Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi—Walindeni Watoto Wenu!

Wazazi—Walindeni Watoto Wenu!

Wazazi—Walindeni Watoto Wenu!

WAZAZI wanaojali huuliza hivi, “Kwa nini vijana wengi wanatumia dawa za kitiba vibaya?” Sababu za wao kufanya hivyo zinatofautiana. Vijana fulani huzitumia kwa ajili ya msisimuko. Wengine wanataka kujifunza vizuri zaidi au kupunguza wasiwasi. Huenda wengine wakawa wanaugua kimwili au kihisia na wanataka tu kupata nafuu. Kwa kweli, hata watoto wenye umri wa miaka 12 wamekuwa wakitumia dawa vibaya, na huenda wamekuwa wakizipata kupitia mamia ya maelfu ya Tovuti zinazouza dawa hizo, bila kujali ni nani anayezinunua. Wengine wamenunua tembe kutoka kwa watu wanaodai kuwa marafiki. Ikiwa wewe ni mzazi, unaweza kufanya nini ili uwalinde watoto wako?

Hatua moja ni kuzungumza nao waziwazi kuhusu hatari za kutumia dawa iwe zimeagizwa na daktari au zile za kulevya. Hatua nyingine ni kuweka dawa mahali salama, labda hata kuzifungia katika kabati. Fahamu ni dawa gani zilizo nyumbani na uchunguze ni kiasi gani kinachotumiwa. Ikiwa dawa haitumiwi tena, itupe. Ikiwa kijana wako ameacha kukohoa lakini bado anatumia dawa, mwulize kwa nini anafanya hivyo. Mwishowe, uwe macho ili utambue anapobadili marafiki, sura, au tabia yake au maksi zake zinaposhuka kwa ghafula shuleni.

Ikiwa Mtoto Anatumia Dawa Vibaya

Ikiwa mtoto wako anatumia dawa vibaya au unashuku kwamba ana tatizo hilo, unaweza kufanya nini? Unahitaji kuzungumza kwa upendo na fadhili na mtoto wako kuhusu wasiwasi wako. “Fikra za mtu zimefichika kama kilindi cha maji,” inasema Biblia, “lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.” (Methali 20:5, Biblia Habari Njema) Kupata ukweli kutoka kwa mtoto anayedhaniwa kuwa anatumia dawa vibaya ni kama kuteka maji kwa kutumia kamba inayoweza kukatika kwa urahisi. Ukivuta kamba hiyo kwa nguvu sana kwa kumshutumu au kumkasirikia kwa uchungu, unaweza kukata kamba ya mawasiliano. Kumbuka kwamba unataka kutimiza mambo mawili. Kwanza, unataka kujua ikiwa kuna tatizo. Na pili, ikiwa kuna tatizo, ni nini kinacholisababisha. Mara nyingi, tatizo linaweza kusababishwa na moja kati ya mambo haya.

Marafiki wasiofaa na kushinikizwa nao. “Msidanganyike,” inasema 1 Wakorintho 15:33, “urafiki mbaya huharibu tabia njema.” (BHN) Kwa hiyo, wazazi wenye hekima watawasaidia watoto wao waone hatari ya kuwa na marafiki wasiofaa ambao wanaweza kuwa na uvutano mkubwa kwao. Kwa upande mwingine, wazazi kama hao watawasaidia watoto wao wachague marafiki wazuri. (Methali 13:20) Huenda Baba na Mama wakawaalika marafiki kama hao nyumbani au kwenye tafrija ya familia.

Mfadhaiko. Katika ulimwengu wa leo, watoto wanashinikizwa sana wafanikiwe, na wazazi wanafanya mambo yawe mabaya hata zaidi kwa kuwashinikiza zaidi. * Je, unajua uwezo na udhaifu wa watoto wako? Je, unawawekea miradi yenye kiasi na kuwasaidia kuifikia? Je, sikuzote unaepuka kumlinganisha mtoto wako na wengine ili asishuke moyo? Kwa kweli, ikiwa watoto hawatimiziwi mahitaji yao ya kihisia nyumbani, wataenda kutafuta upendo na urafiki wanaotaka kwingineko. Pia wazazi wenye hekima hujaribu kusitawisha mazoea mazuri ya ibada nyumbani, labda kwa kusoma Biblia pamoja na watoto wao. Yesu Kristo alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Kukosa kuwekewa mipaka. Vijana fulani hutumia dawa vibaya kwa sababu wazazi wao huwaendekeza. “Mvulana [au msichana] aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu,” inasema Methali 29:15. Ukweli ni kwamba watoto huthamini sheria zilizo wazi zinazowafanya wahisi wakiwa salama na wanapendwa, licha ya kwamba wao hulalamika kuzihusu. Hivyo, Biblia inawatia moyo wazazi wawawekee watoto wao miongozo inayofaa na vilevile wawawekee mfano mzuri. (Waefeso 6:4) Pia Biblia inasema wanapaswa kuhakikisha kwamba sheria hizo zinafuatwa na wawe thabiti. “Acheni Ndiyo yenu imaanishe Ndiyo, na Siyo yenu, Siyo.”—Yakobo 5:12.

Bila shaka, ukijua kwamba mtoto wako anatumia dawa vibaya, itafaa uzungumze na daktari kuhusu jambo hilo. Inaweza kuwa vigumu kuacha uraibu na huenda mtu akahitaji usaidizi kutoka kwa wataalamu. Pia, ikiwa familia yako ni sehemu ya kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, unapaswa kuomba msaada wa wazee. (Yakobo 5:13-16) Wanaume hao wenye sifa za kustahili kiroho wanaweza kukusaidia kutumia kanuni za Biblia ambazo zitasaidia kuacha zoea hilo.

Makala inayofuata itazungumzia kanuni nyingine na pia tumaini zuri la wakati ujao tunaloweza kuwa nalo.

[Maelezo ya Chini]

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Fikra za mtu zimefichika kama kilindi cha maji; lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.”—Methali 20:5, Biblia Habari Njema

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

DALILI ZA VIJANA WALIO HATARINI

▪ Kuna mtu fulani katika familia ambaye amewahi kutumia vibaya dawa au kileo

▪ Kushuka moyo au kujiona hawafai

▪ Kuhisi kwamba hawawezi kuchangamana na wengine; kujiona wao si maarufu

▪ Kujihisi walegevu mara kwa mara; kukosa usingizi

▪ Wajeuri, wenye mtazamo wa kuasi mamlaka *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Inategemea habari zilizochapishwa na Teen Help.