Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya 4: Kuheshimiana

Siri ya 4: Kuheshimiana

Siri ya 4: Kuheshimiana

“Kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.”—Waefeso 4:31.

Hilo linahusisha nini? Familia zenye matatizo na hata zile zilizofanikiwa huwa na hali ya kutoelewana. Lakini familia zenye mafanikio huzungumzia mambo bila kutumia kejeli, matusi, na maneno mengine yenye kuudhi. Watu katika familia hizo hutendeana kama wanavyotaka watendewe.—Mathayo 7:12.

Kwa nini ni muhimu? Maneno yanaweza kuwa silaha na kuwaumiza sana wengine. Methali moja ya Biblia inasema: “Afadhali kuishi jangwani, kuliko kukaa na mwanamke mgomvi na msumbufu.” (Methali 21:19, Biblia Habari Njema) Bila shaka, inaweza kusemwa hivyo kumhusu mwanamume mgomvi. Na Biblia inasema hivi kuwahusu wazazi: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.” (Wakolosai 3:21) Watoto wanaochambuliwa kila wakati wanaweza kuhisi kwamba haiwezekani kuwafurahisha wazazi wao. Wanaweza kukata tamaa kabisa.

Jaribu kufanya hivi. Jaribu kupima kiwango cha heshima katika familia yako kwa kutumia maswali yafuatayo.

Katika familia yangu, je, ni kawaida kwa mtu mmoja kuondoka chumbani kwa hasira kunapokuwa na hali ya kutoelewana?

Ninapozungumza na mwenzi wangu au mtoto wangu, je, mimi hutumia yenye matusi, kama vile “mjinga,” “mpumbavu,” au maneno kama hayo?

Je, nililelewa katika mazingira ambayo watu walizoea kutumia matusi?

Azimia. Fikiria jambo mmoja au mawili unayoweza kufanya ili kuonyesha heshima unapozungumza. (Dokezo: Azimia kusema “mimi” badala ya “wewe.” Kwa mfano, “Mimi hujihisi nimeumia unapo . . . ,” badala ya “Kila wakati wewe . . . ”)

Mbona usimwambie mwenzi wako mambo unayopanga kufanya ili kuonyesha heshima zaidi? Baada ya miezi mitatu, mwulize mwenzi wako ikiwa anaona mabadiliko yoyote.

Fikiria mipaka ambayo unaweza kujiwekea ili usitumie matusi unapozungumza na watoto wako.

Mbona usiwaombe watoto wako msamaha kwa pindi ambazo huenda ulizungumza nao kwa hasira au kwa kejeli?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kama tu mawimbi ya bahari yanavyoweza kumomonyoa miamba migumu, ndivyo mazoea ya kutumia maneno yenye kuumiza yanavyoweza kudhoofisha familia