Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Ubaya Gani Kuishi Pamoja Kabla ya Kuoana?

Kuna Ubaya Gani Kuishi Pamoja Kabla ya Kuoana?

Maoni ya Biblia

Kuna Ubaya Gani Kuishi Pamoja Kabla ya Kuoana?

JE, UNAWEZA kununua suti au vazi bila kwanza kulijaribu? Watu wengi hawawezi. Ukifanya hivyo halafu baadaye ugundue kwamba halikutoshi, utakuwa umepoteza wakati na pesa zako.

Watu wengi hutumia mfano huo kuhusu ndoa. Wanahisi kwamba ni afadhali mwanamume na mwanamke kuishi pamoja kabla ya kuoana kisheria. Wao husema ‘mambo yakienda mrama, wanaweza kutengana bila kukabiliana na matatizo ya talaka yanayogharimu sana.’

Huenda baadhi ya wale walio na maoni hayo wamemwona rafiki yao aliyefunga ndoa akivumilia ndoa mbaya. Au huenda wengine wakawa wamejionea hali mbaya za ndoa ambayo mume na mke hawapendani tena. Kwa sababu hiyo, huenda wakaona kuishi pamoja bila kufunga ndoa kuwa jambo lenye hekima ili kuzuia matatizo ya baadaye.

Biblia ina maoni gani kuhusu jambo hilo? Ili kujibu, tunahitaji kuchunguza kile ambacho Neno la Mungu linasema kuhusu ndoa.

“Mwili Mmoja”

Biblia inaheshimu sana ndoa, na hilo halishangazi kwa kuwa mpango wa ndoa uliidhinishwa na kuanzishwa na Yehova Mungu mwenyewe. (Mwanzo 2:21-24) Tangu mwanzo, Yehova alikusudia kwamba ndoa iwaunganishe mwanamume na mwanamke kuwa “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Baada ya kunukuu simulizi la Biblia linalotaja kuhusu jambo hilo, Yesu aliongezea hivi: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:6.

Ni kweli kwamba wengine ambao hufunga ndoa baadaye hutalikiana. * Watu hawatalikiani kwa sababu kuna tatizo na mpango wenyewe wa ndoa; badala yake wanatalikiana kwa sababu mwenzi mmoja au wote wawili walishindwa kuheshimu kiapo walichotoa siku ya arusi yao.

Kwa mfano: Tuseme mwanamume na mwanamke wana gari, lakini hawalidumishi kulingana na maagizo yaliyotolewa na mtengenezaji wake. Nani atalaumiwa gari hilo linapoharibika? Je, ni mtengenezaji au ni wenye gari ambao walishindwa kulidumisha?

Kanuni hiyohiyo inahusu ndoa. Mume na mke wanapodumisha uhusiano wao na wanajitahidi kutatua matatizo yao kwa kutumia kanuni za Biblia, si rahisi watalikiane. Wanajihisi wakiwa salama katika ndoa ile kwa kuwa kila mmoja anawajibika kwa mwenzake. Kwa sababu hiyo ndoa inakuwa msingi wa uhusiano wenye upendo.

“Mjiepushe na Uasherati”

Lakini bado huenda wengine wakajiuliza: ‘Kwa nini basi tusiishi pamoja kwanza? Je, kujaribu uhusiano huo kabla ya kuanza kuwajibika si kunaonyesha kwamba tunaiona ndoa kuwa takatifu?’

Biblia inatoa jibu la wazi. Paulo aliandika: “Mjiepushe na uasherati.” (1 Wathesalonike 4:3) Neno “uasherati” linamaanisha mahusiano yote ya ngono nje ya ndoa. Hilo linahusisha ngono kati ya watu wawili wanaoishi pamoja, hata kama wanakusudia kuoana. Kulingana na Biblia, basi ni kosa kwa watu wawili kuishi pamoja—hata ikiwa nia yao ni kuoana baadaye.

Je, maoni hayo ya Biblia yamepitwa na wakati? Huenda wengine wakafikiria hivyo. Isitoshe, katika nchi nyingi, ni jambo la kawaida kwa watu kuishi pamoja—iwe wanakusudia kuoana au la. Lakini fikiria matokeo. Je, wale wanaoishi pamoja wamepata siri ya kufanikiwa kwa familia? Je, wana furaha kuliko wale waliofunga ndoa? Je, tarakimu zinaonyesha kwamba wenzi wa ndoa walioishi pamoja kabla ya kuoana ni waaminifu kuliko wale wengine? Uchunguzi unaonyesha jambo tofauti kabisa. Kwa kweli, imeonekana kwamba wenzi wa ndoa walioishi pamoja kabla ya kufunga ndoa wana matatizo mengi zaidi ya ndoa na mwishowe hutalikiana.

Wataalamu fulani wanasema kwamba uchunguzi kama huo una kasoro. “Watu wanaoamua kufunga ndoa bila [kuishi pamoja] kwanza wana mtazamo tofauti kabisa na watu wanaoamua [kuishi pamoja] kwanza,” anaandika mwanasaikolojia mmoja. Anasema kwamba jambo kuu si kuishi pamoja; badala yake jambo kuu ni “kuthamini ile hali ya kuoana.”

Hata ikiwa hilo ni kweli, linakazia tu umuhimu wa kusitawisha maoni ya Mungu kuhusu ndoa. Biblia inasema: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote.” (Waebrania 13:4) Mwanamume na mwanamke wanapoapa kuendelea kuwa mwili mmoja na kuheshimu mpango wa ndoa, wanakuwa na kifungo kisichoweza kukatwa kwa urahisi.—Mhubiri 4:12.

Kwa hiyo, tunaporudia mfano wa kwanza, ni jambo linalopatana na akili kujaribu suti au vazi kabla ya kulinunua. Hata hivyo, wazo hilo haliungi mkono kuishi pamoja kabla ya ndoa. Badala yake, mtu anapaswa kuchukua wakati kumfahamu yule anayekusudia kumwoa. Hiyo ni hatua muhimu ambayo mara nyingi hupuuzwa lakini ni moja kati ya siri za kufanikiwa kwa familia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Biblia inamruhusu mtu amtaliki mwenzi wake na kuoa mwingine ikiwa mwenzi wake amefanya ngono nje ya ndoa.—Mathayo 19:9.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Kwa nini Biblia inaruhusu ngono kati ya watu waliooana tu?—Zaburi 84:11; 1 Wakorintho 6:18.

▪ Unapaswa kutafuta sifa gani katika mwenzi wa ndoa?—Ruthu 1:16, 17; Methali 31:10-31.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

“ANAUTENDEA DHAMBI MWILI WAKE MWENYEWE”

Biblia inasema: “Yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 6:18) Katika miaka ya karibuni, ukweli wa maneno hayo umeonekana kwa sababu ya mamilioni ya watu ambao wamekufa kutokana na UKIMWI na magonjwa mengine ya zinaa. Lakini si hilo tu. Uchunguzi umeonyesha kwamba ni jambo la kawaida kwa vijana wanaofanya ngono kushuka moyo sana na hata kujaribu kujiua. Pia, ukosefu wa maadili husababisha mimba zisizotakiwa, na hilo hutokeza katika visa fulani kishawishi cha kutoa mimba. Kwa kufikiria mambo hakika, tunaweza kukata kauli kwamba sheria ya maadili iliyo katika Biblia haijapitwa na wakati.