Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wape Watoto Wako Mwanzo Mzuri Maishani

Wape Watoto Wako Mwanzo Mzuri Maishani

Wape Watoto Wako Mwanzo Mzuri Maishani

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI KANADA

▪ “Televisheni inaweza kuwa kifaa kizuri sana cha kujifunzia,” inasema ripoti moja katika gazeti The New York Times. Hata hivyo, “akili na miili ya watoto inaathiriwa kwa kutumia saa nyingi kutazama televisheni,” na hivyo kuwanyima nafasi ya kushiriki utendaji unaowasaidia kuwa wabunifu, kujifunza, na kuchangamana na watu.

Baada ya kuchunguza mazoea ya kutazama televisheni ya watoto 2,500, watafiti katika Hospitali ya Watoto huko Seattle, Washington, Marekani, “walitambua kwamba kadiri watoto walio na umri wa kati ya mwaka mmoja hadi miaka mitatu walivyotazama televisheni sana, ndivyo hatari yao ya kukosa kuwa makini ilivyoongezeka walipofikia umri wa miaka saba,” linasema gazeti hilo. Watoto hao walikuwa wajeuri kupita kiasi na hawakuwa watulivu na waliweza kukaza fikira kwa muda mfupi tu. Kulingana na mwanasaikolojia wa masuala ya elimu Dakt. Jane M. Healy, “wazazi wengi ambao watoto wao walikuwa na matatizo ya kukaza fikira walitambua kwamba hali hiyo ilibadilika na kuwa nzuri baada ya kuwazuia watoto wao kutazama televisheni.”

Wazazi wanaweza kufanya nini ili kupunguza muda ambao watoto wao wanatumia kutazama televisheni? Ripoti hiyo ilitoa mapendekezo yafuatayo: Weka mipaka kuhusu ni wakati gani na kwa muda gani watoto wako wanaweza kutazama televisheni kila siku. Epuka kutumia televisheni kuwa mlezi. Badala yake, mhusishe mtoto wako katika kazi nyingi iwezekanavyo za nyumbani. Chagua vipindi ambavyo mtoto wako anaweza kutazama, na uizime televisheni baada ya vipindi hivyo kwisha. Inapowezekana, tazama vipindi ulivyochagua pamoja na mtoto wako na mzungumzie kuhusu mambo mnayotazama. Mwishowe, weka mipaka kuhusu muda ambao wewe mwenyewe unatumia kutazama televisheni.

Unahitaji muda, azimio, na nidhamu ili ufaulu kuwazoeza watoto wawe wabunifu na wawe na uwezo wa kuchangamana na watu. Matokeo mazuri ambayo mtu anapata yanatokana na jitihada anazotia. Hilo linathibitishwa na methali moja ya kale inayosema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” (Methali 22:6) Sehemu moja muhimu katika mazoezi kama hayo inahusisha kuwafundisha watoto wawe na viwango vinavyofaa vya maadili.

Mashahidi wa Yehova wanatumia kwa mafanikio kitabu chao Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu ili kuwafundisha watoto wao masomo muhimu kuhusu tabia zinazofaa. Kwa kweli, mzazi anapokuwa na mawasiliano mazuri na kuwahangaikia kwa upendo watoto wanapokuwa wachanga, atakuwa na matokeo mazuri yenye kudumu. Hakuna jambo linaloweza kuwaridhisha wazazi kuliko kuwaona watoto wao wakikomaa na kuwa watu wazima wenye kuheshimika.