Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Risiti Inayopatana na Rekodi ya Biblia

Risiti Inayopatana na Rekodi ya Biblia

Risiti Inayopatana na Rekodi ya Biblia

▪ Katika miaka ya 1870, bamba la udongo lenye upana wa sentimita 5.5 lilichimbuliwa karibu na jiji la kisasa la Baghdad, Iraki. Mnamo 2007, Michael Jursa, profesa katika Chuo Kikuu cha Vienna, Austria, alipata bamba hilo alipokuwa akifanya utafiti katika Jumba la Makumbusho la Uingereza. Jursa alitambua jina la Nebo-sarsekimu (katika Kibabuloni anaitwa Nabu-sharrussu-ukini,), ofisa wa Babiloni anayetajwa katika Biblia kwenye Yeremia 39:3. *

Nebo-sarsekimu alikuwa mmoja wa makamanda wa Mfalme Nebukadneza Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. na kulingana na bamba hilo, anaitwa “towashi mkuu.” Isitoshe, jina la cheo towashi mkuu lilipewa tu mtu mmoja kwa wakati mmoja, na hivyo kutoa uthibitisho wenye nguvu kwamba Sarsekimu anayetajwa katika bamba hilo alikuwa yuleyule anayetajwa katika Biblia.

Bamba hilo pia linataja dhahabu ambayo Nebo-sarsekimu alipeleka kwenye hekalu la Marduki, au Merodaki, mungu mkuu wa Babiloni, ambaye jina lake pia linatajwa katika Biblia. (Yeremia 50:2) Tarehe iliyo kwenye risiti hiyo ni mwaka wa 10, mwezi wa 11, na siku ya 18 ya utawala wa Nebukadneza. Lakini, dhahabu hiyo haikuhusiana na vitu vilivyoporwa Yerusalemu miaka kadhaa baadaye. (2 Wafalme 25:8-10, 13-15) Hata hivyo, “kupata kitu kama bamba hili, ambalo linaonyesha jina la mtu aliyetajwa katika Biblia akitoa malipo katika hekalu la Babiloni na kunukuu tarehe hususa, ni jambo lisilo la kawaida,” anasema Profesa Jursa. Kwa kuwa limeitwa moja kati ya magunduzi muhimu zaidi katika uchimbuzi wa vitu vya kale vya Biblia, bamba hilo “linategemeza wazo la kwamba vitabu vya kihistoria vya Agano la Kale vinatokana na mambo hakika,” linasema gazeti Telegraph la Uingereza.

Hata hivyo, usahihi wa Biblia hautegemei vitu vya kale vilivyochimbuliwa. Uthibitisho wenye nguvu unaweza kupatikana katika Biblia yenyewe, hasa unabii wake. (2 Petro 1:21) Kwa mfano, zaidi ya miaka 100 mapema, Yehova Mungu, akizungumza kupitia nabii Isaya, alitabiri kwamba vitu vyote vyenye thamani vya Yerusalemu “vitachukuliwa kwenda Babiloni.” (Isaya 39:6, 7) Vivyo hivyo, kupitia nabii Yeremia, Mungu alitabiri hivi: “Nitavitoa vitu vyote vya jiji hili [Yerusalemu] vilivyowekwa akiba . . . [nitavitia] mkononi mwa adui zao. Na hakika wao watavipora na . . . kuvipeleka Babiloni.”—Yeremia 20:4, 5.

Nebo-sarsekimu alikuwa mmoja kati ya maadui hao na hivyo yeye pia alijionea utimizo wa unabii wa Biblia. Kwa kweli, iwe alijua au la, alishiriki katika utimizo wa unabii huo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, andiko la Yeremia 39:3 linasema hivi: “Samgar-nebo, Sarsekimu, Rabsarisi,” kupatana na maandishi ya Kiebrania ya Wamasora. Lakini maandishi ya konsonanti ya Kiebrania yanaweza kusomwa hivi: “Samgar, Nebo-sarsekimu yule Rabsarisi [au, Ofisa Mkuu wa Makao ya Kifalme],” ambayo yanapatana na maandishi yaliyo kwenye bamba hilo la udongo.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 11]

Copyright The Trustees of the British Museum