Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutendewa Kama Mtu Asiye na Maana

Kutendewa Kama Mtu Asiye na Maana

Kutendewa Kama Mtu Asiye na Maana

“Katika mwaka wangu wa kwanza katika shule ya msingi nchini Hispania watoto wengine darasani walinibandika majina kwa sababu nilikuwa mfupi sana. Kila siku nilikuwa nikienda nyumbani nikilia.”—Jennifer, binti ya wahamiaji Wafilipino.

“Nilipohamia shule mpya, wanafunzi wenzangu wazungu waliniita majina ya kunishushia heshima. Nilijua walitaka nipigane nao. Hata hivyo, nilijidhibiti lakini nilihisi vibaya na kwamba sifai.”—Timothy, Mmarekani mwenye asili ya Kiafrika.

“Nilipokuwa na umri wa miaka saba, Waigbo na Wahausa nchini Nigeria walikosana. Chuki yao iliniathiri, na nikaanza kumdhihaki mvulana darasani mwetu ambaye ni Mhausa, ingawa mbeleni tulikuwa marafiki wakubwa.”—John, wa kabila la Igbo.

“Mimi na mmishonari mwenzangu tulikuwa tukiwahubiria majirani ujumbe wa Biblia wakati watoto waliochochewa na viongozi wa kidini wa eneo hilo walipoanza kutufuata na kututupia mawe. Viongozi wa kidini walitaka tuondoke.”—Olga.

JE, UMEWAHI kushushiwa heshima kwa kubaguliwa isivyo haki? Huenda ilikuwa kwa sababu ya rangi, dini, hali ya kiuchumi, jinsia, au umri wako. Wale ambao hubaguliwa kwa ukawaida wanaishi wakiogopa kutendewa vibaya hata zaidi. Huenda wakashikwa na wasiwasi mwingi sana wanapotembea mahali palipo na kikundi fulani cha watu, wanapoingia ndani ya duka, wanapohamia shule mpya, au wanapoalikwa kwenye sherehe fulani.

Isitoshe, watu wanapochukiwa na kubaguliwa inaweza kuwa vigumu kupata kazi, au wapate matibabu na masomo ya hali ya chini, au wanyimwe huduma au haki wanazopewa raia wengine. Wenye mamlaka wanapounga mkono ubaguzi, mambo mabaya kama vile mauaji ya kikabila na maangamizi ya jamii nzimanzima yanaweza kutokea. Mfano mmoja wa kale wa jaribio la kuangamiza jamii nzima unapatikana katika kitabu cha Biblia cha Esta. Ona jinsi chuki na ubaguzi zilivyochangia jambo hilo.—Esta 3:5, 6.

Ubaguzi na chuki unaweza kuendelezwa hata katika maeneo ambako kuna sheria zinazoupinga. Aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Haki za Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa anasema hivi: “Miaka 60 baada ya Azimio la Haki za Kibinadamu kwa Wote . . . , bado ulimwengu haujawa na usawa na watu hawajaacha kuwa na ubaguzi.” Hilo ni jambo la kusikitisha, kwa kuwa wahamiaji na wakimbizi wameongezeka na kubadili sana idadi ya watu katika nchi nyingi.

Je, kweli inawezekana kuwa na jamii yenye usawa? Au je, ubaguzi unaweza kumalizwa? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.