Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanakabili Matatizo Gani?

Vijana Wanakabili Matatizo Gani?

Vijana Wanakabili Matatizo Gani?

Je, matatizo ambayo vijana wa kizazi hiki wanakabili ni magumu sana kuliko ya vizazi vilivyopita? Ikiwa jibu lako ni la, huenda ukahisi kwamba vijana leo ni wenye furaha sana kuliko vijana wa vizazi vilivyopita.

Katika nchi nyingi, kuna dawa za kutibu magonjwa ambayo zamani yawaliwalemaza au kuwaua vijana. Tekinolojia imetokeza vifaa na vitu vya kuchezea vya elektroni ambavyo vizazi vilivyopita havikuwa navyo. Maendeleo ya kiuchumi yameboresha maisha ya familia nyingi zilizokuwa maskini. Kwa kweli, wazazi wengi sana wanafanya kazi kwa bidii ili kuwaandalia watoto wao makao na elimu bora ambayo wao wenyewe hawakupata.

Bila shaka, vijana leo wana mambo mengi mazuri. Lakini pia wanakabili matatizo mengi sana kuliko ilivyokuwa zamani. Sababu moja ni kwamba sasa wanadamu wanaishi katika kipindi ambacho Biblia inakiita “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3) Yesu Kristo alitabiri kwa usahihi kwamba kipindi hiki kingekuwa na migogoro mikubwa ya kijamii. (Mathayo 24:7, 8) Biblia inaita kipindi hichohicho kuwa “siku za mwisho” na inafafanua hali zilizopo katika jamii kuwa “ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Fikiria baadhi ya matatizo magumu kushughulika nayo yanayowakumba vijana leo.

Tatizo la 1

Vijana Wanazidi Kujitenga

Sinema, vipindi vya televisheni, na magazeti huonyesha vijana wakiwa wamezingirwa na marafiki kuanzia shuleni hadi wanapokuwa watu wazima. Hata hivyo, hali ni tofauti kabisa kwa vijana wengi.

Watafiti Barbara Schneider na David Stevenson, ambao walichanganua mahojiano yaliyofanyiwa maelfu ya vijana huko Marekani, waligundua kwamba “ni wanafunzi wachache sana ambao walidumisha marafiki au kikundi cha marafiki kwa kipindi kirefu.” Vijana wengi “hawana uhusiano na wengine na wana marafiki wachache sana ambao wanaweza kuwaeleza matatizo au mawazo yao,” wanasema Schneider na Stevenson.

Inaonekana kwamba vijana walio na marafiki hawana wakati wa kuwa pamoja nao. Uchunguzi mmoja wa kina nchini Marekani ulifunua kwamba vijana wengi sana hutumia asilimia 10 ya wakati wao wakiwa pamoja na marafiki wao lakini wanatumia asilimia 20 ya wakati wao peke yao, na huo ni muda mwingi kuliko ule wanaotumia wakiwa ama na familia au marafiki wao. Wanakula peke yao, wanasafiri peke yao, na kujifurahisha peke yao.

Kuongezeka kwa vifaa vya elektroniki kumechangia vijana kujitenga na wengine. Kwa mfano, katika mwaka wa 2006, gazeti Time liliripoti kwamba huko Amerika, vijana wenye umri wa kati ya miaka 8 na 18 walitumia kwa wastani saa sita na nusu kwa siku wakitazama televisheni, wasikiliza muziki kupitia vidude vinavyowekwa kwenye masikio, au wakicheza michezo ya video au kutumia kompyuta. *

Bila shaka, kizazi hiki si cha kwanza kutumia muda mwingi kufurahia muziki au kucheza. (Mathayo 11:16, 17) Lakini sasa wanatumia muda mwingi sana wakicheza na vifaa vya elektroni badala ya kushirikiana na watu wa familia na hilo linaweza kuwadhuru. Watafiti Schneider na Stevenson wanasema hivi: “Vijana hao wanasema kwamba wanapokuwa peke yao, hawajiheshimu, hawana furaha, hawafurahii wanachokifanya, na hawana mengi ya kufanya.”

Tatizo la 2

Kushinikizwa Wafanye Ngono

Vijana na watoto walio na umri wa chini ya miaka 13 wanashinikizwa sana wafanye ngono. Nathan, kijana anayeishi Australia anasema hivi: “Watoto wengi ninaowafahamu shuleni walianza kufanya ngono wakiwa na umri wa kati ya miaka 12 na 15.” Vinbay, msichana anayeishi Mexico, anasema kwamba kufanya ngono ovyoovyo lilikuwa jambo la kawaida sana kati ya vijana shuleni. “Vijana waliokataa kufanya ngono walionekana kuwa wa ajabu,” anasema Vinbay. “Kufanya ngono ovyoovyo ni jambo la kawaida kati ya vijana wenzangu hivi kwamba haitoshi kukataa mara moja tu,” anasema Ana, mwenye umri wa miaka 15 anayeishi Brazili. “Lazima ukatae tena na tena.”

Watafiti huko Uingereza walichunguza vijana 1,000 wenye umri wa kati ya miaka 12 na 19 kutoka malezi mbalimbali. Waligundua kwamba karibu nusu ya vijana hao walijihusisha na aina fulani ya ngono. Zaidi ya asilimia 20 ya vijana hao walikuwa na umri wa miaka 12 tu! Dakt. Dylan Griffiths, aliyesimamia utafiti huo anasema hivi: “Udhibiti ambao familia, kanisa, na mashirika mengine ulikuwa nao umepotea, na vijana ndio majeruhi.”

Je, kweli vijana wanaofanya ngono ni “majeruhi”? Katika ripoti iliyochapishwa mnamo 2003, watafiti Rector, Noyes, na Johnson walisema kwamba kushuka moyo na kuongezeka kwa visa vya kujaribu kujiua kumehusianishwa na vijana kufanya ngono. Walichanganua majibu ya vijana 6,500 waliohojiwa na wakagundua kwamba “kuna uwezekano mkubwa zaidi kwa wasichana wanaofanya ngono kushuka moyo kuliko wasichana wasiofanya ngono.” Na kati ya wavulana “kuna uwezekano maradufu wa wale wanaofanya ngono kushuka moyo kuliko wale wasiofanya ngono.”

Tatizo la 3

Familia Zilizovunjika

Vijana nchini Marekani wameona mabadiliko makubwa katika muundo wa familia na kubadilika kwa viwango katika jamii. “Katika miaka ambayo imepita kumekuwa na mabadiliko kadhaa makubwa ambayo yameathiri maisha ya vijana,” kinasema kitabu The Ambitious Generation—America’s Teenagers, Motivated but Directionless. “Ukubwa wa familia ya kawaida ya Marekani umepungua, kwa hiyo vijana hawana ndugu wengi kama zamani. Idadi ya talaka inapozidi kuongezeka, watoto wengi zaidi wanalelewa na mzazi mmoja. Na akina mama wengi wenye watoto walio chini ya umri wa miaka 18 wanafanya kazi, kwa hiyo mara nyingi hakuna mtu mzima nyumbani.”

Iwe watoto wanaishi na mzazi mmoja au wote wawili, wengi wanahisi kwamba wametengwa na wazazi wao wakiwa katika umri wanaowahitaji zaidi. Uchunguzi uliofanyiwa vijana 7,000 katika muda wa miaka kadhaa uligundua kwamba wengi wa vijana waliwaona wazazi wao kuwa wenye upendo na ufikirio. Hata hivyo, “ni asilimia 33 tu waliosema kwamba wanapata msaada wanapokuwa na tatizo.” Pia ripoti hiyo iligundua kwamba “kwa vijana wengi, matatizo hugunduliwa wakati ambapo wazazi hawawezi kutoa msaada wowote.”

Nchini Japani, vifungo imara vya familia vinazoroteshwa na tamaa ya kupata mali. Yuko Kawanishi, profesa wa sosholojia, anasema hivi: “Wazazi wengi wa vijana leo walizaliwa baada ya vita vya pili vya ulimwengu wakati watu walizaa watoto wengi, na walilelewa na viwango vipya vilivyokazia ufanisi wa kiuchumi na mali.” Wazazi hao wanafundisha watoto wao viwango gani? “Wazazi wengi leo wanahangaikia kufanikiwa kwa watoto wao kielimu,” anasema Kawanishi. “Maadamu watoto wao wanasoma,” anaendelea kusema, “mambo mengine nyumbani yanachukua nafasi ya pili, au hata hayazingatiwi.”

Vijana wanaweza kuathiriwaje wazazi wanapokazia fikira kupita kiasi ufanisi wa kiuchumi na elimu? Nchini Japani vyombo vya habari huzungumza mara nyingi kuhusu kireru—neno linalofafanua njia ambayo vijana hufoka ghafula kwa hasira wanaposhinikizwa kufanya vema. “Watoto wanapoanza kutenda kana kwamba wana kichaa,” akasema Kawanishi, “ni kwa sababu wanaona kwamba familia yao haiwezi kudhibiti tabia yao.”

Sababu za Kutazamia Mema

Kwa kweli, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, mbali na kutabiri kwamba watu wanaoishi wakati huu watakabili matatizo mengi, Biblia inazungumzia mambo mengine mengi.

Biblia inatoa mashauri yenye kujenga juu ya jinsi vijana wanavyoweza kuboresha maisha yao. Yehova Mungu, Mtungaji wa Biblia, anatamani sana kuwafundisha vijana jinsi ya kukabiliana na matatizo. (Methali 2:1-6) Anataka wawe na maisha mazuri. Neno lake linaweza “kuwapa werevu wale wasio na uzoefu, kumpa kijana ujuzi na uwezo wa kufikiri.” (Methali 1:4) Fikiria jinsi ambavyo kanuni za Biblia zinaweza kutusaidia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Vijana wanaojitenga vyumbani mwao wamekuwa wengi nchini Japani hivi kwamba wamepewa jina hikikomori. Watu fulani wanakadiria kwamba kuna hikikomori kati ya 500,000 na 1,000,000 huko Japani.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Kulingana na uchunguzi mmoja, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwa wasichana wanaofanya ngono kushuka moyo kuliko wasichana wasiofanya ngono

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Tabia Zenye Madhara

Ripoti ya serikali ya mwaka wa 2006 ilifunua kwamba nchini Uingereza idadi ya vijana walio na umri wa miaka 11 hadi 15 wanaotumia kokeini iliongezeka maradufu katika mwaka mmoja. Vijana 65,000 hivi walisema kwamba wamewahi kutumia dawa hiyo ya kulevya. Inasemekana kwamba nchini Uholanzi zaidi ya asilimia 20 ya vijana kati ya miaka 16 na 24 ni waraibu wa kileo kwa kadiri fulani au wana ugonjwa fulani unaosababishwa na kileo.

Vijana wengi huonyesha kwamba wana matatizo ya kihisia kwa kufanya mambo yanayodhuru miili yao moja kwa moja. Wanajikata, kujiuma, au kuchoma miili yao wenyewe. “Inakadiriwa kwamba Wamarekani milioni tatu wanajiumiza, na kijana mmoja kati ya 200 ana tatizo la kudumu la kujiumiza,” wanasema watafiti Len Austin na Julie Kortum.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Vijana wengi hawana marafiki wa karibu ambao wanaweza kuzungumza nao mambo ya kibinafsi