Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Vijana Wanavyoweza Kupata Msaada

Jinsi Vijana Wanavyoweza Kupata Msaada

Jinsi Vijana Wanavyoweza Kupata Msaada

Katika hali zinazofaa, wazazi wenye upendo wangewaelekeza na kuwafunza watoto wao. Wangezungumza, kusoma, kula pamoja nao, na kuwaelewa. Hata hivyo, wazazi si wakamilifu. Biblia inasema hivi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23.

Ikiwa wewe ni kijana, huenda ukahisi kwamba maisha ya nyumbani hayafai, na huenda ikawa hivyo. Hata hivyo, unaweza kufanya mengi ili kupunguza mahangaiko yako na kupata furaha zaidi. Ona jinsi kufuata kanuni za Biblia kunavyoweza kukusaidia.

Pendekezo la 1

Shirikiana na Watu na Usijitenge

“Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Vijana fulani hawajihisi huru wanapochangamana na watu na wanaona ni afadhali kutazama televisheni au kucheza mchezo wa video. Wengine ni wenye haya sana, kwa hiyo, wao hujitenga. Kijana anayeitwa Elizabeth anasema kwamba yeye huwa na “haya kila wakati.” Anasema hivi: “Hisia yangu ya haya ni kama tu woga. Ni vigumu sana kwangu kuwafikia watu na kuzungumza nao.”

Elizabeth alikabilianaje na tatizo hilo la kuwa na haya? Yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, naye huhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Elizabeth anasema: “Licha ya kuwa na haya, nimejiwekea mradi wa kuzungumza na mtu mmoja kila mkutano. Nikishindwa, sikati tamaa. Badala yake, mimi hukazia fikira mambo ninayotimiza. Ninaona kwamba nimefaidika sana kwa kuwafahamu wengine.”

Mbona usiandike majina ya watu wawili au watatu ambao ungependa kuwafahamu vizuri? Jiwekee mradi wa kujifunza jambo jipya kuhusu mmoja wao juma linalofuata. Andika jambo moja zuri unaloweza kumfanyia kila mmoja wao mwezi huu, na ulifanye.—Matendo 20:35.

Ukijitenga na watu au kwa sababu ya matatizo, utaanza kujifikiria sana kwa njia isiyofaa. Kwa upande mwingine, Biblia inatushauri kwamba ‘tuendelee kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yetu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Ukifuata kanuni hiyo unaposhughulika na familia yako na wengine, utakuwa na maoni yanayofaa kuhusu matatizo yako na utaweza kuyashughulikia kwa njia nzuri.

Pendekezo la 2

Ukimbie Uasherati

“Ukimbieni uasherati. Kila dhambi nyingine ambayo mtu huenda akafanya iko nje ya mwili wake, lakini yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 6:18) Unaweza kuepukaje kushinikizwa kufanya ngono haramu, zoea ambalo limeenea sana miongoni mwa vijana?

Kwanza, unahitaji kufikiria jambo hilo kabla ya kushinikizwa au kushawishiwa. “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake,” inasema methali moja yenye hekima. (Methali 14:15) Mbali, msichana anayeishi Afrika Kusini anasema hivi: “Nikiwa shule ya sekondari, mvulana fulani katika darasa langu aliniomba mara kwa mara niwe mpenzi wake. Wasichana katika darasa walinishinikiza nikubali kwa sababu alikuwa na sura yenye kuvutia, alikuwa mwanamitindo na alicheza katika timu ya mpira shuleni. Nilivutiwa naye, lakini tayari nilikuwa nimeamua kutovunja viwango vyangu vya maadili. Marafiki wangu hawakuona ubaya wowote wa kufanya ngono ovyoovyo. Lakini nilijua yaliyo sawa na makosa na nilikuwa nimeamua nitafanya nini nikikabili hali hiyo.”

Pili, sali kwa Mungu akusaidie kushikilia viwango vyake vya maadili. Maggie, kijana anayeishi Uingereza anasema hivi: “Sala hunisaidia kupata nguvu ninazohitaji kukabiliana na shinikizo la kufanya ngono. Sijawahi kufikiri kwamba ninaweza kubaliana na hali hiyo peke yangu. Pia mimi huzungumzia jambo hilo pamoja na wazazi wangu na nyakati nyingine huzungumzia tatizo hilo na marafiki wengine wakomavu.”

Pendekezo la 3

Elewa Hisia za Wazazi Wako

“Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo.” (1 Petro 3:8) Si wewe utakayeamua ikiwa wazazi wako watatengana au la, au kuamua ikiwa wote wawili watafanya kazi muda wote. Lakini kwa kadiri fulani wewe ndiye utakayeamua ikiwa utaruhusu hali hizo ziharibu uhusiano wako nao. Njia moja ya kupunguza wasiwasi na kuwa mwenye furaha zaidi ni kuwahurumia wazazi wako na kujaribu kuelewa matatizo wanayokabili.

Kijana anayeitwa Amber alifuata shauri hilo. Anakiri kwamba nyakati nyingine kuna hali ya kutoelewana, mfadhaiko, na kuudhika kati yake na mama yake. Hata hivyo, anasema hivi: “Mama yangu amepitia hali ngumu maishani. Ametulea sisi watoto wanne akiwa peke yake. Sikuzote ametuandalia makao, chakula, na mavazi. Ninashangazwa sana na nguvu zake, na ninatumaini kwamba nitatenda kama yeye ninapokabili matatizo.”

Ukijitahidi kujiweka katika hali ya wazazi wako na kuhisi kama wanavyohisi, itakusaidia kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu matatizo yako. Kufanya hivyo kutakusaidia pia utambue na kuiga sifa nzuri za wazazi wako.

Chanzo cha Mashauri Yanayotegemeka

Mapendekezo yaliyotajwa ni baadhi ya hekima inayopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Unapojifunza mengi zaidi kuhusu kitabu hiki, utathamini mashauri yake yanayotegemeka. *

Njia moja ambayo unaweza kujifunza mengi kuhusu Biblia ni kwa kushirikiana na Mashahidi wa Yehova na kujifunza pamoja nao. Utapata marafiki wa kweli miongoni mwao ambao watakutegemeza wakati wa shida na kukusaidia kufuata shauri la Biblia lenye hekima maishani. Bila shaka, si rahisi kuishi kupatana na viwango vya Biblia. Lakini ukichagua kufanya hivyo, utapata faida za kudumu.—Isaya 48:17, 18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ni chanzo kizuri sana cha mashauri ya Biblia yanayoweza kuwasaidia vijana kukabiliana na shinikizo wanalokabili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Vijana Wanahitaji Nini Kutoka kwa Wazazi?

Kuwa Pamoja na Wazazi: Yehova Mungu aliwaambia wazazi Waisraeli kwamba walipaswa kuzungumza na watoto wao mara nyingi—“unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Ili kufanya hivyo, wazazi wanahitaji kutumia wakati pamoja na watoto wao. Ni wazi kwamba Yesu alihisi anapaswa kutumia wakati wake pamoja na watoto. Kwa mfano, ‘watu walipoanza kumletea watoto wachanga ili awaguse,’ Yesu alifanya nini? “Alichukua watoto na kuanza kuwabariki.” (Marko 10:13, 16) Huo ni mfano mzuri sana kwa wazazi!

Zungumzeni kwa Unyoofu na Uhuru: Biblia inasema: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.” (Methali 15:22) Mazungumzo ya siri pamoja na watoto wako yalihitajika watoto walipokuwa wachanga. Mazungumzo hayo yanahitajika hata zaidi wakati wa ujana, wakati ambapo yaelekea vijana watatumia muda mchache nyumbani na kutumia muda mwingi pamoja na marafiki shuleni na kwingineko. Ikiwa hakutakuwa na mazungumzo ya siri, yaani, mazungumzo manyoofu na uhuru kati ya watoto na wazazi, vijana watawatendea wazazi wao kama watu wasiowajua.

Nidhamu Inayofaa: Nidhamu inamaanisha kurekebisha na kuzoeza, ingawa pia inaweza kutia ndani kutoa adhabu. “Yeyote aliye mpumbavu hudharau nidhamu ya baba yake, lakini mtu yeyote anayejali karipio ni mwerevu,” inasema Methali 15:5. Kijana hawezi ‘kujali karipio’ ikiwa halitolewi. Bila shaka, wazazi wanahitaji kuwa na usawaziko wanapowatia nidhamu vijana. Wanapaswa kuepuka kuwa wakali mno hivi kwamba wanawakasirisha watoto wao na huenda hata wakawafanya wasijiheshimu. (Wakolosai 3:21) Hata hivyo, wazazi hawapaswi kuwaendekeza watoto wao na kukosa kuwafundisha inavyofaa. Kuendekeza kunaweza kuwa na matokeo mabaya sana. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 29 Unaweza kupata habari zaidi kwenye sura ya 5 na 6 ya kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.