Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Vibaya Kuteketeza Maiti?

Je, Ni Vibaya Kuteketeza Maiti?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Vibaya Kuteketeza Maiti?

Watu fulani wanahisi kwamba kuteketeza maiti hadi iwe majivu hakuonyeshi heshima kwa mwili na mtu aliyekufa. Wanasema hivi: ‘Zoea hilo ni la kipagani na kwa sababu hiyo linapaswa kuepukwa na wale wanaodai kumwabudu Mungu.’ Wengine wanaamini kwamba kuteketeza maiti ni njia inayokubalika na kuheshimika ya kushughulikia maiti. Wewe una maoni gani?

KATIKA nyakati za Biblia lilikuwa jambo la kawaida kuwazika wafu. Kwa mfano, Abrahamu alimzika mke wake, Sara, katika pango. Mwili wa Yesu uliwekwa katika kaburi lililokuwa limechimbwa katika mwamba. (Mwanzo 23:9; Mathayo 27:60) Je, Biblia inasema kwamba kuzika ndiyo njia pekee inayokubalika ya kushughulikia maiti? Je, inaonyesha kwamba watumishi wa kale wa Mungu walipinga kuteketezwa kwa maiti?

Je, Kunaonyesha Mtu Hana Kibali cha Mungu?

Inaposomwa kijuujuu, huenda mistari fulani ya Biblia ikaonekana kuonyesha kwamba maiti za watu fulani ambao hawakupata kibali cha Mungu ndizo ziliteketezwa. Kwa mfano, Sheria ya Musa ilisema kwamba ikiwa binti ya kuhani wa Yehova angekuwa kahaba, alipaswa ‘kuteketezwa katika moto’ baada ya kuuawa. (Mambo ya Walawi 20:10; 21:9) Vivyo hivyo, Waisraeli waliposhindwa na watu wa Ai kwa sababu ya kutotii kwa Akani na familia yake, Waisraeli wenzao waliipiga familia hiyo kwa mawe kisha “wakawateketeza kwa moto.” (Yoshua 7:25) Wasomi fulani wamependekeza kwamba hivyo ndivyo watu waliokufa kifo cha aibu walivyotendewa na kwamba kuteketeza maiti kuliwanyima watenda-dhambi maziko yenye heshima.

Isitoshe, Mfalme Yosia alipojaribu kuondoa ibada ya sanamu kutoka Yuda, alivunja makaburi ya makuhani waliokuwa wakitoa dhabihu kwa Baali na kuteketeza mifupa yao juu ya madhabahu zao. (2 Mambo ya Nyakati 34:4, 5) Je, mifano hiyo inaonyesha kwamba wale ambao maiti zao zinateketezwa hawana kibali cha Mungu? Hapana, kama inavyoonyeshwa na simulizi lingine la Biblia.

Wafilisti walipomshinda Mfalme Sauli wa Israeli vitani, bila heshima walifunga maiti yake na ya wanawe watatu, kwenye ukuta wa jiji la Beth-shani. Hata hivyo, Waisraeli waliokuwa wakiishi Yabesh-gileadi, waliposikia jinsi maiti hizo zilivyotendewa bila heshima, waliziondoa na kuziteketeza, kisha wakazika mifupa yao. (1 Samweli 31:2, 8-13) Huenda ikaonekana kwamba simulizi hilo linathibitisha kwamba haifai kuteketeza maiti kwani Sauli pia alikuwa mwovu; alipigana na Daudi, mtiwa-mafuta wa Yehova, na alikufa bila kibali cha Mungu.

Hata hivyo, ona ni nani mwingine aliyekufa pamoja na Sauli. Mmoja wa wanawe aliyeitwa Yonathani. Mwili wake pia ulitendewa vivyo hivyo. Hakuwa mtu mbaya. Badala yake, Yonathani alikuwa rafiki wa karibu wa Daudi na alimuunga mkono. Waisraeli walitambua jambo hili kumhusu Yonathani: “Alifanya kazi na Mungu.” (1 Samweli 14:45) Daudi aliposikia jinsi wanaume wa Yabesh-gileadi walivyotenda, aliwasifu na kuwashukuru kwa maneno haya: “Mbarikiwe na Yehova, kwa kuwa mmeonyesha hizi fadhili zenye upendo kwa bwana wenu, kwa Sauli.” Ni wazi kwamba kuteketezwa kwa maiti ya Sauli na Yonathani hakukumsumbua Daudi.—2 Samweli 2:4-6.

Hakuwezi Kuzuia Mtu Afufuliwe

Biblia inafundisha waziwazi kwamba Yehova Mungu atawafufua watu wengi ambao sasa wamekufa. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 5:28, 29) Kikitoa unabii kuhusu wakati ambapo wafu watakuwa hai tena, kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinasema: “Bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake.” (Ufunuo 20:13) Ili kutimiza hilo, Mungu Mweza-Yote ana uwezo wa kumfufua mtu iwe maiti yake ilizikwa, iliteketezwa, ilizama baharini, ililiwa na wanyama-mwitu, au hata ililipuliwa na bomu la atomu.

Biblia haitoi mwelekezo hususa juu ya jinsi maiti inavyopaswa kushughulikiwa. Yehova hashutumu kuteketezwa kwa maiti. Hata hivyo, ni wazi kwamba maziko yanapaswa kuwa yenye kuheshimika.

Hata hivyo, mtu anapaswa kufikiria maoni ya watu katika jamii kuhusu desturi za maziko. Wale wanaoishi kupatana na kanuni za Biblia hawapaswi kufanya jambo ambalo litawaudhi majirani wao bila sababu. Pia haingefaa kujihusisha katika zoea ambalo huenda linaonyesha kwamba mtu anaamini mafundisho ya dini ya uwongo, kama vile nafsi inaendelea kuishi baada ya mwili kufa. Hata hivyo, jinsi maiti itakavyoshughulikiwa ni uamuzi wa mtu mwenyewe au wa familia yake.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Ni mtumishi gani mwaminifu anayetajwa katika Biblia ambaye mwili wake uliteketezwa?—1 Samweli 31:2, 12.

▪ Daudi aliwatendea jinsi gani wanaume walioteketeza maiti ya Sauli?—2 Samweli 2:4-6.

▪ Ni nini kinachoonyesha kwamba kuteketezwa kwa maiti hakuwezi kumfanya mtu asifufuliwe?—Ufunuo 20:13.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Biblia haitoi mwelekezo hususa juu ya jinsi maiti inavyopaswa kushughulikiwa