Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Chuki na Ubaguzi—Kufichua Mizizi Yake

Chuki na Ubaguzi—Kufichua Mizizi Yake

Chuki na Ubaguzi—Kufichua Mizizi Yake

“Wanadamu wote wanazaliwa wakiwa huru na sawa katika adhama na haki. Wamejaliwa uwezo wa kusababu na dhamiri pia, nao wapaswa kutendeana kwa roho ya udugu.”—Kifungo cha 1 cha Azimio la Haki za Kibinadamu kwa Wote.

LICHA ya malengo hayo mazuri, bado chuki na ubaguzi unaendelea kuwakumba wanadamu. Hali hiyo yenye kusikitisha inaonyesha mambo yanayotukia sasa na pia hali ya kutokamilika kwa wanadamu. (Zaburi 51:5) Lakini kuna matumaini. Ni kweli kwamba huenda tusiweze kuondoa ubaguzi kutoka kwa watu wengine, lakini sisi wenyewe tunaweza kujitahidi kuondoa mawazo yoyote ya ubaguzi yaliyo mioyoni mwetu.

Jambo la kwanza tunalopaswa kujua ni kwamba sote tunaweza kuonyesha ubaguzi. Kitabu Understanding Prejudice and Discrimination kinasema hivi: “Huenda mambo muhimu zaidi ambayo tumejifunza katika utafiti kuhusu ubaguzi ni haya: (1) kila mwanadamu aliye na uwezo wa kufikiri na kusema anaweza kuwa na ubaguzi, (2) kwa kawaida lazima mtu atambue anaweza kuonyesha ubaguzi na ajitahidi sana ili asifanye hivyo, na (3) mtu akichochewa inavyofaa anaweza kufaulu.”

Imesemwa kwamba “njia bora zaidi” ya kukabiliana na ubaguzi ni kuwaelimisha watu. Kwa mfano, elimu inayofaa inaweza kufichua mizizi ya ubaguzi, kutuwezesha tuchunguze mitazamo yetu vizuri zaidi, na kutusaidia kutenda kwa hekima tunapobaguliwa.

Kufichua Mizizi

Ubaguzi huwafanya watu wapotoshe, waelewe vibaya, au wapuuze mambo hakika yanayopingana na maoni yao. Lakini chanzo cha ubaguzi ni nini? Mtu anapochunguza kwa uangalifu, anaweza kugundua kwamba huenda ubaguzi ukatokana na viwango vya familia vilivyopotoshwa lakini vinavyoonekana kuwa sawa, au unaweza kupandwa na watu wanaoendeleza maoni yasiyofaa kuhusu watu wa jamii au utamaduni mwingine. Ubaguzi unaweza kuchochewa pia na utaifa na mafundisho ya dini za uwongo. Unaweza kutokezwa na kiburi. Unapofikiria mambo yafuatayo na kanuni zinazofaa za Biblia, mbona usichunguze mitazamo yako mwenyewe na uone ikiwa unahitaji kufanya mabadiliko?

Marafiki. Kwa kawaida, wanadamu wanapenda kushirikiana na wengine na hilo ni jambo zuri. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba “mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe” na hata atashindana na hekima inayotumika. (Methali 18:1) Hata hivyo, tunapaswa kuchagua marafiki wetu kwa hekima kwa kuwa wanaweza kuwa na uvutano mkubwa kwetu. Kwa hiyo, wazazi wenye hekima wanapendezwa sana kujua marafiki wa watoto wao. Uchunguzi umeonyesha kwamba hata watoto wenye umri wa miaka mitatu wanaweza kuwa na ubaguzi wa rangi, kwa sababu ya mtazamo, maneno, na mambo ambayo wengine wanafanya. Bila shaka, wazazi wanapaswa kufanya yote wanayoweza ili wawe na uvutano mzuri kwa watoto wao, kwa kuwa wazazi ndio huchangia sehemu kubwa katika ukuzi wa mtoto.

Biblia inasema nini? “Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri, naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.” (Methali 22:6, Biblia Habari Njema) “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Ikiwa wewe ni mzazi, jiulize hivi: ‘Je, ninawaelekeza watoto wangu katika njia ya kweli na iliyo sawa machoni pa Mungu? Je, ninashirikiana na watu walio na uvutano mzuri kwangu? Je, nina uvutano mzuri kwa wengine?’—Methali 2:1-9.

Uzalendo. Kamusi moja inafafanua uzalendo kuwa “kutukuza taifa moja juu ya mataifa mengine yote na kusisitiza kuendelezwa kwa utamaduni wake na mapendezi ya taifa hilo badala ya yale mataifa mengine.” Ivo Duchacek, profesa wa siasa, alisema hivi katika kitabu chake Conflict and Cooperation Among Nations: “Uzalendo hugawanya wanadamu katika visehemu visivyoweza kuvumiliana. Kwa sababu hiyo, watu hujiona kuwa Wamarekani, Warusi, Wachina, Wamisri, Waperu, au watu wa taifa lingine, kisha wanajiona kuwa wanadamu—ikiwa kwa vyovyote wao hujifikiria hivyo.” Aliyekuwa katibu mkuu wa UM aliandika hivi: “Matatizo mengi tunayokabili leo ni kwa sababu ya, au yanatokana na mitazamo isiyofaa ambayo tumesitawisha, mengine bila kujua. Mawazo hayo yanatia ndani wazo la kwamba ‘nitaitetea nchi yangu iwe imekosea au la.’”

Biblia inasema nini? “Mungu aliupenda ulimwengu [wanadamu wote] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Jiulize hivi, ‘Ikiwa Mungu anawapenda bila ubaguzi watu wa mataifa yote kutia ndani mimi, je, sipaswi kumwiga, hasa ikiwa ninadai kwamba ninamwabudu?’

Ubaguzi wa rangi. Watu wenye ubaguzi wa rangi wanaamini “kwamba rangi ya mtu inaamua tabia au uwezo wake na kwamba watu wa rangi fulani ni bora kuliko wengine,” inasema kamusi moja. Hata hivyo, kulingana na The World Book Encyclopedia, watafiti “hawajagundua msingi wowote wa kisayansi wa kuthibitisha madai kama hayo kwamba [watu wa rangi fulani] ni bora kuliko wengine.” Ukosefu mkubwa sana wa haki unaochochewa na ubaguzi wa rangi, kama vile kuwanyima wanadamu wenzao haki zao, ni uthibitisho wenye kusikitisha kwamba ubaguzi wa rangi unatokana na maoni ya uwongo.

Biblia inasema nini? “Kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) “[Mungu] alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” (Matendo 17:26) “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Jiulize hivi: ‘Je, mimi hujaribu kuwaona wanadamu wote kama Mungu anavyowaona? Je, mimi hujaribu kuwaelewa na kuwafahamu kabisa watu wa rangi au utamaduni mwingine?’ Tunapowafahamu watu vizuri, inakuwa rahisi zaidi kuwa na maoni yanayofaa kuwahusu.

Dini. Kitabu The Nature of Prejudice kinasema: “Chuki hutokea watu wanapotumia dini yao kutetea [ubinafsi] na mapendezi ya kikabila. Hapo ndipo dini na ubaguzi hupatana.” Kitabu hichohicho kinasema kwamba jambo linaloshangaza zaidi ni jinsi watu wengi wanaodai kufuata dini “wanavyopoteza sifa zao za kiroho kwa urahisi na kuwa na ubaguzi.” Jambo hilo linaonekana wazi katika dini za watu wa rangi moja, chuki na jeuri kati ya vikundi vya kidini, na ugaidi unaochochewa na dini.

Biblia inasema nini? “Hekima inayotoka juu [kwa Mungu] . . . ni . . . yenye kufanya amani, yenye usawaziko, . . . haifanyi tofauti zenye ubaguzi.” (Yakobo 3:17) “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23) ‘Wapendeni adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.’ (Mathayo 5:44) Jiulize hivi: ‘Je, dini yangu inanichochea kuwapenda watu wote kikweli, kutia ndani hata wale ambao huenda wakataka kuniumiza? Je, dini yangu inamkaribisha kila mtu bila kujali taifa, rangi, jinsia, hali yake ya kiuchumi, au ya kijamii?’

Kiburi. Mtu anapoanza kujivuna au kujiona kuwa mtu wa maana kupita kiasi, kiburi kinaweza kumfanya aanze kuonyesha ubaguzi. Kwa mfano, kiburi kinaweza kumfanya mtu ajione kuwa bora kuliko wengine au awadharau watu ambao hawana elimu kama yake au walio maskini. Huenda pia kikamfanya aamini propaganda zinazotukuza taifa au kabila lake. Watu walio na ustadi wa kueneza propaganda kama vile dikteta wa Nazi Adolf Hitler, wamechochea kimakusudi watu wajivunie taifa na rangi yao ili kutafuta wafuasi na kuwaharibia jina wale wanaoonwa kuwa tofauti au hawafai.

Biblia inasema nini? “Kila mtu mwenye kiburi moyoni ni chukizo kwa Yehova.” (Methali 16:5) ‘Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mwaone wengine kuwa ni bora kuliko ninyi.’ (Wafilipi 2:3) Jiulize hivi: ‘Je, moyoni mwangu mimi hufurahi watu wanaposifu rangi au kabila langu na kuwadharau wengine? Je, nina mwelekeo wa kuwaonea wivu watu walio na vipawa ambavyo mimi sina, au mimi hufurahia kutoka moyoni uwezo wao?’

Hiyo ndiyo sababu Biblia inatuonya hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) Hivyo, ona moyo wako kuwa kitu cha thamani na usiache kitu chochote kiupotoshe! Badala yake, ujaze hekima kutoka kwa Mungu. Ni kwa kufanya hivyo tu ndipo ‘uwezo wa kufikiri na utambuzi utakulinda, ili kukukomboa kutoka katika njia mbaya, na kutoka kwa mtu anayesema mambo mapotovu.’—Methali 2:10-12.

Lakini unaweza kufanya nini ikiwa unachukiwa au kubaguliwa? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Tunapowafahamu watu vizuri, inakuwa rahisi zaidi kuwa na maoni yanayofaa kuwahusu