Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kukabilianaje na Kifo cha Mzazi?

Ninaweza Kukabilianaje na Kifo cha Mzazi?

Vijana Huuliza

Ninaweza Kukabilianaje na Kifo cha Mzazi?

“Mama yangu alipokufa, nilihisi nimechanganyikiwa. Yeye ndiye aliyeunganisha familia yetu.”—Karyn. *

NI MAMBO machache sana maishani yanayoweza kumwathiri mtu zaidi kuliko kifo cha mzazi. Zaidi tu ya uchungu mwingi unaopata, wakati wako ujao utakuwa tofauti na ulivyotarajia.

Huenda ulitazamia kwamba mama au baba yako mpendwa atakuwapo utakapomaliza shule au kwamba angeshiriki shangwe ya siku yako ya arusi. Sasa, matumaini hayo yamepotelea mbali, yakikuacha ukiwa umehuzunika, umekata tamaa, au hata ukiwa umekasirika. Unaweza kukabilianaje na hisia nyingi zinazotokana na kufiwa na mzazi?

‘Je, Ni Kawaida Kuhisi Hivi?’

Unaporudiwa na fahamu na kutambua kwamba mama au baba yako amekufa, huenda ukalazimika kukabiliana na hisia mbalimbali ambazo hujawahi kuzipata. Brian aliyekuwa na umri wa miaka 13 tu baba yake alipokufa kutokana na mshtuko wa moyo, anasema, “Usiku ule tuliopata habari, tulilia na kukumbatiana tu.” Natalie aliyekuwa na umri wa miaka kumi baba yake alipokufa kutokana na kansa, anakumbuka: “Nilichanganyikiwa sana. Kwa hiyo ni kana kwamba sikuhisi chochote. Ni kama nilikufa ganzi.”

Kifo humwathiri kila mtu kwa njia tofauti. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba “kila mmoja” ana “pigo lake na maumivu yake mwenyewe.” (2 Mambo ya Nyakati 6:29) Ukiwa na hilo akilini, hebu fikiria jinsi ambavyo kifo cha mzazi wako kimekuathiri wewe. Andika hapa chini (1) jinsi ulivyohisi ulipojua kwamba mzazi wako amekufa na (2) jinsi unavyohisi sasa. *

(1) ․․․․․

(2) ․․․․․

Huenda majibu yako yanaonyesha kwamba hisia zako zinapungua kwa kadiri fulani. Hilo ni jambo la kawaida. Halimaanishi eti umemsahau mzazi wako. Kwa upande mwingine, huenda bado ukawa unahisi uchungu au uchungu umeongezeka. Huenda huzuni yako huja kama mawimbi ambayo yanapungua kisha yanapiga ufuo bila kutazamiwa. Hilo pia ni jambo la kawaida—hata ikiwa linatukia miaka kadhaa baada ya kifo cha mzazi. Swali ni, Unaweza kukabilianaje na huzuni?

Njia za Kukabiliana na Hisia Zako

Usijizuie kulia! Kulia kunasaidia kupunguza uchungu wa kufiwa. Hata hivyo, huenda ukahisi kama Alicia, aliyekuwa na umri wa miaka 19 mama yake alipokufa. Anasema hivi, “Nilihisi kwamba nikionyesha hisia nyingi, wengine watafikiri sina imani.” Lakini fikiria hili: Yesu Kristo alikuwa mwanadamu mkamilifu aliyekuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Hata hivyo, ‘alitokwa na machozi’ rafiki yake mpendwa Lazaro alipokufa. (Yohana 11:35) Hivyo, usiogope kulia. Hilo halimaanishi kwamba huna imani! Alicia anasema: “Mwishowe, nililia. Nililia sana. Kila siku.” *

Kabiliana na hisia za hatia. “Kila siku nilienda kumbusu mama yangu na kumwambia awe na usiku mwema,” anasema Karyn, aliyekuwa na umri wa miaka 13 mama yake alipokufa. “Siku moja sikufanya hivyo. Asubuhi iliyofuata, Mama alikufa. Najua sipaswi kuwa na hisia za hatia, lakini ninajihisi nina hatia kwa kuwa sikumwona usiku huo wa mwisho na pia kwa sababu ya mambo yaliyotukia siku iliyofuata. Baba yangu alikuwa ameenda safari ya kikazi na aliniomba mimi na dada yangu tumtunze Mama. Lakini tuliamka tukiwa tumechelewa. Nilipoingia chumbani mwake, Mama hakuwa akipumua. Nilihisi vibaya sana, kwa sababu alikuwa sawa Baba alipoondoka!”

Kama Karyn, huenda kwa kiasi fulani unahisi hatia kwa mambo ambayo ulipuuza kufanya. Huenda hata ukajitesa kwa kujuta. ‘Laiti ningemhimiza Baba amwone daktari.’ ‘Laiti ningeenda kumwona Mama mapema.’ Ikiwa mawazo kama hayo yanakusumbua, kumbuka hili: Ni jambo la kawaida kujuta kwamba ungefanya mambo kwa njia tofauti. Ukweli wa mambo ni kwamba ungefanya mambo kwa njia tofauti ikiwa tu ungejua mambo ambayo yangetokea. Lakini hukujua. Hivyo, hupaswi kuhisi hatia. Hukusababisha kifo cha mzazi wako! *

Zungumza kuhusu hisia zako. Methali 12:25 inasema: ‘Neno jema huchangamsha.’ (Biblia Habari Njema) Kufungia hisia zako kunaweza kufanya iwe vigumu kwako kukabiliana na huzuni. Kwa upande mwingine, kuzungumza kuhusu hisia zako na mtu unayemwamini kutakuwezesha kupata ‘maneno mema’ yenye kutia moyo wakati una huzuni. Hivyo, mbona usijaribu mojawapo ya mapendekezo yafuatayo?

Zungumza na mzazi wako. Ingawa mzazi wako anakabiliana na hali ngumu, bila shaka angependa kukupa msaada unaohitaji. Hivyo mwambie jinsi unavyohisi. Mazungumzo kama hayo yatafanya upate kitulizo na pia mtakuwa na uhusiano wa karibu zaidi.

Ili uanzishe mazungumzo, jaribu kufanya hivi: Orodhesha mambo mawili au matatu ambayo unatamani ungejua kumhusu mzazi aliyekufa, kisha umwombe mzazi mzungumzie mambo hayo. *

․․․․․

Zungumza na marafiki wa karibu. Biblia inasema kwamba rafiki wa kweli ‘wamezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.’ (Methali 17:17) “Huenda mtu ambaye hukutarajia ndiye atakayekusaidia,” anasema Alicia. “Hivyo usiogope kufunua hisia zako.” Ni kweli kwamba huenda ikawa vigumu kuzungumzia mambo hayo, si rahisi kwako na rafiki yako kupata maneno yanayofaa. Hata hivyo, mwishowe itakuwa vema kuzungumza na wengine kuhusu huzuni yako. David aliyekuwa na umri wa miaka tisa tu baba yake alipokufa kutokana na mshtuko wa moyo anasema hivi: “Nilifungia hisia zangu moyoni. Ningefaidika ikiwa ningezungumzia hisia zangu. Ingenisaidia sana kukabiliana na huzuni yangu.”

Zungumza na Mungu. Inaelekea kwamba utahisi vizuri zaidi baada ya ‘kummiminia’ Yehova Mungu ‘moyo wako’ katika sala. (Zaburi 62:8) Hiyo si njia ya kukutuliza tu. Unaposali, unamsihi “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

Njia moja ambayo Mungu anatumia kutufariji ni kupitia roho yake takatifu. Inaweza kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida,” ili uvumilie uchungu wa kufiwa. (2 Wakorintho 4:7) Pia Mungu anatupa “faraja kutokana na Maandiko.” (Waroma 15:4) Hivyo mwombe Mungu akupe roho yake, na utumie wakati kusoma kitia-moyo kilicho katika Neno lake, Biblia. (2 Wathesalonike 2:16, 17) Kwa nini usiweke orodha ya maandiko ambayo yanakufariji? *

Uchungu Ninaohisi Utawahi Kwisha?

Huzuni inachukua muda kwisha. “Si kana kwamba unaweza tu kuamua kutohisi,” anasema Brianne aliyekuwa na umri wa miaka 16 mama yake alipokufa. “Mara nyingine mimi hulia hadi nilale. Nyakati nyingine badala ya kufikiria sana kifo cha mama yangu, mimi hujaribu kukazia fikira mambo ambayo Yehova ameahidi nitafurahia pamoja na mama yangu katika paradiso.”

Biblia inatuhakikishia kwamba katika Paradiso ambayo Brianne alitaja, “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4) Huenda kutafakari ahadi hizo kukakusaidia pia kukabiliana na kifo cha mzazi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 8 Ikiwa ni vigumu kwako kujibu maswali hayo sasa, unaweza kujaribu kufanya hivyo baadaye.

^ fu. 13 Usifikiri kwamba ni lazima ulie ili kuonyesha huzuni yako. Watu huonyesha huzuni kwa njia mbalimbali. Jambo muhimu ni hili: Ukihisi unataka kulia, tambua kwamba huo ni “wakati wa kulia.”—Mhubiri 3:4.

^ fu. 15 Mawazo kama hayo yakiendelea kukusumbua, zungumza na mzazi wako au mtu mwingine mzima. Baada ya muda, utakuwa na mtazamo wenye usawaziko.

^ fu. 18 Ikiwa ulilelewa na mzazi asiye na mwenzi au ikiwa kwa sababu fulani huishi na mzazi wako, unaweza kuzungumza na mtu mzima aliyekomaa.

^ fu. 22 Watu fulani wamefarijiwa na maandiko yafuatayo: Zaburi 34:18; 102:17; 147:3; Isaya 25:8; Yohana 5:28, 29.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Utatumia mapendekezo gani yaliyo katika makala hii? ․․․․․

▪ Hapa chini, andika maandiko machache yatakayokufariji unapolemewa na huzuni. ․․․․․

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

NI SAWA KULIA . . . WALILIA!

Abrahamu—Mwanzo 23:2.

Yosefu—Mwanzo 50:1.

Daudi—2 Samweli 1:11, 12; 18:33.

Maria, dada ya Lazaro—Yohana 11:32, 33.

Yesu—Yohana 11:35.

Maria Magdalene—Yohana 20:11.

ANDIKA HISIA ZAKO

Kuandika mawazo yako kuhusu mzazi aliyekufa kunaweza kukusaidia sana kukabiliana na huzuni. Kuna mambo mengi unayoweza kuandika. Yafuatayo ni mapendekezo machache.

▪ Andika pindi nzuri ulizofurahia na mzazi wako.

▪ Andika mambo ambayo ungemwambia mzazi wako alipokuwa hai.

▪ Wazia kwamba una ndugu au dada mdogo ambaye anakabiliana na hisia za hatia kuhusu kifo cha mzazi wako. Andika mambo ambayo ungesema ili umfariji. Hilo linaweza kukusaidia uwe na usawaziko kuhusu hisia zako za hatia.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

TAARIFA KWA MZAZI

Ni jambo linaloumiza sana kumpoteza mwenzi wako wa ndoa. Hata hivyo, amekufa wakati ambapo kijana wako anahitaji msaada wako. Unaweza kumsaidiaje akabiliane na huzuni, bila kupuuza hisia zako?

Usifiche hisia zako. Mtoto wako amejifunza masomo muhimu zaidi maishani mwake kwa kukutazama. Pia atajifunza kukabiliana na huzuni kwa kukutazama. Kwa hiyo, usione kwamba unapaswa kuficha hisia zako ili mtoto wako aone una nguvu. Ukifanya hivyo utamfundisha kijana wako kuficha hisia zake pia. Tofauti na hilo, unapoonyesha hisia zako, atajifunza kwamba ni afadhali kuonyesha hisia badala ya kuzificha na kwamba ni jambo la kawaida kwake kujihisi amehuzunika, amekata tamaa, au hata amekasirika.

Mtie moyo kijana wako azungumze. Bila kumshinikiza mtoto wako, mtie moyo akueleze yaliyo moyoni. Akisitasita, mnaweza kuzungumzia makala hii pamoja? Pia, zungumza kuhusu pindi ulizofurahia pamoja na mwenzi wako aliyekufa. Mweleze kwamba unajua haitakuwa rahisi kwako kuvumilia. Kijana wako anapokusikia ukizungumza kuhusu hisia zako itakuwa rahisi kwake kufanya hivyo pia.

Tambua mipaka yako. Inaeleweka kwamba ungependa kumtegemeza mtoto wako katika pindi hii ngumu. Lakini kumbuka, umeathiriwa sana na kifo cha mwenzi wako mpendwa. Kwa hiyo, hisia zako zimeathiriwa na nguvu zako za kiakili na za kimwili zimeathiriwa kwa kadiri fulani. (Methali 24:10) Hivyo, utahitaji kuomba msaada wa watu wengine wa familia na marafiki wakomavu. Kuomba msaada ni ishara ya ukomavu. Methali 11:2 inasema: “Wenye kiasi wana hekima.”

Msaada bora zaidi unaoweza kupata unatoka kwa Yehova Mungu ambaye anawaahidi hivi waabudu wake: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isaya 41:13.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Huenda huzuni yako huja kama mawimbi ambayo yanapungua kisha yanapiga ufuo bila kutazamiwa