Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Familia Zilizofanikiwa—Sehemu ya Kwanza

Familia Zilizofanikiwa—Sehemu ya Kwanza

Familia Zilizofanikiwa—Sehemu ya Kwanza

Kama ambavyo toleo hili la pekee la Amkeni! limeonyesha, familia zilizofanikiwa zinapatwa pia na matatizo. Hilo si jambo lenye kushangaza, kwa kuwa tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Lazima matatizo ya aina moja au nyingine yatatokea katika kila familia.

Hata hivyo, kumbuka kwamba mafanikio hayategemei kuwa chini ya hali nzuri tu. Tofauti na hilo, Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Familia ambazo hutosheleza uhitaji wao wa kiroho kwa kufuata kanuni za Biblia zimegundua siri ya kupata mafanikio hata ingawa zinakabili hali ngumu. Fikiria mifano kadhaa.

Kumtunza mtoto mlemavu. Biblia inakazia sana kuwatunza watu wa familia, kutia ndani wale walio na mahitaji ya pekee. Inasema hivi: “Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.”—1 Timotheo 5:8.

Kwenye ukurasa wa 15, Victor, baba mmoja nchini Afrika Kusini, anasimulia jinsi ambavyo yeye na mke wake wamemtunza mtoto wao mlemavu kwa zaidi ya miaka 40.

Kulelewa na wazazi ambao si wako. Kanuni za Biblia zinaweza kumsaidia mtu ajiheshimu hata ingawa aliachwa na wazazi wake halisi. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba Yehova Mungu ni “msaidizi” wa wale wasio na baba.—Zaburi 10:14.

Kwenye ukurasa wa 16, Kenyatta, msichana anayeishi Marekani, anaeleza jinsi alivyojifunza kukabiliana na hisia zenye kuumiza kwa sababu ya kutowajua wazazi wake halisi.

Kukabiliana na kifo cha mzazi. Kufiwa na mama au baba kunaweza kuacha maumivu makali ya kihisia ambayo hayawezi kupona kwa urahisi. Biblia inaweza kusaidia. Mtungaji wake, Yehova, ni “Mungu wa faraja yote.”—2 Wakorintho 1:3.

Kwenye ukurasa wa 17, Angela, msichana anayeishi Australia, anaeleza jinsi uhusiano wake na Mungu unavyomsaidia kukabiliana na maumivu hayo makali.

Kila familia inakabili matatizo fulani. Kama utakavyoona katika maelezo yaliyo kwenye kurasa zinazofuata, wale wanaofuata kanuni za Biblia wamepata siri inayowasaidia kukabiliana na matatizo yao.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

Kumtunza Mtoto Mlemavu

Limesimuliwa na Victor Maynes, Afrika Kusini

“Tangu alipozaliwa, Andrew ametutegemea ili tumvishe, tumwogeshe, na nyakati nyingi hata tumlishe. Sasa ana umri wa miaka 44.”

TULISHUKU kwamba kuna kasoro fulani Andrew alipokosa kutembea alipokuwa na umri wa mwaka mmoja. Kisha, karibu na wakati huo, alizimia. Tulimkimbiza Andrew hospitalini na tukagundua kwamba alikuwa na kifafa. Lakini si hilo tu. Uchunguzi zaidi ulionyesha kwamba Andrew alikuwa na tatizo la akili.

Baada ya kujaribu matibabu mengi mbalimbali, tatizo lake la kuzimia lilipungua. Kwa muda, alihitaji kutumia dawa nne tofauti mara tatu kwa siku. Bila shaka, tatizo lake la akili haliwezi kutibiwa kwa dawa. Hata sasa, ingawa Andrew ana umri wa miaka 44, akili yake ni kama ya mtoto wa umri wa miaka mitano au sita hivi.

Madaktari walitushauri tumpeleke Andrew katika makao fulani ya kuwatunzia watu wenye mahitaji ya pekee, lakini tulikataa kufanya hivyo. Kwa kuwa tulikuwa na uwezo wa kumtunza Andrew, tuliamua kumtunzia nyumbani, licha ya hali ngumu ambayo tungekabili.

Kwa hiyo, sote katika familia yetu tunashirikiana kumtunza Andrew. Watoto wetu wengine, binti wawili na mvulana mmoja waliokuwa wakiishi nasi wakati huo, walisaidia sana kumtunza, na ninawashukuru sana. Pia, tukiwa Mashahidi wa Yehova, tumesaidiwa sana na washiriki wa kutaniko letu. Nyakati nyingine, wametuandalia chakula au wamemtunza Andrew tulipokuwa katika utumishi au tulipokuwa tukishughulikia mambo mengine.

Sikuzote tumekumbuka maneno ya Isaya 33:24 ambapo tunapata ahadi ya Mungu inayosema kwamba siku moja “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” Tunaamini kabisa kwamba Mungu atatimiza kusudi lake kwa ukamili la kuleta ulimwengu mpya na kuondoa kabisa magonjwa. (2 Petro 3:13) Tunatarajia wakati ambapo Andrew atakuwa na afya nzuri. Kwa sasa, tuna imani katika maneno ya Yesu kwamba ikiwa tutatanguliza mambo ya Ufalme wa Mungu katika maisha yetu, tutaandaliwa mahitaji yetu. (Mathayo 6:33) Sikuzote tumeona kwamba Mungu hutuandalia mahitaji yetu. Hatujakosa chochote kamwe.

Ni kweli kwamba si kila mtu anaweza kumtunzia nyumbani mtu wa familia aliye mgonjwa. Kwa wale wanaofanya hivyo, ningependekeza wasali kwa bidii na kwa ukawaida. (1 Petro 5:6, 7) Pili, mtunze mtoto wako kwa upendo mwingi, na usipuuze uwezo wake wa kujifunza kumpenda Yehova Mungu. (Waefeso 6:4) Tatu, wahusishe watu wote katika familia yako, na uwaruhusu wakusaidie. Nne, kumbuka kwamba mtoto wako atapata upendo mwingi nyumbani. Kwa kweli, hali hutofautiana. Sisi hatujuti kamwe kumtunza Andrew nyumbani. Kwa maoni yangu, yeye ndiye mtoto na ndiye mwanamume ninayempenda zaidi.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16]

Kulelewa na Wazazi Ambao Si Wako

Limesimuliwa na Kenyatta Young, Marekani

“Ikiwa wewe ni mtoto wa kambo basi una uhusiano wa damu na mzazi mmoja. Lakini mimi sina uhusiano wowote wa damu na wazazi walionilea. Hata sijui ninafanana na nani.”

SIJUI baba yangu ni nani, na sijawahi kumwona mama yangu mzazi. Alikuwa mraibu wa kileo na alitumia dawa za kulevya alipokuwa mjamzito. Nilichukuliwa na serikali nilipozaliwa na kupelekwa katika makao kadhaa ya kuwatunzia watoto kabla ya kuchukuliwa nikiwa na umri wa karibu miaka miwili na wazazi walionilea.

Baba yangu mlezi anasema kwamba alipoonyeshwa picha yangu, aliamua mara moja kunichukua. Mara moja nilimpenda mama yangu mpya. Nilimwambia kwamba yeye alikuwa mama yangu na kwamba nilitaka kwenda nyumbani pamoja naye.

Hata hivyo, ninakumbuka nikiwa mtoto niliogopa kwamba nitafanya jambo baya na kurudishwa kwenye makao ya kuwatunzia watoto. Nilihisi kwamba sipaswi kukasirika au hata kuwa mgonjwa kama watoto wengine. Hata nilijaribu kuepuka kupatwa na mafua! Wazazi wangu waliendelea kunihakikishia kwamba wananipenda na hawatawahi kuniacha.

Hata sasa nikiwa mtu mzima, nyakati nyingine mimi hujihisi kwamba sina thamani kama watu waliolelewa na wazazi wao halisi. Ninapoanza kuikubali hali yangu, mtu fulani huniambia, “Unapaswa kushukuru sana kwamba una wazazi wazuri ambao walikuwa tayari kukuchukua!” Ninashukuru, lakini maneno kama hayo hunifanya nihisi nina tatizo fulani na kwamba mtu alihitaji kujitahidi sana ili anipende.

Si rahisi kwangu kukubali ukweli wa kwamba huenda sitawahi kumjua baba yangu halisi. Nyakati nyingine mimi humkasirikia mama yangu kwamba hakuacha kutumia dawa za kulevya na kileo ili anilee. Mimi hujiuliza ikiwa aliona sifai hata kidogo kutunzwa. Lakini nyakati nyingine mimi humwonea huruma. Mara nyingi mimi hujiambia kwamba nikikutana naye, ningependa kumwambia kwamba nilifanikiwa maishani na hapaswi kujihisi vibaya kwa sababu ya kuniacha.

Wazazi wangu walionilea ni Mashahidi wa Yehova, na zawadi bora zaidi ambayo nimepata kutoka kwao ni ujuzi wa Biblia. Sikuzote maneno ya Zaburi 27:10 hunifariji sana: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” Hilo limethibitika kuwa kweli katika maisha yangu. Na nimepata matokeo mazuri kwa kulelewa na wazazi hao. Kwa mfano, ninapendezwa na watu, malezi yao na maisha yao, labda kwa sababu sijui wazazi wangu halisi. Ninawapenda watu, na hilo ni jambo muhimu katika utumishi wa Kikristo. Kuwa Shahidi wa Yehova na kuzungumza kuhusu Biblia hunisaidia nijiheshimu na kuwa na kusudi maishani. Ninaposhuka moyo, mimi huenda kuwasaidia wengine. Kwa kuwafundisha watu Biblia, ninaona kwamba ninakuwa na uhusiano mzuri pamoja nao. Kila mmoja wao ana mambo anayoweza kuzungumzia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 17]

Kukabiliana na Kifo cha Mzazi

Limesimuliwa na Angela Rutgers, Australia

“Baba yangu alipokufa, sikujihisi tena nikiwa salama. Yule mtu ambaye alijua kila kitu na ambaye angerekebisha kila kitu maishani mwangu hakuwapo tena.”

BABA yangu alikufa miaka kumi iliyopita nilipokuwa kijana. Miezi sita kabla ya hapo, alikuwa amefanyiwa upasuaji, na punde tu baada ya upasuaji, daktari alituambia kwamba hakuna matibabu zaidi wanayoweza kumpa. Mama yangu alitaka sana kupata habari zaidi, kaka yangu alizimia, nami nilisongwa na hisia nyingi. Miezi sita baadaye, baba yangu alikufa.

Nilipatwa na hisia mbalimbali. Nilitaka marafiki waelewe hali yangu, lakini sikutaka kuhurumiwa kupita kiasi. Hivyo, nilijitahidi kuficha hisia zangu. Kwa upande mwingine, nilihisi kwamba kama ningefurahia ushirika wao hilo lingeonyesha kwamba maisha yangu yamerudia hali ya kawaida na haikuwa hivyo. Mimi hufikiria jinsi ambavyo marafiki wangu walinivumilia!

Je, mimi hujihisi nikiwa na hatia kwa sababu ya kifo cha baba yangu? Ndiyo! Laiti ningemwambia “ninakupenda!” mara nyingi zaidi. Laiti ningemkumbatia mara nyingi zaidi au kutumia wakati mwingi zaidi naye. Hata nikijiambia mara nyingi kadiri gani kwamba baba hangependa nifikiri kwa njia hiyo, jambo hilo bado linanihangaisha.

Nikiwa Shahidi wa Yehova, ninafarijiwa sana na tumaini la Biblia kuhusu ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Ninajaribu kuwazia kwamba baba yangu amesafiri tu kwenda ng’ambo na siku moja atarudi nyumbani ingawa siku hususa haijulikani. Kwa kushangaza, mwanzoni sikufarijika watu waliponiambia, “Baba yako atafufuliwa.” Nilijiambia, ‘Namtaka baba yangu hapa sasa hivi!’ Lakini mfano wa kwamba amesafiri kwenda ng’ambo ulinisaidia. Mfano huo unaonyesha kwamba kutakuwa na ufufuo wakati ujao, nao hunifanya niweze kukabiliana na kifo cha baba.

Wakristo wenzangu wamenitegemeza sana. Ninakumbuka mmoja ambaye aliniambia kwamba hakujihisi huru kuzungumzia kifo cha baba yangu, lakini alikuwa akinifikiria sana na familia yetu. Niliendelea kufikiria maneno yake. Yalinisaidia wakati ambapo hakuna mtu aliyesema chochote kwa sababu nilitambua kwamba hata ingawa hawakusema chochote, walikuwa wakinifikiria na familia yetu. Hilo lilinifariji sana.

Miezi minne baada ya kifo cha Baba, Mama alianza kufanya mengi zaidi katika utumishi na niliona kwamba hilo lilimpa shangwe nyingi. Kwa hiyo nilijiunga naye. Inashangaza jinsi kuwasaidia wengine kunavyoweza kukusaidia kukabiliana na huzuni yako. Kufanya hivyo kumeimarisha imani yangu katika Biblia na ahadi za Yehova, na kumenisaidia kukazia uangalifu mambo mengine badala ya huzuni yangu.