Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu changu kidogo cha rangi ya waridi

Kitabu changu kidogo cha rangi ya waridi

Kitabu changu kidogo cha rangi ya waridi

Limesimuliwa na Cynthia Newell

NILIPOKUWA na umri wa miaka saba, msichana mmoja tuliyesafiri pamoja katika basi la shule huko Shreveport, Louisiana, Marekani, alinionyesha kitabu kidogo cha rangi ya waridi kinachoitwa Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. Aliniambia angenipa kitabu hicho kwa gharama ya senti 50 tu za Marekani. Kwa hiyo, alikuja kwetu na tukahesabu peni 50 pamoja.

Nilipenda sana kitabu hicho. Punde tu baada ya kukipokea, nilikuwa mgonjwa na nikalazwa hospitalini. Ili kunifariji, baba yangu alinisomea kitabu hicho nilichokipenda. Hata hivyo, nilipoendelea kukua sikusoma sana kitabu hicho, kwa kuwa kilikuwa kitabu cha watoto. Kitabu hicho kilinifundisha mambo muhimu, lakini nilihitaji uelewevu wenye kina. Niliamua kuhudhuria kanisa tofauti kila juma nikitafuta majibu ya maswali yangu ya Biblia. Hata hivyo, sikupata majibu yenye kuridhisha.

Kufikia wakati nilipoanza shule ya upili, dini haikuwa muhimu sana kwangu ingawa bado nilitamani kupata ujuzi wa Biblia na nilisoma Biblia yangu kwa ukawaida. Siku moja niliona kwamba mwanafunzi mwenzangu hakusema kiapo cha uaminifu. Nilimuuliza kuhusu jambo hilo na akanijibu, “Tayari mimi ni mwaminifu kwa Yehova na hivyo siwezi kuwa mwaminifu kwa mtu mwingine.” Jibu lake lilipatana sana na akili. Lakini nilijiuliza, ‘Huyo Yehova ni nani?’

Kila swali nililouliza, mwanafunzi mwenzangu alijibu kwa kutumia Biblia. Nilijiuliza: ‘Alijifunza wapi mambo hayo yote? Tuna umri mmoja, lakini yeye anaijua Biblia sana!’ Alijibu hivi: “Mimi hujifunza Biblia kwenye Jumba la Ufalme.” Nilikubali haraka aliponialika kuhudhuria mikutano Jumapili. Nilikuwa nimeenda kwa kila kanisa katika mji huo lakini kwa sababu fulani sikuwa nimefika kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Jumapili hiyo niligundua mara moja kwamba nimepata mahali ambako kweli ya Biblia inafundishwa.

Baada ya mikutano, nilienda kwenye dawati ya vitabu na kwenye safu ya juu nikaona kitabu changu kidogo cha rangi ya waridi! Miaka kumi ilikuwa imepita tangu nilipopata kitabu hicho kutoka kwa msichana katika basi la shule, na hata nilikuwa nimesahau ni nani aliyenipa. Lakini sasa nilikumbuka kwamba ni msichana yuleyule, aliyeitwa Nancy, ambaye alikuwa amenialika mikutanoni siku hiyo!

Baada ya hapo, nilianza kujifunza Biblia kila juma na nikafanya maendeleo haraka. Kwa kuwa nilikuwa nimejifunza mambo mengi sana kutoka katika kitabu changu kidogo, nilielewa haraka mambo niliyojifunza kutoka kwa Biblia. Punde si punde, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mwaka wa 1985 nikiwa na umri wa miaka 18. Wakati huo, Nancy alikuwa amehamia Florida na hatukuwasiliana tena.

Baada ya miaka michache niliolewa. Mnamo 1991, mimi na mume wangu Drew, tulianza utumishi wa wakati wote tukiwa mapainia katika mji mdogo mashariki mwa Texas. Lakini sikuwa na habari zozote kumhusu Nancy. Kisha usiku mmoja nilipokuwa nikisoma gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1992, (1/12/1992) nilisema hivi kwa sauti: “Ndiye huyu Nancy! Ndiye huyu Nancy!” Alikuwa kwenye picha ya wale waliohitimu Shule ya Gileadi. Yeye na mume wake, Nick Simonelli, walikuwa wamepewa mgawo wa kwenda Ekuado, Amerika Kusini.

Mnamo 2006, mimi na mume wangu tulituma maombi ya kuwa wajitoleaji katika miradi ya ujenzi wa kimataifa ya Mashahidi wa Yehova. Tulifurahi kama nini kujua kwamba mgawo wetu wa kwanza ulikuwa mradi wa upanuzi wa ofisi ya tawi ya Ekuado! Siku ya kwanza tulipowasili kwenye ofisi ya tawi, nilimwona Nancy akiingia mlangoni! Alikuwa ameamua kuja kwenye ofisi ya tawi siku hiyo. Tulionana tena na kukumbatiana miaka 32 tangu nilipopokea kitabu changu kidogo cha rangi ya waridi! Ninamshukuru sana Yehova kwa kitabu hicho na kwa msichana mdogo aliyenipa!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

VIMEBADILI MAISHA YA MAMILIONI YA WATU

Mnamo 2003, baada ya kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu kuwa kimetumiwa kwa miaka 32, kitabu kilichorekebishwa kilichapishwa. Kina kichwa Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Kufikia sasa, jumla ya nakala milioni 65 ya vitabu hivyo viwili kuhusu mafundisho ya Yesu vimechapishwa katika lugha zaidi ya 100. Unaweza kumwomba Shahidi wa Yehova katika eneo lenu kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Picha ndogo: Tulipofahamiana tukiwa watoto

Cynthia

Nancy

Nyuma: Tukiwa kwenye ofisi ya tawi ya Ekuado miaka mingi baadaye