Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo Hushinda Chuki

Upendo Hushinda Chuki

Upendo Hushinda Chuki

“Jamii mpya ya kidini ilitokea kwa mara ya kwanza katika historia: si kikundi fulani kinachoendeleza utaifa, lakini kikundi cha wajitoleaji ambao wameshinda tofauti za kijamii, rangi, na kitaifa: wanaume kwa wanawake wakiungana kwa usawa mbele ya mungu wao.”—Kitabu cha Paul Johnson, A History of Christianity.

UKRISTO wa kweli ulipoenea kotekote katika Milki ya Roma, watu waliona jambo la kushangaza—familia ya kimataifa ya watu wanaomwabudu Mungu ambao wamejifunza kuishi pamoja kwa amani ya kweli na umoja. Siri ya “familia” hiyo kuwa na amani ilikuwa upendo wa kweli uliotegemea kanuni za Mungu wala si hisia tu.

Yesu Kristo alifundisha kanuni hizo kwa maneno na matendo, ingawa yeye mwenyewe alibaguliwa sana na kuchukiwa. (1 Petro 2:21-23) Kwanza, alitoka eneo la Galilaya, na Wagalilaya ambao wengi wao walikuwa wakulima na wavuvi walidharauliwa na viongozi wa kidini Wayahudi huko Yerusalemu. (Yohana 7:45-52) Pia, Yesu alikuwa mwalimu stadi ambaye alipendwa na kuheshimiwa na watu wa kawaida. Kwa sababu hiyo, viongozi wa kidini walimwonea wivu hivi kwamba wakaeneza habari za uwongo kumhusu na hata wakapanga njama ya kumwua!—Marko 15:9, 10; Yohana 9:16, 22; 11:45-53.

Hata hivyo, Yesu ‘hakulipa uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Kwa mfano, Mafarisayo—waliokuwa washiriki wa dini ya Kiyahudi iliyompinga Yesu—walipomwendea wakiwa mmoja-mmoja kwa unyoofu na kumwuliza maswali, aliwajibu kwa fadhili. (Yohana 3:1-21) Hata alikula pamoja na Mafarisayo, kutia ndani mmoja ambaye alimbagua Yesu. Jinsi gani? Katika siku hizo ilikuwa kawaida kuosha miguu ya mgeni; lakini Farisayo huyo hakumwosha Yesu miguu. Je, Yesu alikasirika? Hapana. Alitumia jioni hiyo kuwafundisha jambo muhimu kuhusu huruma na kusamehe.—Luka 7:36-50; 11:37.

Yesu Aliwapenda Waliodharauliwa

Moja kati ya mifano ya Yesu inayojulikana zaidi, ni ile ya Msamaria mwema ambaye alitoa pesa zake mwenyewe kumsaidia Myahudi ambaye alikuwa amepigwa na kunyang’anywa mali zake. (Luka 10:30-37) Kwa nini tendo la Msamaria huyo lilikuwa jema sana? Wayahudi na Wasamaria walidharauliana. Kwa kweli, neno “Msamaria” mara nyingi lilitumiwa na Wayahudi kumshushia mtu heshima, hata Yesu mwenyewe aliitwa hivyo wakati mmoja. (Yohana 8:48) Chini ya hali hizo, mfano wa Yesu wa kuwapenda majirani bila ubaguzi ulikuwa wenye nguvu kama nini.

Matendo ya Yesu yalithibitisha jambo hilo kwa kumponya Msamaria mwenye ukoma. (Luka 17:11-19) Isitoshe, Yesu alizungumza kwa muda mrefu na mwanamke Msamaria, na hilo lilikuwa tukio la maana sana. (Yohana 4:7-30, 39-42) Kwa nini? Marabi Wayahudi walioshikilia sana sheria hawangezungumza na mwanamke yeyote hadharani, hata awe mtu wa ukoo wa karibu, sembuse mwanamke Msamaria!

Lakini, Mungu anamwonaje mtu mwenye ubaguzi anayejitahidi kuondoa hisia hizo moyoni mwake? Biblia inasema mambo yenye kufariji kuhusu jambo hilo.

Mungu Ni Mwenye Subira Kwetu

Katika karne ya kwanza, Wakristo wengi Wayahudi waliathiriwa na maoni yenye ubaguzi kuelekea watu wasio Wayahudi, ambao wengi wao waligeuka na kuwa waamini. Yehova Mungu alishughulikiaje jambo hilo ambalo lingeweza kuwagawanya watu? Alilifundisha kutaniko la Kikristo kwa subira. (Matendo 15:1-5) Subira hiyo ilikuwa na matokeo mazuri, kwa kuwa kama ilivyotajwa mwanzoni mwa makala hii, ‘walishinda tofauti za kijamii, rangi, na kitaifa.’ Kwa sababu hiyo, “makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka hesabu siku baada ya siku.”—Matendo 16:5.

Tunajifunza nini? Usikate tamaa, lakini endelea kumwomba Mungu msaada kwa kuwa yeye anawapa hekima na nguvu za kufanya yaliyo sawa wale ‘wanaoendelea kuomba kwa imani.’ (Yakobo 1:5, 6) Je, unawakumbuka Jennifer, Timothy, John, na Olga waliotajwa katika makala ya kwanza ya mfululizo huu? Jennifer alipoenda kwenye shule ya sekondari, alikuwa amekomaa kiroho na alikuwa amejifunza kupuuza matusi kuhusu rangi na kimo chake. Muda mfupi baadaye, msichana mwingine alipotukanwa mara nyingi na wanafunzi wenzake, Jennifer alimtetea na kumfariji.

Ni nini kilichomsaidia Timothy kuwa mtulivu wanafunzi wenzake walipomtukana kwa sababu ya rangi yake? Anasema: “Sikutaka kuliletea suto jina la Yehova Mungu. Pia nilikumbuka kwamba tunapaswa ‘kuendelea kuushinda uovu kwa wema’ na kutoruhusu uovu utushinde.”—Waroma 12:21.

John alishinda hisia zake za ubaguzi dhidi ya mwanafunzi mwenzake ambaye ni Mhausa. “Nilipokuwa kijana,” anasema, “nilikutana na wanafunzi Wahausa na tukawa marafiki. Nilifanya mradi mmoja wa shule pamoja na mmoja wao, na tulipatana sana. Sasa ninajitahidi kuwaona watu jinsi walivyo, si kwa kutegemea rangi au kabila lao.”

Olga na mmishonari mwenzake hawakuogopa walipoteswa na wapinzani wenye chuki, lakini waliendelea kuwa imara, wakiwa na uhakika kwamba watu fulani watathamini ujumbe wa Biblia. Wengi waliuthamini. “Miaka 50 hivi baadaye,” anasema Olga, “mwanamume mmoja alinipa mfuko maridadi sana. Ndani yake kulikuwa na mawe madogo yaliyokuwa yameandikwa sifa za Kikristo kama vile wema, fadhili, upendo, na amani. Kisha aliniambia kwamba alikuwa mmoja wa wale wavulana walionitupia mawe na sasa yeye ni ndugu yangu Mkristo. Yeye na mke wake wakanipa maua meupe 24 ya waridi pamoja na ule mfuko wenye mawe.”

Wakati Ubaguzi Hautakuwapo Tena!

Hivi karibuni hakutakuwa na chuki na ubaguzi. Hilo litawezekanaje? Kwanza, dunia itakuwa na Mtawala mmoja, yaani, Yesu Kristo, ambaye alionyesha kwamba “hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu.” (Isaya 11:1-5) Isitoshe, raia wa kidunia wa Yesu wataiga kikamilifu mtazamo wake, kwa kuwa yeye na Baba yake, Yehova Mungu, watakuwa wamewafundisha.—Isaya 11:9.

Elimu hiyo ya kiroho inaendelea sasa, ikiwatayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya maisha katika mfumo mpya kabisa wa mambo. Kwa hiyo, tunakutia moyo ujiunge na mpango huo wa kujifunza Biblia bila malipo. * Naam, Mungu hana ubaguzi; ni mapenzi yake kwamba watu wa namna zote “waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Ikiwa ungependa kujifunza Biblia bila malipo wakati na mahali panapokufaa, twakualika uwasiliane na Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme au mojawapo ya ofisi za tawi zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5. Au uwasiliane na Mashahidi wa Yehova kwenye kituo cha Intaneti www.watchtower.org.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Hivi karibuni wanadamu hawatatatizwa na chuki na ubaguzi

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa8, 9]

KANUNI ZA MUNGU TUNAZOPASWA KUFUATA

“Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:17-21) Tunajifunza nini? Wengine wakikutendea mambo mabaya, jifunze kuwatendea kwa njia nzuri. “Walinichukia bila sababu,” alisema Yesu Kristo. Hata hivyo, yeye hakuwachukia.—Yohana 15:25.

“Na tusiwe wenye kujisifu, . . . tukioneana wivu.” (Wagalatia 5:26) Wivu na kiburi hudhuru hali ya kiroho, na mara nyingi humfanya mtu awe na chuki na ubaguzi.—Marko 7:20-23.

“Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Jiulize, ‘Ningependa kutendewa jinsi gani?’ Watendee watu wengine kwa njia hiyo, haidhuru wana umri, rangi, utamaduni au wanazungumza lugha gani.

“Mkaribishane, kama vile Kristo pia alivyotukaribisha sisi.” (Waroma 15:7) Je, wewe hujaribu kuwafahamu watu wa malezi na utamaduni mbalimbali, hasa ikiwa wao ni watumishi wenzako wa Mungu?—2 Wakorintho 6:11.

“Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zaburi 27:10) Hata wengine wakutendee namna gani, Mungu hatakuacha kamwe ukiendelea kuwa mshikamanifu kwake.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Msamaria mwenye ujirani anamsaidia Myahudi ambaye amevamiwa na wanyang’anyi