Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Familia Zilizofanikiwa—Sehemu ya Pili

Familia Zilizofanikiwa—Sehemu ya Pili

Familia Zilizofanikiwa—Sehemu ya Pili

Kama ilivyoelezwa katika makala “Familia Zilizofanikiwa—Sehemu ya Kwanza,” Biblia ina kanuni zinazoweza kuimarisha familia wakati wa taabu. * Kwa wale wanaoishi kulingana na viwango vyake, Yehova Mungu anawaahidi hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”—Zaburi 32:8.

Kukabiliana na matatizo ya kiuchumi. Mara nyingi mambo yanayohusiana na pesa ndiyo chanzo cha mizozo mingi katika ndoa. Lakini kanuni za Biblia zinaweza kusaidia familia kushughulikia masuala ya pesa kwa njia inayofaa. Yesu alisema: “Acheni kuhangaika juu ya nafsi zenu kuhusu kile mtakachokula au kile mtakachokunywa, au juu ya miili yenu kuhusu kile mtakachovaa. . . . Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.”—Mathayo 6:25, 32.

Kwenye ukurasa wa 23, Issachar, anayeishi Marekani, anaeleza jinsi yeye na familia yake walivyokabiliana na hali ngumu ya kifedha baada ya nyumba yao kuharibiwa na Kimbunga Katrina.

Mtu katika familia anapokuwa mgonjwa. Karibu wanadamu wote huwa wagonjwa. Mara nyingi, ugonjwa huwa wa muda tu kisha mtu anapata nafuu. Lakini, namna gani ikiwa mtu katika familia anapata ugonjwa wa kudumu? Biblia inasema kwamba Yehova anaweza kumtegemeza mtu aliye katika kitanda cha ugonjwa. (Zaburi 41:1-3) Yehova anawezaje kutumia familia kumtegemeza mgonjwa?

Kwenye ukurasa wa 24, Hajime, ambaye ni mume anayeishi Japani, anaeleza jinsi ambavyo yeye na binti zake walishirikiana ili kumsaidia mke wake, Noriko, ambaye aligunduliwa ana ugonjwa mbaya.

Wakati mtoto anapokufa. Kifo cha mtoto ni moja kati ya misiba mibaya sana inayoweza kuikumba familia. Yehova anaahidi kufuta machozi ya huzuni ambayo husababishwa na msiba huo. (Ufunuo 21:1-4) Hata sasa, anatoa faraja kwa waliofiwa.—Zaburi 147:3.

Kwenye ukurasa wa 25, Fernando na Dilma, wanaoishi Marekani, wanasimulia jinsi Biblia ilivyowaimarisha kukabiliana na kifo cha binti yao mchanga.

Biblia inatoa mwongozo unaotegemeka kwa familia zilizokumbwa na misiba, kama masimulizi kwenye kurasa zinazofuata yanavyoonyesha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ona ukurasa wa 14-17 wa gazeti hili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

Kukabiliana na Matatizo ya Kiuchumi

Limesimuliwa na Issachar Nichols, Marekani

“Kimbunga Katrina kiliharibu nyumba yetu kabisa. Kwa mwezi mmoja na nusu maji yalijaa kwenye shule ambayo nilifanya kazi.”

WAKATI wa kiangazi cha 2005, mimi, mke wangu, Michelle, na Sydney, binti yetu mwenye umri wa miaka miwili, tuliishi huko Bay St. Louis, Mississippi, Marekani. Kwa kuwa mimi na Michelle ni Mashahidi wa Yehova, tulikuwa tumeweka mradi wa kushiriki kikamili katika huduma ya Kikristo. Nilikuwa mwalimu, na shule niliyofundisha ilikuwa huko New Orleans, Louisiana. Nilifanya kazi siku tatu kwa juma na nikatumia sehemu kubwa ya muda uliosalia kuwafundisha watu Biblia. Ratiba yetu ilitufaa sana. Kisha tukapata habari kwamba Kimbunga Katrina kilikuwa karibu kupiga eneo letu. Tulipanga kuondoka mara moja.

Dhoruba ilipokwisha, nyumba yetu huko Bay St. Louis na vilevile shule ambayo nilifundisha huko New Orleans, zilikuwa zimeharibiwa kabisa. Pesa za bima na msaada kutoka serikalini ulituwezesha kupata nyumba, lakini ilikuwa vigumu kwangu kupata kazi. Isitoshe, mke wangu alishikwa na ugonjwa kwa sababu ya kutumia maji machafu. Mfumo wake wa kinga ulidhoofika, na baadaye akaambukizwa virusi vya West Nile alipoumwa na mbu. Wakati huohuo, gharama za maisha na za bima ziliendelea kupanda.

Ili tuweze kubadilikana kulingana na hali zetu mpya, tulijifunza jinsi ya kutumia pesa zetu kwa uangalifu. Nilihitaji kukubali kazi yoyote ambayo ningepata.

Lazima nikubali kwamba tulisikitika sana kupoteza mali yetu. Lakini tulishukuru sana kuwa hai. Mambo yote yaliyotokea yalikazia uhakika wa kwamba vitu vya kimwili havina thamani sana. Kwa kweli, tulikumbushwa maneno haya ya Yesu: “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” —Luka 12:15.

Pia tulitambua kwamba hatupaswi kusikitika sana kwa sababu kulikuwa na watu wengi ambao walipoteza vitu vingi zaidi kuliko sisi. Wengine hata walipoteza maisha yao. Kwa sababu hiyo, mara tu baada ya msiba huo nilijiunga na kikundi cha kutoa msaada na kuwategemeza kihisia wengine ambao walikuwa wamepoteza mali zao.

Katika kipindi hicho cha msiba, andiko la Zaburi 102:17 lilitufariji sana. Linasema kwamba Yehova Mungu “hakika ataielekea sala ya wale waliovuliwa kila kitu, naye hataidharau sala yao.” Tumehisi utegemezo wake tukiwa familia!

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

Baada ya Vimbunga Katrina na Rita kukumba pwani ya Marekani inayopakana na Ghuba ya Mexico mnamo 2005, Mashahidi wa Yehova walianzisha vituo 13 vya kutoa msaada, mabohari tisa, na vituo vinne vya petroli. Karibu Mashahidi 17,000 walijitolea kutoka sehemu mbalimbali za Marekani na nchi nyingine 13 ili kutoa msaada. Wamekarabati maelfu ya nyumba.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

Mtu Katika Familia Anapokuwa Mgonjwa

Limesimuliwa na Hajime Ito, Japani

“Tulifurahia sana kupika pamoja kabla ya Noriko kuwa mgonjwa. Sasa hawezi kula, kunywa, au hata kuzungumza kwa kutumia mdomo wake. Lazima atumie kiti cha magurudumu na anapumua kwa kutumia mashine ya kumsaidia kupumua.”

MNAMO Mei (Mwezi wa 5) 2006, mke wangu, Noriko, alianza kuwa na matatizo ya kuzungumza. Kisha miezi michache baadaye akawa na matatizo ya kula na kunywa. Kufikia Septemba (Mwezi wa 9) iligunduliwa kwamba ana ugonjwa unaoitwa amyotrophic lateral sclerosis (ALS)—ugonjwa ambao polepole huathiri chembe za neva katika ubongo na uti wa mgongo. Katika muda wa miezi minne tu, maisha yetu yalibadilika kabisa. Na huo ulikuwa mwanzo tu wa matatizo yake.

Baada ya muda, ulimi wa Noriko ukapooza, na mkono wake vilevile. Alifanyiwa upasuaji ili kuingiza mrija tumboni ambao angeutumia kula, kisha akafanyiwa upasuaji mwingine shingoni ili aweze kupumua kwa hiyo hangeweza kuzungumza. Siwezi kuwazia kadiri ambavyo Noriko alijihisi kwani sikuzote amekuwa na bidii sana. Sisi ni Mashahidi wa Yehova, na Noriko pamoja na binti zangu wamekuwa wakitumia wakati wao wote katika utumishi wa Kikristo. Sasa Noriko anatumia mashine ya kumsaidia kupumua, na muda wote yuko kitandani.

Lakini tatizo hilo halijamfunga Noriko! Kwa mfano, yeye huenda kwenye mikutano akitumia kiti cha magurudumu akiwa na mashine yake ya kupumulia. Uwezo wake wa kusikia umedhoofika, kwa hiyo, binti yangu huandika maandishi makubwa wakati wa mikutano ili anufaike kutokana na programu. Na hata ingawa Noriko amelazimika kuacha utumishi wa wakati wote, bado anawaandikia watu barua, akiwafundisha kuhusu ujumbe wa tumaini unaopatikana katika Biblia kwa kutumia vifaa vya pekee ambavyo vimeunganishwa kwenye kompyuta yetu.—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-4.

Tumeshirikiana kama familia kumtunza Noriko. Binti zangu walitafuta kazi nyingine ili waweze kusaidia zaidi nyumbani. Sisi watatu hufanya kazi nyingi sana ambazo Noriko alikuwa akifanya.

Nyakati nyingine ninapomtazama Noriko asubuhi, yeye huonekana mchovu. Kisha mimi hujiambia, ‘Ningependa kumwambia apumzike leo.’ Lakini Noriko anataka kuwaeleza wengine ujumbe wa Biblia. Ninapoanza kumtayarishia kompyuta, macho yake hung’aa! Anapoandika, yeye hujihisi vizuri. Sasa nimeona umuhimu wa mtu ‘sikuzote kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’—1 Wakorintho 15:58.

Simulizi la Jason Stuart aliyeugua ugonjwa wa ALS, lililo kwenye gazeti la Januari (Mwezi wa 1) 2006 la Amkeni! limemsaidia sana Noriko asijihurumie kupita kiasi. Wafanyakazi wa hospitali walipouliza kwa nini Noriko alikuwa na mtazamo mzuri hivyo, Noriko aliwaambia kuhusu makala hiyo, na tuliwapa nakala nyingi. Kuwafundisha watu kuhusu imani yake kumemsaidia sana mke wangu.

Mimi na Noriko tumeoana kwa miaka 30, lakini katika miaka mitatu ambayo imepita, nimethamini sana mambo yake fulani ambayo hapo awali niliyapuuza. Ninafurahi sana kwamba nilimwoa!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

Wakati Mtoto Anapokufa

Limesimuliwa na Fernando na Dilma Freitas, Marekani

“Huzuni ya kumpoteza mtoto katika kifo ni jambo lisiloweza kuelezeka. Hakuna uchungu mkubwa kuliko huo.”

BINTI yetu tuliyemwita Precious, alikufa Aprili 16, 2006. Alikuwa ameishi kwa siku kumi tu. Mke wangu alipokuwa na mimba ya miezi mitatu hivi, ilisemekana kwamba mtoto aliyekuwa tumboni alikuwa na ugonjwa mbaya wa moyo. Kadiri siku ya kujifungua ilivyokaribia, iligunduliwa kwamba hata ikiwa angezaliwa akiwa hai, bado angekufa muda mfupi tu baada ya kuzaliwa. Lilikuwa jambo gumu sana kwetu kukubali. Tulikuwa na watoto watatu wenye afya. Hatukuamini kwamba mtoto wetu angekufa.

Baada ya Precious kuzaliwa, mtaalamu fulani wa matatizo ya kromosomu alisema kwamba binti yetu alikuwa na tatizo linaloitwa Trisomy 18, ambalo humpata mtoto 1 kati ya 5,000. Ilikuwa wazi kwamba Precious hataishi kwa muda mrefu. Tulijihisi tukiwa hoi kabisa kwa kuwa hatungeweza kumsaidia. Jambo pekee ambalo tungeweza kufanya lilikuwa kuwa pamoja naye kwa muda mfupi wa maisha yake. Na hivyo ndivyo tulivyofanya.

Tunashukuru sana kwamba tulifaulu kuwa na Precious kwa siku kumi. Wakati huo sisi na binti zetu watatu tulifanyiza uhusiano wa karibu sana naye. Tulimpakata, tukazungumza naye, tukamkumbatia, tukambusu, na tukampiga picha nyingi kadiri ambavyo tungeweza. Pia tulizungumza kuhusu ni nani katika familia ambaye alifanana zaidi naye. Yule mtaalamu aliyegundua tatizo la Precious alitutembelea kila siku hospitalini. Alilia pamoja nasi na akatuambia pole nyingi sana. Hata alipokuwa akizungumza nasi alichora picha ya Precious ili aweze kumkumbuka. Alitupatia nakala ya picha hiyo.

Kwa kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, tunaamini kabisa kwamba kama Biblia inavyofundisha, Mungu ataifanya tena dunia iwe paradiso na kwamba anatamani sana kuwafufua wale wote ambao wamekufa—kutia ndani, watoto wachanga, kama vile Precious. (Ayubu 14:14, 15; Yohana 5:28, 29) Tunatazamia siku ambayo tutampakata na kumkumbatia tena. Kila wakati tunaposikia neno “paradiso,” tumaini hilo huchangamsha mioyo yetu! Kwa wakati huu, tunafarijiwa na wazo la kwamba Precious yumo katika kumbukumbu la Mungu na hateseki tena.—Mhubiri 9:5, 10.