Rafiki yetu mpya, Muumba wetu, Yehova. Tulikuwa tumepata kitu chenye thamani, yaani, kweli za ajabu na siri takatifu zinazopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. (Mathayo 13:52) Mnamo Desemba 1985 mimi na Rose tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Sasa watu wetu wa ukoo wanawaheshimu sana Mashahidi wa Yehova, kwa kuwa wameona mabadiliko mazuri maishani mwetu tangu tulipobatizwa.

Naam, nilipata nilichokuwa nikitafuta! Biblia inajibu maswali muhimu kwa njia rahisi sana na inayopatana na akili. Niliridhika nilipojifunza kuhusu kusudi la uhai, kwa nini tunakufa, na ahadi ya Mungu kwamba tutakutana tena na binti yetu Kayla na kumwona akikua katika mazingira makamilifu. (Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:4) Baada ya muda, nilijifunza pia kwamba hatupaswi kutumia miili yetu vibaya, kutoheshimu uhai, au kuchochea mashindano. (Wagalatia 5:26) Ingawa uamuzi niliopaswa kufanya ulikuwa mgumu, niliamua kuacha kushiriki jambo lolote linalohusiana na mashindano ya fahali ili nimpendeze Mungu.

Ujuzi sahihi wa Biblia umetuweka huru kutokana na ushirikina ambao umewanasa Wenyeji wengi wa Asili wa Amerika, kama vile imani ya kwamba bundi anapotua karibu na nyumba au mbwa anapolia anaweza kusababisha kifo cha mshiriki wa familia. Hatuogopi tena kwamba roho zisizoonekana katika viumbe au vitu visivyo na uhai zitatudhuru. (Zaburi 56:4; Yohana 8:32) Sasa tunathamini uumbaji wa ajabu wa Yehova. Nina marafiki kutoka mataifa mengi ambao ninawaita ndugu na dada, nao wanatuona kuwa sawa na kuwa watumishi wenzi wa Mungu. (Matendo 10:34, 35) Wengi wao wanajitahidi kujifunza utamaduni na imani za Wenyeji wa Asili wa Amerika kutia ndani lugha ya Blackfoot, ili waweze kuhubiri ujumbe wa Biblia katika njia inayopendeza zaidi.

Familia yetu inaishi kwenye eneo lililotengewa jamii ya Blood, kusini mwa Alberta, ambako tuna shamba dogo. Bado tunafurahia utamaduni wa kienyeji, kutia ndani chakula, muziki, na dansi za kitamaduni. Hatushiriki katika dansi za kitamaduni zinazohusisha watu wengi ambazo pia zinaitwa powwow, lakini tunafurahia kuzitazama inapofaa. Pia nimejaribu kuwafundisha watoto wetu kuhusu utamaduni wao na lugha ya Blackfoot. Wenyeji wengi wa Asili wa Amerika wajulikana kwa sifa zao nzuri kama vile, fadhili, unyenyekevu, na upendo kuelekea watu wa ukoo na marafiki. Pia, wanajulikana kwa ukarimu wao na kwa kuwaheshimu watu wengine kutia ndani watu kutoka malezi tofauti. Bado ninathamini na kuvutiwa na sifa hizo.

Furaha yetu kubwa zaidi inatokana na kutumia wakati na mali zetu kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova na kumpenda. Mwana wetu, Jared, ni mjitoleaji katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova karibu na Toronto. Nina pendeleo la kutumika kama mzee katika Kutaniko la Macleod, na mimi, Rose, na Carma ni mapainia wa kawaida, au waeneza-injili wa wakati wote. Ni shangwe kuhubiri katika lugha yetu ya Blackfoot. Inachangamsha moyo kuwaona wengine wakikubali kweli kumhusu Muumba na makusudi yake.

Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Ukimtafuta, ataacha umpate.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Ninashukuru kwamba ametimiza ahadi yake ya kunisaidia mimi na familia yangu kupata kile tulichokuwa tukitafuta.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Sasa hakichapishwi tena.

^ fu. 27 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 13]

‘Ikiwa kuna Muumba, yuko wapi? kwa nini watu wanakufa?’

[Picha katika ukurasa wa 16]

‘Wenyeji wengi wa Asili wa Amerika wanajulikana kwa sifa zao za fadhili na unyenyekevu’

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nyanya yangu alinifundisha utamaduni wa Blackfoot

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nilijihusisha kabisa katika mashindano ya fahali

[Picha katika ukurasa wa 15]

Trakti ya pekee “You Can Trust the Creator” inapatikana katika lugha ya Blackfoot na lugha nyingine

[Picha katika ukurasa wa 15]

Sasa ninapata shangwe kwa kushiriki ujuzi wa Biblia na wengine

[Picha katika ukurasa wa 15]

Leo, nikiwa na familia yangu