Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Hatukutoa Mimba

Sababu Hatukutoa Mimba

Sababu Hatukutoa Mimba

VICTORIA, aliyetajwa katika makala ya kwanza, alimwambia mpenzi wake, Bill kwamba hatatoa mimba. “Nilihisi kwamba kuna uhai ndani yangu,” akasema Victoria. “Nilitambua kwamba ikiwa ningeendelea kuwa na uhusiano na Bill, yeye hangenitunza wakati wa mimba yangu, kwa hiyo, nikaondoka.”

Hata hivyo, baadaye Bill alibadili maoni yake na akamwomba Victoria waoane. Lakini haikuwa rahisi kumtunza mwana wao. “Hatukuwa na gari, pesa, tulikuwa na nguo chache tu, na vitu vingine vichache,” anaeleza Victoria. “Bill alipata mshahara mdogo, na tuliishi katika nyumba mbovu, lakini tulijikaza kisabuni.”

Wengine pia wamekabili hali ngumu kwa sababu ya kupata mimba isiyotarajiwa. Hata hivyo, wao pia wamekataa kutoa mimba. Ni nini kilichowasaidia kuwa thabiti na kukabiliana na mfadhaiko wa kumlea mtoto asiyetarajiwa? Siri ilikuwa kufuata hekima ya Biblia.

Usiharakishe—Fanya Mipango Inayofaa

Biblia inasema hivi kwa hekima: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.”Methali 21:5.

Connie, mama mwenye wavulana watatu, kutia ndani mvulana mmoja mlemavu, alisongwa na mawazo alipogundua ana mimba. “Hatungeweza kumtunza mtoto mwingine,” akasema. “Kwa hiyo, tulifikiria kutoa mimba hiyo.” Lakini kabla ya kufanya uamuzi wa haraka, alizungumza na Kay, mfanyakazi mwenzake. Kay alimsaidia kutambua kwamba alikuwa amebeba mtu hai, na jambo hilo lilibadili mawazo yake.

Hata hivyo, Connie alihitaji kusaidiwa kufanya mipango. Kwa kuwa shangazi ya Connie aliishi karibu, Kay alipendekeza kwamba Connie azungumze naye. Shangazi huyo alikubali kusaidia. Isitoshe, mume wa Connie alianza kufanya kazi za ziada na wakahamia kwenye nyumba yenye kodi ya chini. Hivyo, walifaulu kumtunza mtoto wao.

Pia, Kay alimsaidia Connie awasiliane na mashirika yanayowasaidia watu waliopata mimba bila kutarajia. Katika nchi nyingi, kuna mashirika kama hayo yanayowasaidia akina mama wenye uhitaji. Unaweza kupata mashirika hayo kutoka kwa Intaneti au vitabu vya simu. Huenda jitihada nyingi sana zikahitajika, lakini “mipango ya mwenye bidii” ndiyo huleta faida.

Tambua Ni Mtu Aliye Hai

“Mtu yeyote mwenye hekima,” inasema Biblia, “macho yake yamo katika kichwa chake; lakini mjinga anaendelea kutembea katika giza tupu.”Mhubiri 2:14.

Mwanamke mwenye hekima hafungi macho yake asione mambo kihalisi na ‘kutembea gizani.’ Anatumia ‘macho yaliyo kichwani mwake,’ ambayo huongoza nguvu zake za kufikiri. Hilo humsaidia kupima matokeo ya matendo yake. Hivyo, tofauti na yule anayefunga macho yake asione kile kinachoendelea ndani ya tumbo lake la uzazi, mwanamke mwenye hekima hutenda kwa huruma inayotoka moyoni ili kulinda kiini-tete chake kilicho hai.

Stephanie, msichana aliyetaka kutoa mimba, alionyeshwa picha ya kompyuta ya mtoto wake wa miezi miwili aliyekuwa tumboni. “Niliangua kilio,” akasema Stephanie. “Nilijiambia: Kwa nini ninataka kuua kitu kilicho hai?”

Denise, msichana mwingine mjamzito ambaye hajaolewa, alitambua kwamba amebeba mtu aliye hai tumboni mwake. Mpenzi wake alipompa pesa za kutoa mimba hiyo, Denise alijibu: “Eti nitoe mimba? Siwezi kufanya hivyo!” Kwa hiyo, alikataa kumwua mtoto wake.

Kuwaogopa Watu Kunaweza Kukuathirije?

Ni jambo la hekima kufikiria methali hii ya Biblia iwapo watu wengine wanakushinikiza utoe mimba: “Kuwaogopa watu ni kujitega mwenyewe, lakini anayemtumaini Mwenyezi-Mungu yu salama.”Methali 29:25, Biblia Habari Njema.

Monica mwenye umri wa miaka 17 alitungwa mimba na mpenzi wake muda mfupi tu kabla ya kwenda chuo cha taaluma ya biashara. Mama yake, ambaye alikuwa mjane mwenye watoto watano, alitamauka sana. Alitaka binti yake ajifunze ufundi fulani ili ajiondoe kwenye umaskini ulioikumba familia hiyo. Kwa kuwa hakuwa na la kufanya, mama yake alisisitiza kwamba Monica atoe mimba hiyo. “Daktari aliponiuliza ikiwa nilitaka kutoa mimba hiyo,” anaeleza Monica, “nilimwambia ‘Hapana!’”

Akifikiria jinsi Monica alivyokuwa akipoteza nafasi nzuri ya kuboresha maisha yake na pia mfadhaiko wa kumtunza mtoto mwingine, mama yake alimfukuza nyumbani. Monica alienda kuishi na mama yake mdogo. Baada ya majuma machache, mama yake alibadili nia na kumruhusu arudi nyumbani ili azae. Mama ya Monica alimsaidia kumtunza Leon na alikuja kumpenda sana mvulana huyo.

Robin, mwanamke aliyeolewa alishinikizwa kwa njia tofauti. Robin anasema hivi: “Daktari wangu alinitibu kwa ugonjwa wa figo kabla ya kuchunguza ikiwa nina mimba. Niliambiwa kuna uwezekano mkubwa kwamba ningezaa mtoto mwenye akili punguani.” Daktari alimhimiza atoe mimba hiyo. “Nilimweleza maoni ya Biblia kuhusu uhai,” Robin anasema. “Nilimwambia kwamba siwezi kamwe kutoa mimba.”

Ingawa daktari alikuwa na sababu nzuri za kuhangaika, uhai wa Robin haukuwa hatarini. * “Nilipomzaa binti yangu alifanyiwa uchunguzi,” anasema Robin, “na iligunduliwa alikuwa amepooza ubongo kidogo tu. Maisha yake si mabaya. Sasa akiwa na umri wa miaka 15, anaendelea kuboresha uwezo wake wa kusoma. Ninampenda sana, na ninamshukuru Yehova mara nyingi kila siku kwa kunipa binti huyu.”

Urafiki na Mungu Una Nguvu

Biblia inasema: “Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa.”Zaburi 25:14.

Wengi kati ya wale wanaokataa kutoa mimba hufikiria jinsi Muumba wao anavyohisi kuhusu jambo hilo. Kuwa na urafiki na Mungu, na kufanya yale yanayompendeza ndilo jambo kuu maishani mwao. Jambo hilo ndilo lililomfanya Victoria ambaye alitajwa awali, asitoe mimba. Anasema: “Niliamini kabisa kwamba Mungu ndiye humpa mtu uhai na sikuwa na haki ya kuua uhai uliotoka kwake.”

Victoria alipoanza kujifunza Biblia kwa bidii, urafiki wake na Mungu ulikua. Alisema: “Uamuzi niliofanya wa kumzaa mtoto wangu ulifanya nijihisi nikiwa karibu zaidi na Mungu na ulifanya nitake kumpendeza katika sehemu zote za maisha yangu. Nilipomwomba mwongozo, mambo mengine yote yalifanikiwa.”

Kuwa rafiki ya Mungu, ambaye ndiye Chanzo cha uhai, hufanya tuheshimu zaidi uhai wa mtoto aliye katika tumbo la uzazi. (Zaburi 36:9) Isitoshe, Mungu anaweza kutoa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili kumsaidia mwanamke na familia yake kukabiliana na mimba isiyotarajiwa. (2 Wakorintho 4:7) Wanapotafakari uamuzi wao, wale walioheshimu maoni ya Mungu kuhusu uhai wanahisi namna gani?

Hawana Majuto

Wazazi hao hawana hatia, huzuni ya kuendelea, na hawaombolezi. Muda ulipopita, waliona kuwa “uzao wa tumbo” ni thawabu, si laana! (Zaburi 127:3) Connie, aliyetajwa mapema, alikubaliana na maneno hayo saa mbili tu baada ya kujifungua! Kwa msisimko, alimpigia simu Kay, mfanyakazi mwenzake, na kumwambia jinsi alivyotarajia kwa hamu kumlea msichana wake mdogo. Akiwa amefurikwa na shangwe, Connie aliongezea hivi: “Ni kweli kabisa kwamba Mungu huwabariki wale wanaofanya mambo yanayompendeza.”

Kwa nini kuna faida kutenda kupatana na maoni ya Mungu kuhusu uhai? Kwa sababu akiwa Chanzo cha uhai, Mungu ameweka sheria na viwango vyake katika Biblia ‘kwa faida yetu,’ au “kwa manufaa [yetu] wenyewe.”—Kumbukumbu la Torati 10:13; BHN.

Kulingana na Victoria na Bill, ambao walitajwa mwanzoni mwa makala hii na ile ya kwanza, uamuzi wao wa kutotoa mimba ulibadili maisha yao. Wanaeleza hivi: “Tulikuwa tukitumia sana dawa za kulevya na huenda tungekufa ikiwa tungeendelea. Lakini kuheshimu uhai wa mtoto wetu ambaye hakuwa amezaliwa kulitufanya tufikirie maisha yetu wenyewe. Kwa msaada wa Mashahidi wa Yehova, tulifanya mabadiliko.”

Lance, mwana wao, sasa anakaribia umri wa miaka 34 na amekuwa katika ndoa kwa zaidi ya miaka 12. Lance anasema hivi: “Tangu nilipokuwa mchanga, wazazi wangu walinifundisha kufanya maamuzi yanayotegemea Biblia. Hilo limenifaidi mimi, mke wangu, na mtoto wetu, na tumekuwa na furaha zaidi.” Baba yake ambaye hapo mwanzoni alimtaka Victoria atoe mimba anasema hivi, “Tunahuzunika sana tunapofikiria jinsi tulivyokuwa karibu kumpoteza mwana wetu mpendwa.”

Fikiria kisa cha Monica ambaye alikataa kushinikizwa na mama yake kutoa mimba. “Majuma mawili baada ya kumzaa mwana wangu,” anasema, “nilikutana na Mashahidi wa Yehova na kujifunza jinsi ya kupatanisha maisha yangu kikamili na sheria za Mungu. Nilianza kumfundisha mwana wangu Leon umuhimu wa kumtii Mungu, na baada ya muda akaja kumpenda Mungu sana. Sasa Leon ni mwangalizi anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova.”

Akitafakari yale ambayo mama yake alifanya, Leon alisema hivi: “Kujua kwamba alinipenda sana hivi kwamba akaniruhusu niendelee kuishi licha ya kushinikizwa sana kulinifanya nitake kutumia maisha yangu kwa njia bora zaidi ili nimwonyeshe Mungu kwamba ninathamini zawadi hiyo nzuri.”

Wengi ambao wamejua maoni ya Mungu kuhusu uhai hawana majuto kwa uamuzi wao wa kutomuua mtoto wao ambaye sasa wanampenda sana. Wanaweza kusema hivi wakiwa na mioyo iliyojaa shukrani, “Hatukutoa mimba!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Ikiwa wakati wa kuzaa kuna uhitaji wa kuchagua kati ya uhai wa mama na ule wa mtoto, ni juu ya watu wanaohusika kufanya uamuzi huo. Hata hivyo, maendeleo ya kitiba katika nchi nyingi yamepunguza sana uwezekano wa hali hiyo kutokea.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuona picha ya kompyuta ya mtoto wake wa miezi miwili aliyekuwa tumboni kulimsaidia Stephanie kufanya uamuzi

(Tumechora kuzunguka kiini-tete)

[Picha katika ukurasa wa 8]

Victoria na Lance

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Victoria na Bill leo, pamoja na Lance na familia yake

[Picha katika ukurasa wa 9]

Monica na mwana wake Leon wanashukuru sana kwamba alikataa kushinikizwa kutoa mimba miaka 36 iliyopita