Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Nina Kazi Nyingi Sana!’

‘Nina Kazi Nyingi Sana!’

‘Nina Kazi Nyingi Sana!’

WANYANYUAJI wa vyuma wa Olimpiki hawajaribu kuweka rekodi mpya kila siku. Wao hufanya mazoezi kwa ukawaida wakitumia vyuma vidogo na kwa njia hiyo wanapata nguvu za kunyanyua vyuma vizito. Ikiwa wangejilazimisha kunyanyua vyuma vizito sana kila wakati, wangejiumiza misuli na viungo na huenda wangeacha kushiriki katika mashindano.

Vivyo hivyo, huenda wewe ukiwa mwanafunzi unajitahidi sana shuleni. Na unapopewa migawo migumu au unapojiandaa kwa ajili ya mitihani, unatia bidii hata zaidi. * Lakini namna gani ikiwa kila siku ungekuwa tu ukifanya kazi za shule na migawo mingine? Huenda ikawa vigumu kwako kula vizuri au hata kulala vya kutosha. Mwishowe huenda ukawa mgonjwa kwa sababu ya mfadhaiko mwingi wenye kuendelea. Huenda ukawa unahisi hivyo sasa. *

Kazi ya Shule Isiyoisha

“Kazi za shule zinaongezeka na kuwa ngumu zaidi ninapoenda darasa linalofuata. Inachukua muda mwingi zaidi kuzimaliza,” anasema Hiroko, * mwanafunzi mwenye umri wa miaka 15 nchini Japani. “Nina mambo mengine mengi ninayotaka kufanya, lakini lazima niwe nimemaliza kazi ya shule siku inayofuata. Nyakati nyingine mimi huwa na wasiwasi.” Svetlana, mwenye umri wa miaka 14 kutoka Urusi anasema hivi kuhusu kazi ya shuleni anayopewa: “Inazidi kuwa vigumu zaidi kumaliza kazi yangu ya shuleni. Kila mwaka idadi ya masomo inaongezeka na walimu wananipa migawo mingi zaidi. Isitoshe, kila mwalimu huona somo lake kuwa muhimu zaidi. Ni vigumu kuwa na usawaziko na kufanya kila jambo.”

Kwa nini walimu wanawapa wanafunzi kazi nyingi sana za shuleni? Gilberto, mwenye umri wa miaka 18 kutoka Brazili anasema: “Walimu wanasema kwamba wanatutayarisha ili tuweze kupata kazi katika ulimwengu usio na kazi za kutosha.” Hata ingawa huu ndio ukweli wa mambo, huenda ukahisi umelemewa na kazi nyingi unayopewa shuleni. Pengine unaweza kupunguza mfadhaiko kwa kubadili maoni yako kuhusu kazi ya shuleni na kuchukua hatua zinazofaa ili ufanye mambo kwa utaratibu.

Ona kazi nyingi unazopewa shuleni kuwa mazoezi unayohitaji ili ufanikiwe utakapokuwa mtu mzima. Ingawa huenda ikaonekana kuwa kazi za shuleni hazitawahi kuisha, miaka unayotumia shuleni itapita upesi kuliko unavyofikiria. Unapoanza kufanya kazi ili ujiruzuku, utafurahi kwamba ulimaliza migawo hiyo migumu. ‘Utaona mema kwa sababu ya kazi ngumu’ uliyofanya shuleni.—Mhubiri 2:24.

Unaweza kupunguza mfadhaiko mwingi kwa kuwa na bidii na mwenye utaratibu. (Ona sanduku  “Njia za Kupunguza Mfadhaiko.”) Unapokuwa na zoea la kufanya kazi za shule kwa wakati na kwa uangalifu, huenda walimu wako watakuamini na watataka kukusaidia. Wazia kwamba una uhusiano kama huo pamoja na mmoja wa walimu wako. Ikiwa jambo lisilotazamiwa lingetokea na umwambie kimbele kwamba hungeweza kumaliza mgawo fulani kwa wakati, je, hufikiri kwamba mwalimu wako angekupa muda zaidi wa kufanya kazi hiyo? Danieli, mtumishi wa Mungu “alikuwa mwenye kutegemeka wala haukupatikana ndani yake uzembe wowote wala jambo lolote lenye ufisadi.” Bidii ya Danieli katika kazi yake ilifanya asifiwe na kuaminiwa na mfalme. (Danieli 6:4) Ukimwiga Danieli unapofanya migawo yako ya shule, huenda mwalimu akakuonyesha ufikirio zaidi.

Je, kusikiliza kwa makini darasani, kufanya kazi za shule, na kumaliza miradi ya shule kwa wakati kutakuondolea mfadhaiko shuleni? Hapana, lakini huenda baadhi ya mfadhaiko ukatokana na tamaa yako ya kufaulu. Badala ya kujaribu kutafuta njia ya kuepuka kufanya kazi za shule, huenda ukataka hasa kujifunza na kufaidika kutokana na masomo yako.

Mfadhaiko wa aina hiyo ni mzuri na una faida. Hata hivyo, huenda ukakabili mfadhaiko unaodhuru na usio wa lazima.

Utendaji wa Baada ya Shule Unawapa Shughuli Nyingi

Mfikirie mtu ambaye huendesha gari lake kwa kasi sana na anapofika kwenye ishara anasimama ghafula. Kisha anakanyaga mafuta na kuondoka kwa kasi huku magurudumu yakizunguka kwa kasi. Dereva huyo mwenye kichaa atafanya nini gari lake? Kuna uwezekano mkubwa kwamba ataharibu injini na sehemu nyingine za gari hilo. Lakini hata kabla ya kufanya hivyo, anaweza kuliharibu katika aksidenti mbaya.

Kwa njia hiyohiyo, wanafunzi wengi hufanya kazi nyingi sana ya kimwili na kiakili, kabla na baada ya shule. Katika kitabu chake Doing School, Denise Clark Pope aliandika hivi kuhusu wanafunzi kadhaa ambao alikutana nao: “Shughuli zao za shule zilianza mapema sana, karibu saa moja au mbili kabla ya watu wengi wazima kuamka na kuanza kazi, na mara nyingi siku yao iliisha usiku sana baada ya mazoezi ya mpira, mazoezi ya kucheza dansi, mikutano ya vyama vya wanafunzi, kazi ya kuajiriwa ya muda, na kumaliza kazi za shule.”

Wanafunzi wanapokuwa na mambo mengi hivyo ya kufanya kila siku, yaelekea watajiletea matatizo. Kwa sababu ya kupatwa na mfadhaiko mwingi, wanaweza kupatwa na magonjwa ya tumbo na kuumwa na kichwa. Kwa sababu ya kuchoka kila wakati, mfumo wao wa kinga hudhoofika na hivyo wanaweza kuwa wagonjwa. Kisha wanashindwa kufanya mambo waliyokuwa wakifanya na inakuwa vigumu kupata tena nguvu zao. Je, umepatwa na jambo kama hilo?

Ni vizuri kujitahidi kufikia malengo yanayofaa, lakini hata kama una nguvu sana, kuna mipaka kuhusu mambo unayoweza kufanya kwa siku moja. Biblia inatoa mashauri haya yanayofaa: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Neno “usawaziko” linaelezwa kuwa “kutopita kiasi” na “kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi mazuri.” Mtu mwenye usawaziko hufanya maamuzi ambayo hayamdhuru yeye au wengine. Anajionyesha kuwa mtu mkomavu, na hilo ni jambo muhimu sana katika ulimwengu wa leo wenye msukosuko. Kwa hiyo, ili kudumisha afya nzuri, uwe na usawaziko kwa kuepuka utendaji usio wa maana sana.

Kufuatia Utajiri

Hata hivyo, kwa vijana fulani, badala ya kuwasaidia kufikia malengo yao, ni kana kwamba kuwa na usawaziko huwa ni kikwazo. Wanafunzi kama hao huamini kwamba siri ya kufanikiwa ni kuwa na kazi yenye mshahara mnono na utajiri unaotokana na kazi kama hiyo. Pope aliona kwamba baadhi ya vijana aliokutana nao walikuwa na maoni kama hayo. Alisema hivi: “Wanafunzi hao walitamani kulala kwa muda mrefu zaidi na kuboresha afya yao, lakini ratiba yao yenye utendaji mwingi unaotia ndani shule, familia, na kufanya kazi hakukuwaruhusu kufanya mabadiliko waliyotaka. Vivyo hivyo, walitamani kutumia muda mwingi zaidi pamoja na marafiki, kufanya mambo mengine, au kupumzika kwa siku kadhaa lakini wengi waliamini kwamba hawawezi kufanya mambo hayo na bado waendelee kupata maksi za juu. Walitambua kwamba walihitaji kufanya uamuzi na kwa maoni yao, kufanikiwa maishani kulikuwa muhimu zaidi kuliko kupata furaha sasa.”

Ni vizuri kwa wanafunzi kama hao wenye bidii kufikiria maneno haya ya mtu mmoja mwenye hekima: “Je, mtu atafaidi nini akiupata utajiri wote wa ulimwengu na hali amepoteza maisha yake? Au, mtu atatoa kitu gani kiwe badala ya maisha yake?” (Mathayo 16:26, Biblia Habari Njema) Kwa maneno hayo Yesu Kristo alionya kwamba miradi yoyote tunayojitahidi kufikia katika ulimwengu huu haina faida kwa sababu inaweza kutudhuru kimwili, kihisia, na kiroho.

Katika kitabu chake The Price of Privilege, mwanasaikolojia Madeline Levine aliandika kwamba “kuwa na pesa, elimu, mamlaka, umashuhuri, na vitu vya kimwili hakumsaidii mtu asikose furaha au asipatwe na matatizo ya kihisia.” Pope, aliyetajwa awali, alisema hivi: “Mimi huwaona watoto na wazazi wengi wakijaribu kufikia viwango vya juu sana walivyojiwekea kwa sababu wanaamini wakifikia viwango hivyo watafanikiwa.” Aliongeza hivi: “Tunapaswa kujitahidi kuwa na afya kiakili, kimwili, na kutambua mambo yaliyo muhimu maishani.”

Kuna mambo muhimu zaidi kuliko pesa. Mambo hayo yanatia ndani kuwa na afya nzuri ya kihisia, kimwili, dhamiri nzuri, na urafiki pamoja na Muumba wetu. Hizo ni zawadi zenye thamani sana kutoka kwa Mungu. Ukizipoteza kwa sababu ya kufuatilia umashuhuri au utajiri, huenda usizipate tena. Ukiwa na hilo akilini, ona kile ambacho Yesu alifundisha: “Heri wanaojiona kuwa maskini mbele ya Mungu, maana Utawala wa mbinguni ni wao.”—Mathayo 5:3, The New Testament in Kiswahili with Catholic Notes.

Vijana wengi wamekubali kweli hiyo. Ingawa wanajitahidi sana shuleni, wao wanatambua kwamba kufaulu katika masomo na kupata utajiri hakuwezi kuwapa furaha ya kudumu. Wanatambua kwamba kufuatia miradi kama hiyo kunawaletea mfadhaiko usiohitajika. Wanafunzi hao wamejifunza kwamba kumaliza ‘umaskini wao mbele za Mungu’ ndio msingi wa kuwa na furaha wakati ujao. Wachapishaji wa gazeti hili au Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukuonyesha jinsi unavyoweza kuwa na furaha unapomaliza umaskini wako mbele za Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kwa wanafunzi ambao hawafanyi vizuri au hawajitahidi sana, ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Ningeweza Kufanya Vizuri Zaidi Shuleni?” katika Amkeni! la Machi 22, 1998 (22/3/1998), ukurasa wa 20-22.

^ fu. 3 Unaweza kupata habari zaidi katika makala yenye kichwa “Vijana Wanauliza . . . Nifanye Nini Kuhusu Kazi Nyingi ya Shule ya Kufanyia Nyumbani?” la Amkeni! la Aprili 8, 1993 (8/4/1993), ukurasa wa 13-15.

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Hata kama una nguvu sana, kuna mipaka kuhusu mambo unayoweza kufanya kwa siku moja

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Kupata ujuzi juu ya Muumba wako ndiyo elimu bora zaidi unayoweza kujipatia

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

 NJIA ZA KUPUNGUZA MFADHAIKO

❑ Je, wewe hutumia wakati mwingi ukitafuta kitu kilichofichika katikati ya karatasi nyingi na vitabu vingi? Watu fulani wanahitaji kusaidiwa kuwa na utaratibu zaidi. Usiabike kuwaomba wengine mapendekezo.

❑ Je, wewe huahirisha mambo? Jaribu kumaliza mgawo mapema. Utashangaa kuona jinsi utakavyokuwa mwenye utulivu na uradhi na hilo litakuchochea uache kuahirisha kazi za shule.

❑ Je, mara nyingi wewe hujikuta ukiota ndoto za mchana ukiwa darasani? Jaribu kufanya hivi kwa mwezi mmoja: Sikiliza kwa makini mazungumzo ya darasani na uandike mambo makuu ili uyapitie baadaye. Huenda ukashangazwa sana kuona jinsi kazi ya shule itakavyokuwa rahisi. Matokeo hayo mazuri yatapunguza mfadhaiko unaopata shuleni.

❑ Je, umechagua masomo yatakayokufanya utimize mengi kuliko wanafunzi wenzako lakini yanayohitaji wakati na jitihada nyingi zaidi? Je, ni lazima uchague masomo hayo? Zungumza na wazazi wako. Tafuta maoni ya mtu aliye na mtazamo uliosawazika kuhusu elimu. Huenda ukagundua kwamba masomo hayo ya ziada hayatakusaidia sana kumaliza shule haraka.

[Picha katika ukurasa wa 6]

UKUTA WA ULINZI WA KUWAZIA

“Vitu vyenye thamani vya tajiri ni mji wake wenye nguvu, navyo ni kama ukuta wa ulinzi katika mawazo yake.” (Methali 18:11) Zamani, watu walitegemea kuta ndefu ili kujilinda dhidi ya mashambulizi. Lakini hebu wazia unaishi katika jiji lililozungukwa na ukuta wa kuwaziwa tu. Hata ujaribu kujisadikisha kadiri gani, ukuta huo hauwezi kukulinda dhidi ya maadui wako.

Kama watu wanaoishi katika eneo lililo wazi hivyo, vijana wanaofuatilia utajiri watatamaushwa. Je, wewe ni mzazi? Ni vizuri kumsaidia mtoto wako kuepuka mtego wa kufuatilia vitu vya kimwili na kuishi katika jiji kama hilo lenye ukuta wa kuwaziwa.

Kweli za Biblia zifuatazo zinaweza kukusaidia kuzungumza na mwana au binti yako:

▪ Utajiri mwingi hutokeza matatizo mengi kuliko kuyatatua. “Wingi alio nao tajiri haumruhusu kulala.”Mhubiri 5:12; 1 Timotheo 6:9, 10.

▪ Mtu akiwa na mipango mizuri hahitaji kuwa na utajiri ili awe na furaha. “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.”Methali 21:5; Luka 14:28.

▪ Mapato ya kadiri yanayotimiza mahitaji ya mtu humfanya aridhike. “Usinipe umaskini wala utajiri.”Methali 30:8. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 43 Habari zaidi kuhusu mtego wa kufuatilia vitu vya kimwili inaweza kupatikana katika Amkeni! la Aprili 8, 2003, ukurasa wa 20-21.

[Picha katika ukurasa wa 7]

USIONE kazi za shule kuwa tatizo bali kuwa mazoezi kwa ajili ya kazi

[Picha katika ukurasa wa 7]

Huwezi kutimiza mengi ukifanya mambo mengi kupita kiasi