Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilitoroka Mauaji na Kupata Uzima

Nilitoroka Mauaji na Kupata Uzima

Nilitoroka Mauaji na Kupata Uzima

Limesimuliwa na Sam Tan

Mimi na familia yangu pamoja na Wakambodia wengine 2,000 hivi tulikuwa tukitoroka nyumbani kwetu tulipofika kwenye mto unaopakana na Thailand. Tulipanda mashua ndogo zilizokuwa zikiwavusha watu upande wa usalama. Mashua ya mwisho ilipokuwa tu ikiondoka, askari wa Khmer Rouge walifika na kuanza kutufyatulia risasi.

TULIJIHISI tumetulia tulipovuka na kuingia Thailand bila kuumia. Kila mtu alifurahi isipokuwa sisi, kwa kuwa baba yangu na mjomba wangu hawakuwapo, walikuwa wamechukuliwa miezi michache mapema. Mama aliketi chini na kuanza kulia. Lakini kabla ya kuendelea na hadithi yangu, acha nikueleze kidogo kuhusu malezi yangu.

Maisha Yangu Nikiwa Mbudha

Nikiwa mmoja kati ya watoto watatu nilizaliwa huko Kambodia mnamo 1960. Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, mimi na wazazi wangu tuliamua kwamba niende nikatumikie katika hekalu la Budha, jambo lililokuwa la kawaida kwa wavulana. Mtawa huanza kazi saa kumi na mbili hivi asubuhi, anapoondoka hekaluni kwenda nyumba kwa nyumba kuomba chakula. Niliona ikiwa vigumu kuwaomba wenye nyumba fulani chakula kwa sababu kwa kweli walikuwa maskini. Baadaye, sisi watawa vijana tulipika chakula hicho na kuwapa watawa wenye umri mkubwa. Tulikula chakula chetu baadaye.

Saa kumi na mbili jioni, watawa wenye umri mkubwa walikutana ili kusali wakitumia lugha ambayo ni wachache sana wangeelewa. Baada ya miaka miwili, nilihitimu na kuwa mtawa mdogo na nikapewa baadhi ya mapendeleo ya watawa wenye umri mkubwa. Niliruhusiwa pia kusali pamoja nao. Muda huo wote, nilifikiri kwamba dini ya Budha ndiyo iliyokuwa dini pekee ulimwenguni.

Natoroka Kambodia

Nilichoka kuishi hekaluni na nikarudi nyumbani nilipokuwa na umri wa miaka 14. Muda mfupi baadaye, kiongozi wa kisiasa aliyeitwa Pol Pot alianza kutawala. Wanamgambo wake wa Khmer Rouge, waliotawala kuanzia 1975 hadi 1979, waliwalazimisha watu wote waondoke majijini na kurudi vijijini ili kufanya Kambodia iwe nchi ya Kikomunisti. Familia yetu pia ilihamishwa. Baadaye, askari hao wa Pol Pot walimchukua baba na mjomba wangu. Hatukuwaona tena. Kwa kweli, wakati wa utawala wa Khmer Rouge, karibu Wakambodia milioni 1.7 waliuawa katika vile vilivyoitwa viwanja vya uchinjaji au walikufa kwa sababu ya magonjwa, njaa, au kufanyishwa kazi kupita kiasi.

Kama ilivyotajwa mwanzoni, tukiwa watu 2,000, hali hizo zilitufanya tufunge safari hatari ya siku tatu kupitia milimani hadi kwenye mpaka wa Thailand. Sote kutia ndani mtoto mvulana aliyezaliwa njiani tulifika tukiwa salama. Wengi wetu tulikuwa na pesa lakini tulizitupa kwa sababu pesa za Kambodia hazikuwa na thamani yoyote nchini Thailand wakati huo.

Maisha Nchini Thailand

Familia yetu iliishi na watu wa ukoo huko Thailand na nikaanza biashara ya uvuvi. Mara nyingi tukitumia mashua yetu tuliingia kwenye maji ya Kambodia, ambako kulikuwa na samaki wengi, na pia kulikuwa na mashua zilizoshika doria za wanajeshi wa Khmer Rouge. Kama wangetushika, tungepoteza mashua yetu na tungeuawa. Kwa kweli, mara mbili tuliponea chupuchupu. Hata hivyo, wengine hawakuokoka, kutia ndani jirani yangu ambaye alikamatwa na kukatwa kichwa. Ingawa kifo chake kilinihuzunisha sana, bado niliendelea kuvua samaki karibu na pwani ya Kambodia ili familia yetu isife njaa.

Ili kutimiza mahitaji yangu na ya familia yetu, niliamua kwenda kwenye kambi ya wakimbizi nchini Thailand ili niweze kutuma maombi ya kuhamia nchi nyingine, na ikiwa maombi yangu yangefanikiwa, ningeitumia familia yetu pesa kutoka nchi hiyo. Nilipowaambia watu wangu wa ukoo kuhusu jambo hilo, walinipinga sana. Lakini nilikuwa nimefanya uamuzi wangu.

Wageni waliozungumza Kiingereza ambao nilikutana nao katika kambi ya wakimbizi walidai kuwa Wakristo. Jambo hilo lilivunja imani yangu kwamba dini ya Budha ndiyo iliyokuwa dini pekee ulimwenguni. Mimi na rafiki yangu mpya Teng Hann, tulianza kushirikiana na “Wakristo” hao ambao walitupa Biblia na chakula. Niliishi katika kambi hiyo kwa mwaka mmoja na nikatuma maombi ya kuhamia New Zealand.

Maisha Mapya Huko New Zealand

Maombi yangu yalikubaliwa mnamo Mei (Mwezi wa 5) 1979, na muda mfupi baada ya hapo nilikuwa katika kambi ya wakimbizi huko Auckland. Mtu fulani mwenye fadhili alipanga niende kwenye jiji la Wellington nikafanye kazi katika kiwanda fulani. Nilipofika huko, nilifanya kazi kwa bidii na nikatuma pesa nyumbani kama nilivyoahidi.

Ili nielewe Ukristo, nilianza kwenda kwenye makanisa mawili ya Kiprotestanti. Hata hivyo, hawakuzungumzia sana Biblia. Kwa sababu nilitaka kusali kwa njia inayofaa, rafiki yangu alinifundisha ile Sala ya Bwana. (Mathayo 6:9-13) Lakini, hakuna mtu aliyenielezea sala hiyo inamaanisha nini hasa. Kwa hiyo, kama vile nilivyosali nikiwa Mbudha, nilirudia-rudia sala hiyo bila kuelewa nilichokuwa nikisema.

Ndoa Yenye Matatizo

Nilioa mwaka wa 1981. Mwaka mmoja hivi baadaye, mimi na mke wangu tulibatizwa na kasisi fulani kwa kunyunyiziwa maji kichwani. Kufikia wakati huo, nilikuwa na kazi mbili, nyumba nzuri, na maisha yenye starehe, mambo ambayo sikuwa nayo huko Kambodia. Hata hivyo, sikuwa na furaha. Ndoa yetu ilipatwa na matatizo, na ingawa tulienda kanisani hilo halikusaidia. Tabia yangu iliongeza matatizo kwa kuwa nilikuwa nikicheza kamari, kuvuta sigara, kunywa pombe kupita kiasi, na kulala na wanawake wengine. Hata hivyo, dhamiri yangu ilinisumbua na sikudhani ningeenda mbinguni, ambako niliambiwa kwamba watu wote wazuri wataenda wakifa.

Mnamo 1987, niliwatumia mama na dada yangu pesa ili wahamie New Zealand, na wakaishi nasi kwa muda fulani. Na walipoondoka, niliondoka pamoja nao, na tukiwa watatu tukahamia Auckland.

Mwishowe Najifunza Biblia

Siku moja nilipokuwa nikitoka kwa rafiki yangu, nilikutana na wanaume wawili waliokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba. Mmoja wao aliyeitwa Bill, aliniuliza, “Unatarajia kwenda wapi ukifa?” “Mbinguni,” nikajibu. Kisha akanionyesha katika Biblia kwamba ni watu 144,000 peke yao watakaoenda mbinguni kutawala wakiwa wafalme juu ya dunia. Pia aliniambia kwamba dunia itakaliwa na mamilioni ya wanadamu wanaomwogopa Mungu na itafanywa kuwa paradiso. (Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 4; 21:3, 4) Mwanzoni, fundisho hilo lilinikasirisha sana kwa kuwa lilipingana na mambo niliyokuwa nimefundishwa awali. Hata hivyo, moyoni mwangu nilivutiwa sana kuona jinsi wanaume hao walivyojua Biblia na jinsi walivyokuwa watulivu. Kwa kweli, nilisikitika kwamba sikuwauliza wao ni washiriki wa dini gani.

Majuma machache baadaye, nilimtembelea rafiki yangu ambaye watoto wake walikuwa wanajifunza Biblia na wenzi wa ndoa Dick na Stephanie. Walitumia broshua Furahia Milele Maisha Duniani! Nilianza kuisoma broshua hiyo na nikaona kwamba ilisema kweli. Niliambiwa kwamba wenzi hao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Ndipo nikatambua kwamba wale wanaume wawili niliokutana nao awali walikuwa Mashahidi kwa kuwa yale waliyosema yalipatana na yale niliyosoma katika broshua ile.

Kwa kuwa nilitaka kujifunza mengi, niliwaalika Dick na Stephanie kwangu na nikawauliza maswali mengi kuhusu Biblia. Baadaye, Stephanie aliniuliza ikiwa ninajua jina la Mungu. Akanionyesha Zaburi 83:18, ambayo inasema: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Andiko hilo lilinigusa sana moyo na nikaanza kujifunza Biblia kwa ukawaida. Msichana Mlaotia tuliyekuwa tukiishi pamoja, aliyeitwa La, alianza kujifunza Biblia pia. Wakati huohuo niliwatumia ndugu yangu na mke wake pesa ili waje New Zealand. Baada ya kuwasili New Zealand, wao pia walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.

Muda mfupi baada ya hapo, mimi na La tuliacha kujifunza Biblia kwa sababu tulihamia Australia ili nikafanye kazi. Ingawa tulikazia fikira kutafuta pesa, tulianza kutamani kuendelea kujifunza Biblia. Kwa hiyo, usiku mmoja tulisali sana kwa Yehova atusaidie kuwapata watu wake.

Sala Yetu Inajibiwa

Siku chache baadaye, nilirudi nyumbani kutoka dukani na kuwakuta Mashahidi wawili mlangoni mwangu. Nilimshukuru Yehova kimyakimya, kisha mimi na La tukaanza tena kujifunza. Pia tulianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Hata hivyo, nilitambua kwamba ili nimpendeze Mungu, nilihitaji kufanya mabadiliko mengi maishani. Hivyo, niliacha mazoea yangu mabaya na nikanyoa nywele zangu ndefu. Rafiki zangu wa zamani walinitania, lakini nilidhibiti hasira yangu. Pia ilibidi nirekebishe mambo fulani kuhusu uhusiano wangu na La, kwa kuwa hatukuwa tumeoana kihalali na sikuwa nimemtaliki mke wangu wa kwanza. Kwa hiyo, mwaka wa 1990, mimi na La tulirudi New Zealand.

Bila kupoteza wakati, tuliwapigia simu Dick na Stephanie. “Sam nilifikiri hatutawahi kukuona tena!” akasema Stephanie. Tulianza tena kujifunza Biblia pamoja nao na mara tu nilipomtaliki mke wangu wa kwanza, mimi na La tulioana tukiwa na dhamiri safi mbele ya Mungu. Tuliishi New Zealand, na tukiwa huko tulibatizwa ili kuonyesha wakfu wetu kwa Mungu. Nikitamani kuwaambia wengine yale niliyokuwa nimejifunza, nilianza kujifunza Biblia na Wakambodia na watu fulani kutoka Thailand waliokuwa wakiishi huko Auckland na maeneo ya karibu.

Tunarudi Australia

Mnamo Mei 1996, mimi na La tulirudi Australia na tukaanza kuishi huko Cairns, kaskazini mwa Queensland. Nikiwa huku nimepata pendeleo la kupanga kazi ya kuwahubiria Wakambodia, Walaotia, na Wathai katika eneo hili.

Namshukuru sana Yehova kwa kunibariki kwa mambo mengi kutia ndani mke wangu mzuri na wavulana wetu watatu, Daniel, Michael, na Benjamin. Pia, nashukuru sana kwamba mama, dada, ndugu, mama mkwe wangu, na Teng Hann, rafiki niliyekutana naye katika kambi ya wakimbizi huko Thailand, wamekubali kweli ya Biblia. Bado mimi na familia yetu tunaomboleza kumpoteza baba na mjomba lakini hatuhuzuniki kupita kiasi. Tunajua kwamba wakati wa ufufuo, Mungu ataondoa kabisa ukosefu wa haki na mambo hayo “hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17; Matendo 24:15.

Miaka michache iliyopita niliona mtu fulani niliyemfahamu kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Alikuwa Bill, mwanamume aliyenihubiria miaka mingi iliyopita. Nilimwuliza, “Unanikumbuka?”

Alijibu, “Ndiyo. Tulikutana huko New Zealand miaka mingi iliyopita na nikakuambia kwamba ni watu 144,000 tu watakaoenda mbinguni.” Ingawa miaka mingi ilikuwa imepita, bado Bill alinikumbuka. Tulikumbatiana na tukakumbushana mambo mengi sasa tukiwa ndugu.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 21]

Background: AFP/Getty Images