Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri

Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri

Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri

Limesimuliwa na Ona Mockutė

Mnamo Aprili (Mwezi wa 4) 1962, nilipelekwa katika mahakama iliyojaa watu huko Klaipeda, Lithuania nikiwa nimeshtakiwa kwa uhalifu dhidi ya jamii. Oktoba (Mwezi wa 10) mwaka uliotangulia, nilikuwa nimekamatwa na kushtakiwa kwa kushiriki katika utendaji wa kidini ulioonwa kuwa uhalifu dhidi ya Serikali ya Sovieti. Acheni nisimulie mambo yaliyofanya nikamatwe na kufungwa kwa sababu ya kutafsiri kisiri vichapo vya Mashahidi wa Yehova.

NILIZALIWA mwaka wa 1930 magharibi mwa Lithuania karibu na Bahari ya Baltiki. Kabla ya kunizaa, mama yangu alikuwa amesali kwamba mtoto wake awe mtawa wa kike. Lakini aliniambia hivi wakati mmoja: “Siwezi kamwe kusali mbele ya Mtakatifu Petro au sanamu nyingine yoyote isiyo na uhai.” Nikikumbuka maneno yake, niliepuka kupiga magoti nikiwa kanisani, hata ingawa ningefanya hivyo mbele ya msalaba nilipokuwa barabarani kurudi nyumbani kutoka shuleni.

Baadaye, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu vilivyoanza 1939 hadi 1945, niliona ukatili usioelezeka na uliniathiri sana. Siku moja tulipokuwa chini ya utawala wa Ujerumani, nilikuwa nikikusanya matunda msituni pamoja na mama yangu mdogo. Tulifika mahali palipokuwa na mashimo mawili makubwa na tukaona damu. Tukijua kwamba Wayahudi fulani walikuwa wameuawa hivi karibuni, kutia ndani Tese na Sara, marafiki wangu wawili tuliosoma pamoja, tulijua kwamba mashimo hayo yalikuwa kaburi lao la jumla. Kwa mshtuko, nililia hivi: “Ee, Mungu, wewe ni mwema sana! Lakini kwa nini unaruhusu unyama kama huu?”

Mnamo 1949 nilimaliza shule ya sekondari huko Klaipeda karibu na nyumbani kwetu, na baada ya hapo nikaendelea na masomo yangu ya muziki. Mwaka wa 1950, nilijiunga na kikundi cha wanafunzi waliotaka mabadiliko ya kisiasa lakini upesi nilisalitiwa, na mimi pamoja na wanafunzi wengine 12 tukakamatwa. Nilifungwa huko Klaipeda, na nikiwa gerezani nilikutana kwa mara ya kwanza na Shahidi wa Yehova.

Najifunza Kweli za Biblia

Mwanamke fulani aliletwa katika seli yetu. Alitabasamu alipotutazama sisi wanawake wengine saba. Nilimuuliza hivi: “Rafiki yangu, kwa kawaida wafungwa huwa na huzuni wanapofungwa gerezani, lakini wewe unatabasamu! Tafadhali niambie ni kwa nini umeletwa hapa?”

“Kwa sababu ya kweli,” akajibu.

“Lakini kweli ni nini?” nikamuuliza.

Mwanamke huyo aliitwa Lydia Peldszus. Alikuwa Mjerumani na alikuwa amekamatwa kwa sababu ya imani yake kwani alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Tulizungumzia mambo mengi kuhusu Biblia pamoja naye. Kweli zenye kugusa moyo ambazo Lydia alitufundisha hazikubadili maisha yangu tu bali pia maisha ya wanawake wengine watatu ambao tuliishi katika seli moja.

Ujuzi Wangu wa Biblia Waongezeka

Kwa kuwa nilijihusisha katika kikundi kisicho halali cha kupinga Serikali ya Sovieti, nilihukumiwa kifungo cha miaka 25, na pia kifungo cha miaka 5 uhamishoni. Kupitia Mashahidi niliokutana nao nilipokuwa gerezani, vilevile katika kambi za kazi huko Siberia, ujuzi wangu kumhusu Mungu na makusudi yake uliongezeka. Kama Lydia, Mashahidi hawa walikuwa wamefungwa kwa sababu ya imani yao.

Ujuzi wangu kuhusu Biblia uliongezeka wakati huo na pia niliwaambia wengine mambo niliyoamini. Ingawa sikupata nafasi ya kubatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova, wafungwa wengine na wasimamizi wa gereza waliniona kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mnamo 1958, baada ya kutumika miaka minane ya kifungo changu niliachiliwa huru. Nilirudi Lithuania nikiwa na matatizo ya kiafya, lakini nikiwa thabiti katika imani yangu kwa Yehova.

Naanza Kutafsiri kwa Siri

Wakati huo, kulikuwa na Mashahidi wachache tu waliokuwa wamebaki nchini Lithuania. Wengine bado walikuwa wamefungwa gerezani au kupelekwa uhamishoni huko Siberia. Mnamo 1959, Mashahidi wawili walirudi kutoka Siberia na wakapendekeza kwamba nitafsiri vichapo vyetu vya Biblia katika Kilithuania. Nilikubali kazi hiyo, na nikaiona kuwa pendeleo.

Katika Machi (Mwezi wa 3) 1960, nilianza kutafsiri, na Julai (Mwezi wa 7), nilibatizwa kisiri katika Mto Dubysa. Kwa sababu ya upinzani kutoka kwa askari wa KGB (Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti), singeweza kupata kazi ya kunitegemeza, kwa hiyo niliishi na wazazi wangu ambao hawakuipinga imani yangu. Niliwalisha ng’ombe wa baba yangu pamoja na wa majirani. Niliendelea kutafsiri huku nikiwalisha wanyama hao. Ofisi yangu ilikuwa maridadi kwani niliketi kwenye kisiki cha mti nikiwa nimezungukwa na mkeka wa nyasi za rangi ya kijani. Juu ya kichwa changu kulikuwa na anga la bluu, na niliitumia miguu yangu kama dawati.

Hata hivyo, baadaye nilitambua kwamba haikuwa salama kutafsiri nikiwa malishoni, kwa kuwa ingekuwa rahisi kuonekana na askari wa KGB au vibaraka wao. Hivyo nilipopata mahali pa kujificha ili nitafsiri, nilihama kutoka kwa nyumba ya baba yangu. Nyakati nyingine nilifanya kazi nikiwa zizini. Huku wanyama wakiwa upande mmoja niliketi upande ule mwingine nikichapa kwa kutumia taipureta.

Kwa kuwa hakukuwa na umeme, nilifanya kazi wakati wa mchana. Ili sauti ya taipureta isisikike, familia niliyokuwa nikiishi nayo ilijenga kinu cha upepo nje ya zizi. Giza lilipoingia, niliingia katika nyumba kwa ajili ya chakula cha jioni. Kisha nilirudi zizini na kulala juu ya kitanda cha nyasi kavu.

Mnamo Oktoba 1961, mimi pamoja na Mashahidi wengine wawili tulikamatwa wakati kazi yangu kutafsiri vichapo vya kidini ilipogunduliwa. Hilo lilifanya nipelekwe mahakamani mwaka wa 1962 kama nilivyotaja mwanzoni mwa simulizi hili. Tuliruhusiwa kujitetea mbele ya umma na tukafurahia kuwatolea ushahidi watu wengi waliokuja kortini. (Marko 13:9) Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu na kupelekwa gerezani huko Tallinn, Estonia. Ninachojua ni kwamba, wakati huo ni mimi tu niliyekuwa nimefungwa katika gereza hilo kwa sababu ya dini yangu. Wasimamizi wa jiji walinitembelea, na niliwaambia kuhusu imani yangu.

Narudia Kazi ya Kutafsiri

Nilipofunguliwa kutoka gerezani huko Estonia mnamo 1964, nilirudi Lithuania. Nikiwa huko niliendelea kutafsiri vichapo vyetu, hasa kutoka Kirusi hadi Kilithuania. Nilikuwa na kazi nyingi sana. Ingawa wengine walinisaidia, mimi tu ndiye niliyetafsiri Kilithuania wakati wote. Mara nyingi nilifanya kazi siku saba kwa juma kuanzia asubuhi hadi usiku. Singeweza kupata nguvu za kufanya hivyo bila msaada wa Yehova.

Nikitambua jinsi kazi hiyo ilivyokuwa muhimu, sikuzote nilijaribu kuwa mwangalifu. Mara nyingi ndugu na dada Wakristo walijihatarisha na kuhatarisha familia zao ili wanifiche, wanipe chakula, na kunilinda. Ushirikiano huo ulitufanya tuwe na uhusiano wa karibu sana. Nilipokuwa nikifanya kazi, familia ambayo nilikuwa nikiishi nayo ilikuwa macho ili kuona watu ambao wangenishtaki. Ili kutoa tahadhari, mtu angetumia kifaa cha chuma kugonga mabomba ya kupashia nyumba joto mara mbili. Niliposikia onyo hilo, nilificha upesi kitu chochote ambacho kingeonyesha nilikuwa nikifanya kazi gani.

Ikiwa tungegundua kwamba askari walikuwa wakichunguza nyumba niliyokuwa nikifanyia kazi, ningehamia eneo lingine mara moja. Siku hizo ilikuwa ni kosa kubwa kupatikana na taipureta bila kibali cha serikali, kwa hiyo mtu mwingine angepeleka taipureta yangu kwenye eneo jipya la kazi. Kisha, hasa usiku, ningeelekea kwenye eneo hilo jipya.

Yehova alinilinda sana. Ingawa maofisa hawakuwa na uthibitisho, walijua nilichokuwa nikifanya. Kwa mfano, mnamo 1973, wakati Mashahidi wanane wa Yehova waliposhtakiwa, mwendesha-mshtaka aliniita ili aniulize maswali. Aliniuliza hivi moja kwa moja, “Mockutė, umechapisha vichapo vingapi katika miaka iliyopita?”

Nilimwambia kwamba singeweza kujibu swali hilo. Kisha akauliza, “Kwa hiyo ni swali gani unaloweza kujibu?”

Nikamjibu, “Swali lolote ambalo halihusiani na kazi hii.”

Hali Zabadilika

Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1980, hali nchini Lithuania zilianza kubadilika. Haikuwa lazima tena tujifiche kutoka kwa maofisa wa serikali. Kwa hiyo, mnamo 1990, wengine walianza kufanya kazi ya kutafsiri. Kisha, Septemba 1, 1992 (1/9/1992), ofisi ndogo ya kutafsiri ilianzishwa huko Klaipeda, jiji ambalo mwishowe nilikuja kuishi.

Kwa ujumla, nilifanya kazi ya kutafsiri kwa miaka 30 katika maeneo 16. Sikuwa na makao yangu mwenyewe. Ninashangilia kama nini kuona matokeo ya kazi yetu! Leo kuna Mashahidi wa Yehova 3,000 hivi nchini Lithuania. Na kazi ya kutafsiri niliyofanya wakati mmoja nikijificha katika mazizi na vyumba vya darini sasa inafanywa katika ofisi ya tawi yenye starehe ya Lithuania karibu na jiji la Kaunas.

Bado ninakumbuka tukio lenye kupendeza katika seli yenye baridi miaka 60 hivi iliyopita huko Klaipeda. Tukio hilo lilibadili maisha yangu! Sikuzote nitamshukuru Muumba wetu mkuu, Yehova, kwamba nilipata kweli kumhusu na kuhusu makusudi yake na kwamba niliweka maisha yangu wakfu kwake ili nifanye mapenzi yake.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Kweli za Biblia zenye kugusa moyo ambazo Lydia alitufundisha sisi wanne tulipokuwa gerezani zilibadili maisha yetu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kesi yangu iliripotiwa katika gazeti la Sovieti mnamo 1962

[Picha katika ukurasa wa 14, 15]

Baadhi ya vichapo vya Biblia ambavyo nilitafsiri nikihatarisha uhuru wangu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Lydia alinifundisha kweli za Biblia nilipokuwa gerezani

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mashahidi wawili (kushoto) walinifundisha mengi kumhusu Mungu nilipokuwa gerezani katika eneo la Khabarovsk, Urusi, mnamo 1956

[Picha katika ukurasa wa 15]

Taipureta niliyotumia nilipokuwa nikifanya kazi wakati wa marufuku