Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wakatoliki Wahimizwa Watoe Ushahidi

Vijana Wakatoliki Wahimizwa Watoe Ushahidi

Vijana Wakatoliki Wahimizwa Watoe Ushahidi

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI AUSTRALIA

JULAI iliyopita, waumini wa Kanisa Katoliki kutoka ulimwenguni pote walikutana huko Sydney, Australia, kusherehekea Siku ya Vijana Ulimwenguni ya 2008, tamasha ya kidini iliyodhaminiwa na Kanisa Katoliki.

Wageni waliokuwa wamebeba bendera kutoka mataifa 170 walijaa barabarani wakishangilia, wakiimba, na kujaza jiji lote hisi ya sherehe. Maelfu ya watazamaji walijaa kwenye Bandari ya Sydney ili wamwone Papa Benedikto wa 16 aliyewasili kwa meli akiandamana na meli nyingine 12 zenye kuvutia. Watu milioni 500 hivi ulimwenguni walitazama tukio hilo moja kwa moja kwenye televisheni.

Misa ya mwisho, iliyofanywa katika uwanja wa mashindano ya farasi ya jiji hilo, ilihudhuriwa na watu 400,000 hivi, kutia ndani maofisa 4,000 wa kanisa na waandishi wa habari 2,000. Hilo ndilo lililokuwa tukio kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini Australia, likizidi rekodi ya hudhurio iliyowekwa katika michezo ya Olimpiki ya Sydney mwaka wa 2000.

Siku ya Vijana Ulimwenguni ni nini? Kwa nini inaadhimishwa? Ni mambo gani yanayofanywa siku hiyo? Na siku hiyo ilifunua nini kuhusu imani ya vijana huko Sydney?

“Imani Inazorota”

Siku ya Vijana Ulimwenguni ni tukio la kila mwaka linalochochea imani ya vijana Wakatoliki. Kwa kawaida, washiriki wa Kanisa hukusanyika katika dayosisi ya kwao. Hata hivyo, baada ya kila miaka miwili au mitatu, jiji kubwa hupanga sherehe hiyo na vijana Wakatoliki ulimwenguni pote hukaribishwa kuhudhuria. Majiji kumi katika mabara matano tofauti yamepanga sherehe hiyo na mamilioni wamehudhuria.

Lakini, kama tu viongozi wa kanisa wanavyokubali, Siku ya Vijana Ulimwenguni imekusudiwa pia kuzuia kupungua kwa wafuasi katika Kanisa Katoliki. “Tunakabili tatizo kubwa sana kwa kuwa watu wanaacha Ukatoliki na imani inazorota,” akasema George Cardinal Pell, kasisi mwenye cheo cha juu wa Kanisa Katoliki Australia. “Tunajaribu kurekebisha mambo kupitia Siku ya Vijana Ulimwenguni.”

Takwimu za Vatikani zinaonyesha kwamba idadi ya makasisi inapungua sana ulimwenguni. Katika miaka ya karibuni, makumi ya maelfu ya makasisi wamejiuzulu ili waoe. Idadi ya wale wanaosomea ukasisi nchini Australia imepungua kwa zaidi ya asilimia 70 katika miaka 30 iliyopita. Kwa wastani, makasisi wa dayosisi kubwa zaidi nchini Australia wana umri wa miaka 60 hivi, ilhali katika mwaka wa 1977 wastani ulikuwa umri wa miaka 40 hivi.

Vilevile, idadi ya watu wanaoenda kanisani katika nchi nyingi imepungua. Karibu asilimia 25 ya Waaustralia husema wao ni Wakatoliki lakini ni asilimia 14 tu kati yao ambao huenda kanisani kwa ukawaida. Idadi ya vijana wanaoenda kanisani imepungua kwa asilimia 10. Wakati huohuo, Wakatoliki wengi hawatii mafundisho ya kanisa kuhusu maadili, kupanga uzazi, na talaka. Wengine wamevunjwa moyo na kashfa za kidini, kama zile zinazowahusu makasisi wanaolala na watoto.

Siku ya Vijana Ulimwenguni “kwa kweli ni jitihada ya kufa na kupona ya kuzuia kanisa lisiangamie,” linasema gazeti The Sydney Morning Herald. “Viongozi wa kanisa nchini Australia na Rome wanatafuta njia ya kufanya watu wawe na imani tena kupitia vijana.” Viongozi wa dini wanafanya nini ili kuwafikia?

Maonyesho na Sherehe Zenye Kusisimua

Siku ya Vijana Ulimwenguni ya 2008 ilitia ndani maonyesho ya kanisa, mazungumzo ya vikundi, kutembelea maeneo yanayoonekana kuwa matakatifu, na Misa iliyohudhuriwa na watu wengi. Ingawa utendaji wote huo uliwachochea wengi waliohudhuria, wengine wameona kuna mtazamo mwingine unaofanya sherehe hizo zisisimue. Kijana mmoja Mkatoliki anayeitwa Alexandra kutoka Marekani alisema hivi kuhusu Siku ya Vijana Ulimwenguni, “Hiyo ni sherehe kubwa tu.”

Mkusanyiko huo wa siku sita uliofanyiwa Sydney ulikuwa na maonyesho 450 ya sherehe, kutia ndani tamasha za muziki, sinema, michezo ya kuigiza, maonyesho, na sherehe za barabarani. Muziki ulitia ndani opera, nyimbo rasmi za Kikatoliki zinazoimbwa wakati wa sherehe, heavy metal, na rapu. Tamasha za muziki wa roki ziliwavutia maelfu ya vijana wenye kupenda raha.

Wakatoliki fulani walihangaishwa na maonyesho hayo. Pindi hiyo “imekuwa sherehe tu ya kujifurahisha—juma zima la sherehe, tamasha za muziki, na utendaji wa kilimwengu kukiwa na mambo machache sana yaliyo matakatifu kikweli,” akasema kasisi Peter Scott akizungumza na Shirika la Habari la Australia. Kwa kweli, katika mwaka wa 2000, Papa Benedikto wa 16, ambaye wakati huo alikuwa Kadinali Ratzinger, aliandika hivi: “‘Muziki wa roki’ huonyesha hisia nyingi sana za kimwili, na katika tamasha za muziki wa roki hisia hizo hugeuka kuwa za kimadhehebu, kuwa namna ya ibada ambayo kwa kweli, ni kinyume na ibada ya Kikristo.”—The Spirit of the Liturgy.

Huenda mtu akauliza, “Je, Siku ya Vijana Ulimwenguni itabadili maisha ya watu?” “Huenda ikabadili maisha ya wachache,” akasema Paul Collins, ambaye aliacha ukasisi. “Lakini wengi watarudia tu maisha yao ya awali,” akasema. “Mabadiliko muhimu hayaletwi na matukio makubwa, lakini yanakuja kupitia kutafakari, kupanga mambo kwa uangalifu na kuwa tayari kukabiliana na matatizo yaliyokita mizizi.”

“Mtakuwa Mashahidi Wangu”

Viongozi wa kanisa wanatambua mambo hayo. Hivyo, Siku ya Vijana Ulimwenguni ya 2008 ilikuwa na kichwa: “Roho Mtakatifu atakapowashukieni ninyi, mtajazwa nguvu na mtakuwa mashahidi wangu.” *

Maaskofu waliwahimiza waliohudhuria “wawe na bidii nyingi zaidi kama ile ya mitume ya kuwaeleza wengine mafundisho ya Kristo katika ulimwengu wa sasa.” Papa Benedikto wa 16 aliwahimiza waliohudhuria wawe “kizazi kipya cha mitume,” na kwenye pindi nyingine akawasihi waeneze “Habari Njema kati ya marafiki, familia, na wote ambao watakutana nao.”

Watu fulani waliohudhuria walichochewa sana na maneno hayo. Ramido, mwenye umri wa miaka 20 kutoka Marekani, alimwambia hivi mwandishi mmoja wa habari: “Ninachukua kwa uzito jukumu la kuwa shahidi.” Lakini Beatrice, mwenye umri wa miaka 18 kutoka Italia, alisema hivi: “Siku hizi vijana hawazungumzi kumhusu Mungu. Kuwa shahidi katika siku hizi ni jambo gumu sana.” Watu wengi waliohudhuria walikuwa na maoni kama ya wasichana wawili kutoka Texas, Marekani, “Watu pekee ambao hutoa ushahidi nchini kwetu ni Mashahidi wa Yehova!”

Vijana Wanaotoa Ushahidi

Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova, vijana kwa wazee, wanajulikana sana kwa bidii yao ya kutoa ushahidi. Kwa nini wao hufanya kazi hiyo? Kwa sababu ya “kumpenda Mungu, kuwapenda watu, na kuipenda Biblia,” akasema Sotir, Shahidi mwenye umri wa miaka 22 huko Sydney.

Katika Siku ya Vijana Ulimwenguni ya 2008, karibu vijana 400 Mashahidi huko Sydney, walishiriki katika kampeni ya pekee ya kuwaeleza kweli za Biblia Wakatoliki waliohudhuria, ingawa Mashahidi hao hawakuhudhuria sherehe hiyo. “Nilifurahi kukutana na vijana hao Wakatoliki wanaoiheshimu Biblia,” akasema Travas, mwenye umri wa miaka 25. “Wengi wao walikuwa na maswali mazuri ya Biblia, na nilifurahi sana kuwaonyesha majibu yenye kuridhisha.”

“Nilizungumza kwa utulivu na kwa njia isiyo rasmi,” akasema Tarsha, mwenye umri wa miaka 23. “Nilitaka kuwakaribisha katika jiji la Sydney na kusikia waliamini nini.” “Ilipofaa, niliwapa wageni hao zawadi—kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?” * akasema Frazer, mwenye umri wa miaka 20. “Kila mtu niliyekutana naye alifurahia kupata kitabu hicho.”

Ilikuwa wazi kwamba wageni wengi walifurahia mazungumzo yao na vijana Mashahidi. Suzanne, kutoka Fiji, alimwuliza Belinda, Shahidi mwenye umri wa miaka 19, kwa nini Mungu ameruhusu watu wateseke. Belinda alipendekeza kwamba wazungumzie jibu linaloonyeshwa katika kitabu Biblia Inafundisha. Walipomaliza, Suzanne alisema: “Kwa kawaida nikiuliza watu swali hilo, wao huniambia tu kwamba Mungu hufanya mambo kwa njia ya ajabu. Lakini sasa nimepata jibu!” Belinda alipompa kitabu hicho, Suzanne alisema hivi kwa mshangao: “Nilikuwa nikijaribu kukariri kila kitu ulichosema. Sikufikiri ungenipa kitabu hiki!”

Mgeni mmoja Mfilipino alimwomba Marina, Shahidi mwenye umri wa miaka 27, ampige picha mbele ya jengo fulani maarufu huko Sydney. Baada ya mazungumzo ya kirafiki, Marina alimpa mwanamke huyo kitabu Biblia Inafundisha. “Jana usiku nilisali niweze kuielewa Biblia vizuri zaidi,” akasema mwanamke huyo. “Huenda kitabu hiki kikawa jibu la sala hiyo!”

Levi, Shahidi mwenye umri wa miaka 27 alianzisha mazungumzo na wageni wawili kutoka Panama, mama na binti yake. Muda si muda wakaanza kuzungumzia mambo yanayohusiana na kumwabudu Mungu, na wakazungumzia mafundisho mengi ya Biblia. Wote wawili walikubali kitabu Biblia Inafundisha. Baadaye, Levi akauliza, “Mmefurahia nini zaidi katika safari yenu?” Akiwa ameshika kitabu Biblia Inafundisha, yule binti akamjibu, “Tumefurahia zaidi kukutana nawe.”

Naam, vijana wengi Wakatoliki walitaka sana kujua mengi kuhusu Biblia. Namna gani wewe? Je, ungependa kuielewa Biblia vizuri zaidi? Basi mbona usiwaombe Mashahidi wa Yehova wajifunze nawe Biblia bila malipo? Watafurahi sana kukusaidia pia!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Hiyo ni sehemu ya nukuu la andiko la Matendo 1:8 katika The New Testament in Kiswahili with Catholic Notes.

^ fu. 25 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

“Tunakabili tatizo kubwa sana kwa kuwa watu wanaacha Ukatoliki na imani inazorota.”—George Cardinal Pell wa Kanisa Katoliki

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

MAONYESHO YA WITO WA KANISA

Siku ya Vijana Ulimwenguni ya 2008 ilikuwa na maonyesho makubwa zaidi kuwahi kufanywa nchini Australia ya kuhusu wito wa kidini. Zaidi ya makanisa na mashirika 100 ya Kikatoliki yaliwahimiza zaidi ya wageni 50,000 wafikirie kuwa makasisi, watawa, au wafanyakazi wa kidini wa Kanisa Katoliki.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Wahudhuriaji waliovalia mavazi yenye kuvutia walijaa barabarani

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mashahidi wa Yehova walizungumza na wale waliotembelea jiji la Sydney

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]

Getty Images