Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kufanikiwa Ukiwa Mzazi Mmoja

Unaweza Kufanikiwa Ukiwa Mzazi Mmoja

Unaweza Kufanikiwa Ukiwa Mzazi Mmoja

IMESEMEKANA kwamba ikiwa familia yenye wazazi wote wawili ingelinganishwa na mnyama, basi huenda mnyama huyo angekuwa katika orodha ya wanyama wanaokaribia kutoweka. Fikiria: Kuna zaidi ya familia milioni 13 za mzazi mmoja nchini Marekani peke yake, na wengi wao ni akina mama. Uchunguzi unaonyesha kwamba karibu nusu ya watoto wote nchini humo watakapofikia maisha ya ujana wataishi katika familia ya mzazi mmoja.

Ikiwa wewe ni mzazi asiye na mwenzi, uwe na hakika kwamba familia yako inaweza kufanikiwa. Jaribu kutumia mapendekezo yanayofuata.

Epuka kutumia maneno yenye kuvunja moyo. Biblia inasema hivi: “Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.” (Methali 15:15) Ni kweli, huenda maisha yako yasionekane kama karamu. Lakini mstari huo unaonyesha kwamba uchangamfu unatokana na hali ya mtu ya moyoni na si hali zinazomkabili. (Methali 17:22) Hakuna faida unayopata unapowafikiria watoto wako kuwa wamelaaniwa au nyumba yako kuwa isiyoweza kurekebika. Maneno kama hayo yatakuvunja moyo tu na kufanya iwe vigumu zaidi kwako kutimiza majukumu yako ukiwa mzazi.—Methali 24:10.

Pendekezo: Andika orodha ya maneno yenye kuvunja moyo ambayo wewe hutumia kueleza hali yako, kisha kando ya kila neno uandike maneno badala yenye kutia moyo. Kwa mfano, badili “Jambo hili limenishinda” na kando yake andika “Ninaweza kutimiza jukumu langu nikiwa mzazi mmoja, na ninaweza kupata msaada ninaohitaji.”—Wafilipi 4:13.

Panga bajeti. Wazazi wengi wasio na mwenzi, hasa akina mama, huwa na matatizo ya pesa. Hata hivyo, katika visa fulani matatizo ya kiuchumi yanaweza kupunguzwa ikiwa mtu anapangia matumizi yake vizuri. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Ili uepuke “msiba” wa kiuchumi, unahitaji kupanga mambo na kufikiria mbele.

Pendekezo: Andika bajeti yako. Weka rekodi ya matumizi yako ya mwezi na uone jinsi unavyotumia pesa zako. Changanua sana jinsi unavyotumia pesa. Je, unakopa sana? Je, wewe huwanunulia watoto wako vitu ili tu wasione wanakosa mzazi mwingine? Ikiwa watoto wako wana umri wa kutosha, keti chini nao mfikirie njia za kuweka pesa fulani akiba. Hayo yatakuwa mazoezi mazuri kwao. Na hata huenda wakawa na madokezo kadhaa yanayofaa!

Shughulika kwa amani na mwenzi wako wa zamani. Ikiwa nyote wawili mmepewa kibali cha kuwatunza watoto wenu, haifai kumwambia mtoto wako mambo mabaya kumhusu mzazi yule mwingine—au kumtumia mtoto wako kuwa mpelelezi katika maisha yake. * Ni afadhali zaidi kutafuta njia za kushirikiana na mzazi huyo mwingine kuhusu mambo kama kutia nidhamu au jambo lingine lolote linalomhusu mtoto wenu. Biblia inasema: “Kadiri inavyowezekana kwa upande wenu, mwe na amani na watu wote”—na hilo linatia ndani mwenzi wako wa zamani.—Waroma 12:18, Biblia Habari Njema.

Pendekezo: Wakati mwingine hali ya kutoelewana ikitokea tena, mtendee mwenzi wako wa zamani kama mfanyakazi mwenzako. Ukiwa kazini, wewe hujaribu kushirikiana na kila mtu—hata wale ambao huenda huwapendi. Fanya hivyo pia unaposhughulika na mwenzi wako wa zamani. Huenda ninyi wawili msikubaliane nyakati zote, lakini si lazima jambo lolote dogo lianzishe ugomvi.—Luka 12:58.

Uwe mfano mzuri. Jiulize: ‘Ninataka watoto wangu wafuate kanuni na wasitawishe mitazamo gani? Je, mimi hufuata kanuni na mitazamo hiyo?’ Kwa mfano, je, wewe una furaha, licha ya kwamba wewe ni mzazi asiye na mwenzi? Au je, wewe huruhusu hali zako zikufanye uwe na mtazamo usiofaa kuhusu maisha yako? Je, bado unaendeleza chuki kwa sababu ya jinsi mwenzi wako wa zamani alivyokutendea? Au je, umefaulu kukabiliana na hali ambazo huwezi kuzidhibiti? (Methali 15:18) Kwa kweli, huenda hali hizo si rahisi kushughulika nazo, na huenda usizishughulikie kwa njia inayofaa kabisa. Hata hivyo, watoto wako wataiga mitazamo yako.

Pendekezo: Andika sifa tatu ambazo ungependa kila mmoja wa watoto wako awe nazo atakapokuwa mtu mzima. * Kisha kando ya kila sifa, andika ni mambo gani unayoweza kufanya sasa ili kuwawekea mfano utakaowasaidia kukuza sifa hiyo.

Jitunze. Kwa kuwa kuna mambo mengi sana ya kufanya maishani, ni rahisi sana kupuuza afya yako ya kimwili na kihisia. Usiruhusu jambo hilo likupate! Lazima utosheleze ‘uhitaji wako wa kiroho!’ (Mathayo 5:3) Kumbuka—gari lisilo na mafuta haliwezi kwenda mbali. Hali itakuwa hivyo kwako iwapo huchukui wakati wa “kujijaza.”

Pia kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kurukaruka.” (Mhubiri 3:4) Si kupoteza wakati kuwa na tafrija. Inakuburudisha na kukutia nguvu tena ili uweze kuvumilia hali ukiwa mzazi mmoja.

Pendekezo: Zungumza na wazazi wengi wasio na wenzi uwaulize jinsi wanavyojitunza. Bila kupuuza “mambo yaliyo ya maana zaidi,” je, unaweza pia kutumia muda fulani kila juma ukifanya jambo ambalo linakufurahisha? (Wafilipi 1:10) Andika ni mambo gani ambayo ungependa kufanya na ni wakati gani unaweza kuyafanya.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kwa habari zaidi, ona makala “Nyumba Iliyogawanyika—Jinsi Talaka Inavyowaathiri Vijana,” kwenye ukurasa wa 18-21 wa gazeti hili.

^ fu. 11 Huenda ukachagua sifa kama “heshima,” “usawaziko,” na “kusamehe,” zinazozungumziwa kwenye ukurasa wa 6-8 katika gazeti hili.