Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwalimu Abadili Maoni Yake

Mwalimu Abadili Maoni Yake

Mwalimu Abadili Maoni Yake

▪ Miaka michache iliyopita, mwalimu mmoja huko Batumi, nchini Georgia, aliwaomba wanafunzi wake wataje zile Amri Kumi. Mwalimu huyo alishangaa mmoja wa wanafunzi wake anayeitwa Anna alipozitaja kwa usahihi. Pia alijibu maswali mengine ya Biblia kwa njia yenye kuvutia. Akiwa amestaajabu, mwalimu alimwuliza alijifunza wapi mambo hayo yote. Anna alipomwambia kwamba alikuwa amejifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, mwalimu huyo alimkatiza na kusema kwamba watu hao ni washupavu wa kidini.

Pindi moja, mwalimu waliwaambia wanafunzi waandike insha kuhusu maisha ya watu wa Georgia na matatizo ambayo wanakabili. Mwishoni mwa insha yake, Anna aliandika: “Jitihada zozote za wanadamu za kuleta mabadiliko makubwa katika jamii hazitafanikiwa kwa kuwa, Yeremia 10:23 inasema hivi: ‘Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.’ Matatizo yote yatatatuliwa tu na Ufalme wa Mungu.”

Siku iliyofuata, mwalimu alisifu insha ya Anna mbele ya darasa na kusema: “Nilifurahia insha ya pekee ya Anna ambayo aliandika kwa maneno yake mwenyewe. Katika insha hiyo alieleza jinsi hali za ulimwengu zinavyoweza kubadilishwa.” Mwalimu huyo alivutiwa pia na mwenendo wa Anna, na akamsifu mbele ya darasa lote kwa sababu ya tabia zake nzuri na mavazi yenye kiasi.

Mashahidi wa Yehova walipomtembelea mwalimu huyo nyumbani kwake, aliwaambia kwamba zamani aliwaona Mashahidi kuwa washupavu wa kidini lakini sasa amebadili maoni yake kwa sababu ya mwanafunzi wake Anna. Mnamo 2007, mwalimu huyo alihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo pamoja na Mashahidi wa Yehova na akasikiliza programu kwa makini.

Baada ya Ukumbusho, mwalimu wa Anna alikiri kwamba anavutiwa sana na jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyojua sana Biblia. Sasa Mashahidi wanajifunza naye Biblia kwa ukawaida. Kama mwalimu huyo, bila shaka wewe pia unapendezwa kuchunguza ni kwa nini watu wengine wana imani na tabia tofauti na zako. Mbona usimwombe mmoja wa Mashahidi wa Yehova ajifunze nawe Biblia nyumbani kwako bila malipo?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Anna akiandika insha yake