Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya 6: Kusameheana

Siri ya 6: Kusameheana

Siri ya 6: Kusameheana

“Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.”—Wakolosai 3:13.

Hilo linahusisha nini? Wenzi wenye mafanikio hujifunza kutokana na mambo ambayo walifanya zamani; lakini hawaweki hesabu ya mambo mabaya waliyofanyiwa na kuyatumia kutilia chumvi kasoro za wenzi wao kwa kusema, “Wewe huchelewa kila wakati” au “Wewe siku zote hunisikilizi.” Wenzi wote wawili huona kwamba “ni jambo lenye kupendeza [mtu] anapopita kosa.”—Methali 19:11.

Kwa nini ni muhimu? Mungu ‘yuko tayari kusamehe,’ lakini nyakati nyingine wanadamu hawafanyi hivyo. (Zaburi 86:5) Ikiwa mizozano ya zamani haitasuluhishwa, inaweza kutokeza chuki ambayo mwishowe itafanya iwe vigumu sana kusamehe. Huenda kila mwenzi akakataa kuzungumza kuhusu hisia zake na wakati uleule hajali hisia za mwenzake. Wote wanahisi wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo.

Jaribu kufanya hivi. Tazama picha zako na za mwenzi wako mlizopigwa mwanzoni mwa ndoa yenu au wakati wa uchumba. Jaribu kuamsha tena upendo mliokuwa nao kabla ya matatizo kuanza na kuwapofusha. Kisha fikiria kuhusu sifa ambazo zilikuvutia kwa mwenzi wako.

Ni sifa zipi za mwenzi wako ambazo sasa zinakuvutia sana?

Fikiria jinsi unavyoweza kuwaathiri watoto wako kwa njia nzuri kwa sababu ya kuwa mtu mwenye kusamehe.

Azimia. Fikiria njia moja au mbili ambazo unaweza kutumia ili usihusishe mizozo ya wakati uliopita mnapozozana tena.

Mbona usimwambie mwenzi wako ni sifa gani alizo nazo zinazokuvutia?—Methali 31:28, 29.

Fikiria jinsi unavyoweza kuwafundisha watoto kusamehe.

Mbona usizungumze na watoto wako kuhusu kusamehe na jinsi sifa hiyo inavyomnufaisha kila mtu katika familia?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Unaposamehe, deni linafutwa. Usidai tena ulipwe