Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoa Mimba—Si Suluhisho Lisilo na Madhara

Kutoa Mimba—Si Suluhisho Lisilo na Madhara

Kutoa Mimba—Si Suluhisho Lisilo na Madhara

TANGU alipokuwa mchanga, Bill aliamini kwamba kutoa mimba ni dhambi nzito sawa na kuua. Lakini msimamo wake thabiti ulibadilika mwaka wa 1975 alipokumbwa kibinafsi na uamuzi huo. Mpenzi wake Victoria alishika mimba na Bill hakutaka majukumu ya ndoa na kuwa mzazi. “Nilifikiria njia rahisi ya kutatua tatizo hilo,” akasema Bill, “na nikamwambia Victoria lazima atoe mimba hiyo.”

Kama Bill, ni kawaida kwa watu wengi kutumia kile alichokiita njia rahisi ya kutatua tatizo wanapopata mimba isiyotarajiwa au iliyo haramu. Uchunguzi uliofanywa ulimwenguni pote mnamo 2007 uliripoti kwamba mnamo 2003, mimba milioni 42 hivi zilitolewa ulimwenguni pote. Wanawake ambao hutoa mimba ni wa rangi, mataifa, dini mbalimbali, matajiri, maskini, wenye viwango mbalimbali vya elimu, na umri mbalimbali kati umri wa kubalehe na kukoma hedhi. Ikiwa ungepata mimba haramu, ungefanya nini? Kwa nini watu wengi sana huamua kutoa mimba?

‘Niliona Suluhisho Moja Tu’

“Nilikuwa nimetoka tu kuwa na mimba yenye matatizo na nikazaa kwa shida, na kulikuwa na matatizo mengi ya kifedha na ya kifamilia,” akaeleza mwanamke mwenye umri wa miaka 35. “Kisha majuma sita baada ya kuzaa, nilishika mimba nyingine. Tuliamua kuitoa. Moyoni nilihisi kwamba kufanya hivyo ni kosa, lakini niliona suluhisho hilo moja tu.”

Wanawake hutoa mimba kwa sababu mbalimbali zinazotia ndani matatizo ya kifedha, uhusiano uliovunjika, labda kwa sababu ya kutendewa vibaya na mwenzi wao na hivyo hawataki uhusiano zaidi na mwanamume huyo. Au huenda mimba hiyo itahitilafiana na mipango ya mwanamke huyo au wenzi wa ndoa.

Wakati mwingine watu hutoa mimba ili wasijiharibie jina. Ilikuwa hivyo katika kisa kilichoripotiwa na Dakt. Susan Wicklund katika kitabu chake This Common Secret—My Journey as an Abortion Doctor. Mgonjwa wake aliyetaka kutoa mimba alikiri hivi: “Wazazi wangu ni watu wa dini sana. . . . Nikipata mtoto nje ya ndoa, nitawaharibia jina. Marafiki wao wote wataona kwamba binti yao ni mtenda-dhambi.”

Kisha Dakt. Wicklund akamuuliza: “Hata kama watakuona kuwa mtenda-dhambi, wewe unahisije kuhusu kutoa mimba?” Msichana huyo akaniambia: “Aah, kutoa mimba. Hilo ni kosa zito sana. Lakini ni afadhali kwa kuwa hakuna mtu atakayejua. Nikitoa mimba, marafiki [wa wazazi wangu] kanisani hawatajua.”

Haidhuru kuna hali gani, kwa kawaida uamuzi wa kutoa mimba si rahisi. Mara nyingi jambo hilo huumiza sana. Lakini, je, kutoa mimba ni suluhisho lisilo na madhara?

Fikiria Madhara

Uchunguzi wa mwaka wa 2004 uliofanyiwa wanawake 331 Warusi na wanawake 217 Wamarekani waliotoa mimba ulifunua kwamba karibu nusu yao walijihisi vibaya baada ya kutoa mimba. Asilimia 50 hivi ya wanawake Warusi na karibu asilimia 80 ya wanawake Wamarekani walijihisi wakiwa na “hatia” kwa kutoa mimba. Zaidi ya asilimia 60 ya wanawake Wamarekani ‘hawakuweza kujisamehe.’ Kwa kuwa wanawake wengi wanaotoa mimba kutia ndani wale wasiofuata dini huhisi wakiwa na hatia, kwa nini bado wanawake wengi sana hutoa mimba?

Wengi hutoa mimba kwa sababu ya kushinikizwa sana wafanye hivyo. Wazazi, mwenzi wa ndoa, au marafiki wenye nia nzuri humshauri mtu kwamba kutoa mimba ndio njia bora badala ya kuzaa. Hilo linaweza kumfanya mtu afanye uamuzi wa haraka bila kuwa na habari kamili. “Hata hivyo, baada ya kufanya uamuzi na hata kutoa mimba,” anaeleza Dakt. Priscilla Coleman, mtaalamu wa madhara ya akili yanayosababishwa na kutoa mimba, “uwezo wa kufikiri wa mwanamke hurudia hali yake ya kawaida na mara nyingi humfanya awe na hisia nyingi za hatia, huzuni, na majuto.”

Mara nyingi watu hujuta kwa sababu wanajiuliza hivi: Je, kutoa mimba kuliua uhai ambao tayari ulikuwepo? Ripoti ya Kikundi cha Kuchunguza Utoaji-Mimba cha South Dakota ilisema kwamba wanawake wengi wajawazito waliofikiria kutoa mimba “walidanganywa kwamba ni ‘mkusanyo wa chembe kadhaa’ ambazo zingetolewa, na wanasema kwamba hawangetoa mimba ikiwa wangeambiwa ukweli.”

Baada ya kuchunguza “maelezo yenye kushtua na kuhuzunisha sana” ya wanawake 1,940 ambao walitoa mimba, uchunguzi huo ulifikia mkataa huu: “Wengi wa wanawake hao walikasirishwa na huzuni ya kumpoteza mtoto ambaye waliambiwa ni chembe tu.” Pia, uchunguzi huo ulionyesha kwamba “mara nyingi [mwanamke] anapatwa na madhara mengi sana ya kihisia anapotambua kwamba alimuua mtoto wake.”

Lakini ukweli ni nini? Je, kutoa mimba ni kutoa tu mkusanyo fulani wa chembe kutoka katika mwili wa mwanamke mjamzito? Je, mtoto ambaye yuko katika tumbo la uzazi ni mtu aliye hai?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

KUZAA AU KUTOA MIMBA

Uchunguzi uliofanywa mnamo 2006 ulichunguza maisha ya wanawake wengi waliopata mimba walipokuwa vijana. Nusu ya wanawake hao walizaa, na nusu wakatoa mimba. Uchunguzi huo ulifikia mkataa kwamba “wanapolinganishwa na wale wanaotoa mimba kuna uwezekano mdogo wa wanawake wanaozaa hawahitaji sana kupewa mashauri kwa sababu ya matatizo ya kiakili, kukosa usingizi, na kuvuta bangi.”—Journal of Youth and Adolescence.

“Matokeo ya uchunguzi nne mbalimbali ulimwenguni” yalionyeshwa katika ripoti nyingine. Uchunguzi huo ulionyesha nini? “Wanawake ambao wamewahi kutoa mimba wanapatwa na matatizo mbalimbali ya akili wakilinganishwa na wanawake ambao hawajawahi kutoa mimba.”—Ripoti ya Kikundi cha Kuchunguza Utoaji-Mimba cha South Dakota—2005.