Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Suluhisho Bora Kuliko Dawa

Suluhisho Bora Kuliko Dawa

Suluhisho Bora Kuliko Dawa

LENA, aliyetajwa katika makala ya kwanza, alipokuwa na umri wa miaka 32, “alimezwa na hisia za hatia, kutokuwa na tumaini, na hofu ya kufa,” hasa kwa sababu ya tatizo lake la kutumia dawa vibaya. “Nilitaka kuwa mke na mama mzuri,” akaandika, “lakini kila kitu maishani mwangu na ulimwenguni kilinihuzunisha sana na kunitamausha na sikuwa na sababu ya kuwa mzuri. Na mara chache nilipojaribu, sikufanikiwa.”

Kisha Lena akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Muda si muda, kweli ya Biblia ikamfanya awe na amani ya akili na kitulizo, ambacho alieleza kuwa “hisia bora zaidi ambayo nimewahi kuwa nayo.” Kuelewa kanuni za Biblia na tumaini zuri la wakati ujao kulimchochea kubadili maisha yake na kuacha uraibu wake.

Kanuni za Maisha

Sheria na kanuni zinazopatikana katika Biblia ziliwekwa hasa kwa ajili yetu na Muumba wetu, Yehova Mungu. Zaburi 19:7, 8 inasema hivi: “Sheria ya Yehova ni kamilifu, huirudisha nafsi. . . . Maagizo kutoka kwa Yehova ni manyoofu, huufanya moyo ushangilie; amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae.”

Kwa mfano, 2 Wakorintho 7:1 linatuhimiza “tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.” Lena alichukua maneno hayo kwa uzito na hilo lilimsaidia kuacha zoea hilo baya. Ilikuwa vivyo hivyo kwa Myra, ambaye pia alitajwa katika makala ya kwanza ya gazeti hili. Huenda unakumbuka kwamba alikuwa mraibu wa madawa aliyoandikiwa na daktari kwa ajili ya maumivu ya kichwa. Myra alikabiliana jinsi gani na tatizo lake? Alizungumzia jambo hilo waziwazi na daktari ambaye alimsaidia kupata matibabu mengine. * Zaidi ya hilo, alitafuta msaada katika kutaniko la Kikristo na akatiwa moyo.

Pia Lena na Myra walitafuta msaada kupitia sala. Andiko la Wafilipi 4:6, 7 linasema: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” Mtumishi wa Mungu wa nyakati za kale aliyepata amani hiyo ya akili aliandika kwamba ‘fikira zake zinazofadhaisha zilipokuwa nyingi,’ maneno ya Mungu yenye kutia moyo yalimpa kitulizo, yalimfariji, na kumpa shangwe ya moyoni. (Zaburi 94:19) Maneno kama hayo yenye kufariji yanaweza kupatikana katika Biblia na kutoka kwa washiriki Wakristo, kutia ndani wazee Wakristo wanapotutia moyo na kututegemeza.

Hata hivyo, nyakati nyingine, kwa sababu ya zoea la kutumia dawa vibaya, mtu anaweza kujihisi hafai kabisa. Janice, Mkristo ambaye kwa miaka mingi alikuwa mraibu wa dawa za kitiba aliandika hivi: “Waraibu wanaweza kuliona kuwa jambo gumu kumwomba Yehova msaada kwa sababu ya hali yao mbaya ya kiroho na kwa sababu wanajichukia.” Chini ya hali hizo, ni muhimu sana kutafuta msaada wa Wakristo wakomavu. Upendo na subira wanayoonyesha wanapokutia moyo na sala yao ya imani inaweza ‘kumponya mtu asiyejisikia vizuri.’ (Yakobo 5:15) Bila shaka, ikiwa mraibu ni mtoto, wazazi wanapaswa kumsaidia aache uraibu huo na kuwa na uhusiano mzuri na Yehova ili asirudie tena zoea hilo.

Janice alienda kwenye kituo cha matibabu, akashinda zoea lake, na tangu wakati huo hajatumia tena dawa vibaya. Aliandika hivi: “Mimi humtegemea Yehova anisaidie ninapopata hamu ya kutumia dawa. Sasa nina utulivu na utu wenye kupendeza niliokuwa nao zamani.”

Matatizo Yetu Yote Yatakapokwisha

Hivi karibuni, hakutakuwa na dawa zozote. Hilo litawezekanaje? Ufunuo 21:3, 4 inajibu hivi: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani [kutia ndani matatizo tuliyo nayo sasa] yamepitilia mbali.”

Biblia inalinganisha tumaini la Kikristo na “nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara.” (Waebrania 6:18, 19) Mabaharia wa nyakati za kale walipokumbwa na dhoruba, waliangusha nanga ya meli kwenye bahari. Ikiwa nanga ingeshika sakafu ya bahari, ingeizuia meli hiyo isipeperushwe na dhoruba na kugonga matumbawe hatari au fuo za bahari. Vivyo hivyo, tumaini “hakika na imara” linalopatikana katika Biblia linaweza kutufanya tuwe imara kihisia, kiakili na kiroho wakati majaribu yaliyo kama dhoruba yanapotokea, na bila shaka majaribu kama hayo yatatokea.

Tunakualika uchunguze Biblia na uone jinsi ambavyo mashauri na mafundisho yake yanafaa na ni yenye kutia moyo. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia, nawe hutakatishwa tamaa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Hali zote hazifanani na za Myra. Kwa mfano, huenda watu fulani wakawa wanaugua ugonjwa wenye maumivu mengi na wakapendekezewa na daktari dawa kali za kutuliza maumivu ambazo zinaweza kuwafanya wawe waraibu. Mgonjwa kama huyo hatumii dawa hizo ili alewe wala si mraibu.—Ona Methali 31:6.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua . . . , maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu . . . itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”—Wafilipi 4:6, 7

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

NJIA ZA KUBORESHA AFYA YAKO

Mazoezi yanaweza “kuboresha hisia zako kwa muda na kukusaidia kutuliza mshuko wa moyo,” kinasema kitabu Managing Your Mind—The Mental Fitness Guide. Pia kubadili jinsi unavyokula na mazoea yako, ya kimwili na ya kiakili, kunaweza pia kukusaidia. Fikiria mfano wa Valerie, ambaye alitendewa vibaya alipokuwa mtoto. Alikuwa mraibu wa dawa 12 hivi za kitiba. Hata hivyo, alifaulu kuacha zoea hilo na kuishi maisha ya kawaida. Siri ilikuwa nini?

Badala ya kutazama televisheni na kusoma vitabu vya hadithi vyenye kutiliwa shaka, Valerie alisitawisha ratiba nzuri ya kujifunza Biblia na akatenga wakati wa kusoma vichapo vinavyotegemea Biblia vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kutia ndani gazeti hili. Pia alisali bila kukoma ili apate nguvu kutoka kwa Mungu, akaomba msaada kutoka kwa kutaniko la Kikristo, na akatumia wakati wake mwingi akifanya mambo yanayofaa kama vile kuwaambia wengine kuhusu ujumbe wa Biblia wenye kufariji. Zaidi ya hayo, alibadili sana chakula alichokuwa akila ambacho kilitia ndani vyakula visivyo na lishe. Matokeo yalikuwa kwamba alipona haraka hivi kwamba hata madaktari walishangaa. Hajatumia dawa vibaya kwa miaka mingi sasa. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Ikiwa unatumia dawa kwa ajili ya ugonjwa wa kushuka moyo, wa kubadilika-badilika kwa hisia, au ugonjwa mwingine wa akili, hali yako si sawa na ya Valerie. Kwa hiyo, usifanye mabadiliko yoyote bila kuwasiliana na daktari.