Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Haki ya Mgonjwa ya Kuchagua

Haki ya Mgonjwa ya Kuchagua

Haki ya Mgonjwa ya Kuchagua

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI ITALIA

▪ Mashahidi wa Yehova hukataa kutiwa damu mishipani. Wanakataa kwa kufuata amri zilizo katika Biblia. Mojawapo wa amri hizo ambayo iliandikwa zamani sana ni: “Isipokuwa tu nyama pamoja na nafsi yake—damu yake—msile.” Wakristo wa karne ya kwanza waliagizwa hivi: ‘Endeleeni kujiepusha na damu.’—Mwanzo 9:4; Matendo 15:29; Mambo ya Walawi 17:14.

Huko Monterenzio, Italia, wanafunzi wa sekondari waliombwa waandike insha kuhusu umuhimu wa kutoa damu. Mmoja kati ya wanafunzi hao alikuwa Benedetta ambaye ni Shahidi wa Yehova. Aliandika hivi:

“Inajulikana kwamba Mashahidi wa Yehova hawakubali kutiwa damu mishipani kwa sababu wanafuata viwango vya Biblia, lakini hilo halimaanishi kwamba hawakubali aina nyingine za matibabu. Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova huchukua kwa uzito mambo yanayohusu afya yao. Wao hujaribu kutafuta matibabu bora wanayoweza kupata kwa ajili yao na watoto wao. Wako tayari kabisa kushirikiana na madaktari, mradi tu wanaheshimu imani yao.”

Kisha Benedetta akaongezea hivi: “Kila mgonjwa ana haki ya kuchagua matibabu anayoamini kwamba ni bora kabisa kwake, pia ana haki ya kuheshimiwa, vilevile ana haki ya kujua hatari na faida za matibabu ambayo atapewa.”

Tawi la Monterenzio la Shirika la Watu Wanaotoa Damu la Italia (AVIS) liliwapa zawadi wanafunzi ambao walieleza vizuri kabisa maoni yao kuhusu jambo hilo. Ripoti katika gazeti Monterenzio Vivace ilisema hivi: “Benedetta Barbi alisifiwa sana kwa sababu ya insha yake ambayo ilikuwa kinyume na maoni ya watu wengi. Insha hiyo haikupatana na msimamo wa AVIS, lakini kupitia insha hiyo, mwanafunzi huyo alifaulu kueleza imani yake kwa usawaziko na heshima.”

Ingawa msimamo wa Mashahidi wa Yehova kuhusu damu ni “kinyume na maoni ya watu wengi,” madaktari wengi leo wametambua umuhimu wa msimamo huo. Kwa sababu ya msimamo wa Mashahidi, mbinu kadhaa za kupunguza kuvuja kwa damu wakati wa upasuaji zimeanzishwa. Hilo limewafaidi Mashahidi, na pia watu ambao si Mashahidi. Hata hivyo, sababu kuu inayowafanya Mashahidi wa Yehova wakatae kutiwa damu mishipani inategemea kabisa Biblia, kama ilivyoelezwa katika utangulizi wa makala hii.

Mashahidi wa Yehova watakapokutembelea nyumbani, kwa nini usiwaulize maoni ya Muumba kuhusu damu? Watafurahi sana kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe, nao watafanya hivyo kwa “heshima kubwa.”—1 Petro 3:15.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 30]

HABARI ZAIDI

Kwa msaada wa wataalamu wengi, DVD Transfusion Alternatives inachunguza kanuni za kitiba, kisheria, na kiadili kuhusu mbinu za matibabu zinazotumiwa badala ya kutiwa damu mishipani. Unaweza kupata DVD hiyo kutoka kwa Mashahidi wa Yehova.