Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya 7: Kuweka Msingi Imara

Siri ya 7: Kuweka Msingi Imara

Siri ya 7: Kuweka Msingi Imara

Hilo linahusisha nini? Jengo lolote imara linahitaji kuwa na msingi imara, na ndivyo ilivyo na familia zenye nguvu. Familia zenye nguvu hazivumilii matatizo bila jitihada zozote, kama tu vile nyumba haiendelei kusimama kwa miaka mingi bila kuwa na msingi imara. Familia zenye mafanikio zimejengwa juu ya mwongozo unaofaa.

Kwa nini ni muhimu? Vitabu vingi, magazeti, na programu za televisheni hutoa mashauri mengi kuhusu maisha ya familia. Washauri fulani wa ndoa wanaweza kuwahimiza wenzi wa ndoa wenye matatizo waendelee kuishi pamoja, huku wengine wakiwashauri watengane. Hata wataalamu hubadili maoni yao kuhusu mambo ya familia. Kwa mfano, mnamo 1994 mshauri mmoja maarufu ambaye hushughulika na matatizo ya vijana wanaobalehe aliandika kwamba alipoanza kufanya kazi hiyo, alihisi kwamba “ni afadhali watoto waishi pamoja na mzazi mmoja mwenye furaha badala ya kuishi na wazazi waliooana wasio na furaha. Nilidhani kwamba talaka ndilo suluhisho linalofaa badala ya kuwa katika ndoa yenye matatizo.” Hata hivyo, baada ya kufanya kazi hiyo kwa miaka 20, alibadili maoni yake. Alisema hivi: “Talaka huwaumiza watoto wengi.”

Maoni hubadilika, lakini ushauri bora zaidi unaoweza kupatikana lazima uwe unapatana kwa njia fulani na kanuni za Neno la Mungu, Biblia. Ulipokuwa ukisoma makala hizi, huenda umeona kwamba kuna kanuni fulani ya Biblia iliyoandikwa juu kwenye ukurasa wa 3-8. Kanuni hizo zimesaidia familia nyingi kufanikiwa. Kama tu familia nyingine zote, familia zilizofanikiwa pia huwa na matatizo. Tofauti ni kwamba Biblia imewasaidia wawe na msingi imara kwa ajili ya ndoa na familia. Tungetazamia Biblia iandae msingi huo kwa sababu Mtungaji wake, Yehova Mungu, ndiye Mwanzilishi wa familia.—2 Timotheo 3:16, 17.

Jaribu kufanya hivi. Andika orodha ya maandiko yaliyonukuliwa juu kwenye ukurasa wa 3 hadi wa 8. Andika maandiko mengine ambayo yamekusaidia. Weka orodha hiyo mahali inapoweza kupatikana kwa urahisi na usome maandiko hayo mara kwa mara.

Azimia. Azimia kutumia Biblia katika maisha ya familia yako.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Familia yako ikiwa na msingi imara wa Kimaandiko, inaweza kushinda dhoruba zinazoihatarisha