Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Watu Wabaya Watateketezwa Milele?

Je, Watu Wabaya Watateketezwa Milele?

Maoni ya Biblia

Je, Watu Wabaya Watateketezwa Milele?

GERTRUDE, ambaye ni mhubiri katika kanisa la Pentekoste, ameshikilia kwamba kuna moto wa mateso. Kusema tu kwamba hakuna mahali kama hapo kulikuwa kinyume cha kile alichoamini kuwa haki. Alisema kwamba kama hakungekuwa na moto wa mateso, watu wanaofanya mambo ya kikatili hawangeadhibiwa. Gertrude bado anashikilia imani yake. Anasema hivi, “Sidhani ningependa kumwabudu Mungu ikiwa hakuna moto wa mateso wa kuwaadhibu waovu.”

Je, watu wabaya watateketezwa milele, kama dini nyingi zinavyofundisha? Ikiwa hawatateketezwa, wataadhibiwaje?

Mara ya Kwanza Mungu Kumwadhibu Mwanadamu

Kulingana na Biblia, Mungu aliwaumba watu wawili wa kwanza wakiwa wakamilifu. (Mwanzo 1:27; Kumbukumbu la Torati 32:4) Aliwaweka katika bustani ya paradiso na kuwapa nafasi ya kuishi milele. Hata hivyo, wanadamu hao wa kwanza, Adamu na Hawa, waliwekewa sheria moja. Mungu aliwaonya hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.”—Mwanzo 2:16, 17.

Kwa kusikitisha, wazazi wetu wa kwanza walishindwa kudumisha ushikamanifu na hawakutii. Muumba alilazimika kuwapa hukumu ya kifo. “Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”—Mwanzo 3:19.

Kama Adamu na Hawa wangeadhibiwa kwa kuteketezwa, je, Mungu hangewaambia kuhusu adhabu hiyo? Ukweli wa mambo ni kwamba Mungu hakutaja chochote kuhusu kuteseka baada ya kufa. Hawangeteseka. Hawakuwa na nafsi isiyoweza kufa. Biblia inasema hivi waziwazi: “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.”Ezekieli 18:4. *

Akiwa Mpaji wa uhai, Muumba wetu anajua kila kitu kuhusu uzima na kifo. Anatuambia katika Neno lake kwamba “wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Hiyo ndiyo sababu Adamu na Hawa hawangeteseka katika moto wa mateso baada ya kufa. Walirudi tu mavumbini na hawakuendelea kuwapo. ‘Hawakujua lolote kamwe.’

Je, Tunaweza Kuteseka Baada ya Kufa?

Biblia inasema hivi katika Waroma 5:12: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote.” Hivyo basi, je, inapatana na akili kuamini kwamba watu huteseka katika moto kwa sababu ya dhambi zao, ingawa Adamu ambaye aliletea wanadamu wote dhambi alikuwa mavumbi baada ya kufa?—1 Wakorintho 15:22.

Sisi sote tulikuja kuwa chini ya sheria moja kama Adamu. “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” Isitoshe, mtu akifa, “ameondolewa hatia ya dhambi yake.” (Waroma 6:7, 23) Ikiwa wote, wazuri na wabaya wanakufa na hakuna anayeteseka baada ya kufa, je, Mungu atatenda kwa haki?

Hukumu ya Mungu ya Haki

Kusudi la Mungu kwa wanadamu watiifu halijabadilika tangu aumbe wanadamu wawili wa kwanza na kuwaagiza wazae watoto na kuitunza dunia. (Mwanzo 1:28) Hilo bado ndilo kusudi lake, kama alivyotangaza baadaye: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29.

Ona kwamba waadilifu wataishi katika dunia hii. Wataishi kwa afya kamilifu na furaha. Kusudi la awali la Mungu kwamba dunia ijae jamii ya wanadamu waadilifu “hakika litafanikiwa.” Hilo litatendeka atakapoondoa mfumo huu mwovu wa mambo na kuleta ulimwengu mpya.—Isaya 55:11; Danieli 2:44; Ufunuo 21:4.

Mabilioni ya watu waliokufa bila kujua matakwa ya Mungu watafufuliwa na kufundishwa katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Isaya 11:9; Yohana 5:28, 29) Kwa upande mwingine, yeyote atakayekataa kuishi kupatana na sheria za Mungu ataadhibiwa kwa “kifo cha pili.” Hicho ndicho kifo ambacho mtu hawezi kuamka.—Ufunuo 21:8; Yeremia 51:57.

Kwa wazi, akiwa Mungu wa upendo, Yehova hatawatesa watu katika moto wa mateso. (1 Yohana 4:8) Wala hatavumilia uovu milele. Kwa sababu hiyo, Zaburi 145:20 inatuhakikishia kwamba “Yehova anawalinda wale wote wanaompenda, lakini atawaangamiza waovu wote.” Je, hilo si jambo la upendo na haki?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Katika Biblia, “nafsi” humaanisha mtu mzima—si kitu tofauti na mwili wake. Mwanzo 2:7 linasema: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” Adamu hakupewa nafsi kando na mwili. Badala yake, Adamu mwenyewe alikuwa nafsi hai.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, tuna nafsi isiyoweza kufa?—Ezekieli 18:4.

▪ Wafu wako katika hali gani?—Mhubiri 9:5.

▪ Mungu atawaadhibuje waovu?—Zaburi 145:20.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Wafu, hawajui lolote kamwe.”—Mhubiri 9:5

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Photo: www.comstock.com