Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kunapaswa Kuwa na Tofauti Kati ya Makasisi na Waumini?

Je, Kunapaswa Kuwa na Tofauti Kati ya Makasisi na Waumini?

Maoni ya Biblia

Je, Kunapaswa Kuwa na Tofauti Kati ya Makasisi na Waumini?

Padri, Mchungaji, Baba, Baba Mtakatifu, Rabi, Mhadhamu Kadinali, Mtukufu, Mtakatifu—hayo ni baadhi ya majina ya cheo ambayo huwatofautisha makasisi wa dini mbalimbali na waumini wao. Tofauti kati ya makasisi na waumini ni jambo la kawaida katika dini nyingi, lakini je, ni mpango kutoka kwa Mungu, au ni mapokeo ya wanadamu? Je, Mungu anakubali jambo hilo?

“KATIKA Agano Jipya na wakati mitume walikuwa hai hakukuwa na tofauti kati ya viongozi wa kidini na waumini,” akaandika Cletus Wessels, profesa wa mambo ya dini. Kitabu Encyclopedia of Christianity kinasema hivi: “Hatua kwa hatua kukawa na tofauti kati ya makasisi waliokuwa na vyeo na waumini . . . Washiriki wa kanisa wa ‘kawaida’ wakaonwa kuwa watu wasiofaa kitu.” Tofauti hiyo ilionekana wazi katika karne ya tatu W.K.—zaidi ya miaka 200 baada ya Yesu Kristo!

Ikiwa tofauti kati ya makasisi na waumini haitegemei kielelezo kilichowekwa na mitume wa Yesu na Wakristo wengine wa mapema, je, ni vibaya kuwa na tofauti hiyo? Biblia inasema ndiyo. Hebu ona kwa nini inajibu hivyo.

“Ninyi Nyote Ni Ndugu”

Neno la Mungu linatuambia kwamba Wakristo wote ni watumishi wa Mungu na kwamba hakuna yeyote aliye mkubwa au mdogo kuliko mwenzake. (2 Wakorintho 3:5, 6) Wakristo wa mapema “walisisitiza kwamba hakupaswi kuwa na tofauti zozote” kati yao, anasema mwandishi wa mambo ya kidini Alexandre Faivre. ‘Kutokuwa na tofauti zozote’ kunapatana na maneno haya ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Ninyi nyote ni ndugu.”—Mathayo 23:8.

Bila shaka, wanaume waliokuwa wakomavu kiroho walitumika kama waangalizi, jambo lililotia ndani kuwa wachungaji na walimu. (Matendo 20:28) Hata hivyo, wanaume hao hawakulipwa. Wengi wao walikuwa watu wanaofanya kazi za kawaida—waume na akina baba. Isitoshe, walistahili kuwa waangalizi, si kwa kwenda kwenye seminari, bali kwa kuwa wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu na kusitawisha sifa za kiroho ambazo Mungu anataka. Sifa hizo zinatia ndani kuwa “mwenye kiasi katika mazoea, mwenye utimamu wa akili, mwenye utaratibu, mkaribishaji-wageni, mwenye sifa za kustahili kufundisha, . . . mwenye usawaziko, si mtaka-vita, si mwenye kupenda pesa, mwanamume anayeisimamia nyumba yake mwenyewe kwa njia nzuri.”—1 Timotheo 3:1-7.

Hekima ya Kufuata Biblia

“Msipite mambo yaliyoandikwa,” Biblia inasema. (1 Wakorintho 4:6) Kwa kusikitisha, watu wanapopuuza maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu, wanapata madhara ya kiroho, na hivyo ndivyo ilivyo kunapokuwa na tofauti kati ya makasisi na waumini. Kwa njia gani? Tafadhali fikiria hoja sita zifuatazo.

1. Kuwapo kwa jamii ya makasisi kunamaanisha kwamba lazima mtu awe na mwito wa pekee ili awe mtumishi wa Mungu. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba Wakristo wote wa kweli wanapaswa kumtumikia Mungu na kulisifu jina lake. (Waroma 10:9, 10) Na inapohusu kuhudumu ndani ya kutaniko, wanaume Wakristo kwa ujumla wanatiwa moyo wafikie pendeleo hilo, kama ilivyo kawaida ya Mashahidi wa Yehova.—1 Timotheo 3:1.

2. Tofauti kati ya makasisi na waumini hukweza jamii ya makasisi, kama inavyoonyeshwa na majina yao ya cheo. Hata hivyo, Yesu alisema: “Anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mkuu.” (Luka 9:48) Kupatana na roho hiyo ya unyenyekevu, aliwaambia wafuasi wake wasiitwe majina ya cheo ya kidini.—Mathayo 23:8-12.

3. Jamii ya makasisi inayolipwa inaweza kuwalemea waumini kifedha, hasa ikiwa makasisi wanaishi maisha ya juu. Tofauti na hilo, waangalizi Wakristo wanashughulikia mahitaji yao ya kifedha kwa kufanya kazi na hivyo kuwawekea wengine mfano mzuri. *Matendo 18:1-3; 20:33, 34; 2 Wathesalonike 3:7-10.

4. Kwa kuwa huenda kasisi akawa anawategemea wengine ili apate msaada wa kifedha, anaweza kushawishiwa apunguze uzito wa ujumbe wa Biblia ili awapendeze waumini. Kwa kweli, Maandiko yalitabiri kwamba jambo hilo lingetendeka. “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe.”—2 Timotheo 4:3.

5. Tofauti kati ya makasisi na waumini hufanya waumini wawaachie makasisi mambo ya dini, huku wao wakija tu kusikiliza mahubiri kila juma. Hata hivyo, Wakristo wote wanapaswa kutambua uhitaji wao wa kiroho na kuwa wanafunzi wazuri wa Biblia.—Mathayo 4:4; 5:3.

6. Wakati ambapo waumini hawajui kile ambacho Biblia inasema, wanaweza kudanganywa kwa urahisi na viongozi wa kidini, na hata kutumiwa vibaya. Kwa kweli, historia ina mifano mingi ya mambo hayo. *Matendo 20:29, 30.

Ili kufuata kwa ukaribu yale ambayo Biblia inasema, Mashahidi wa Yehova hawana makasisi wanaolipwa, bali wana wachungaji na walimu wa kiroho ambao hulihudumia kundi la Mungu kwa hiari. Mbona usijionee jambo hilo kwa kutembelea Jumba la Ufalme lililo karibu nawe?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Katika karne ya kwanza, waangalizi fulani wanaosafiri ‘waliishi kwa njia ya habari njema’ nyakati fulani kwa kukubali ukarimu na michango iliyotolewa kwa hiari.—1 Wakorintho 9:14.

^ fu. 16 Mifano ya mambo hayo inatia ndani malipo ya kupata msamaha, Baraza la Kikatoliki la Kuhukumu Wazushi, na pia kuchomwa kwa Biblia nyingi na makasisi ambao hawakutaka Neno la Mungu lisomwe na waumini wao.—Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 2002 (15/11/2002), ukurasa wa 27.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, kunapaswa kuwa na tofauti yoyote kati ya watu wote wa Mungu?—Mathayo 23:8.

▪ Wanaume Wakristo wanastahili jinsi gani kutumika wakiwa waangalizi ndani ya kutaniko?—1 Timotheo 3:1-7.

▪ Kwa nini Mungu hakubali kuwe na tofauti kati ya makasisi na waumini?—1 Wakorintho 4:6.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Tofauti na makasisi, Yesu alijiendesha kama “aliye mdogo zaidi”