Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Nilivyoacha Kupenda Vita

Jinsi Nilivyoacha Kupenda Vita

Jinsi Nilivyoacha Kupenda Vita

Limesimuliwa na Thomas Stubenvoll

NILIZALIWA New York City Novemba 8, 1944 (8/11/1944). Nililelewa eneo la South Bronx, eneo ambalo wakati huo lilikuwa limegawanyika kulingana na rangi ya mtu. Nikiwa kijana mdogo nilishinda mitaani, na muda si muda nikajifunza mahali mipaka ya magenge ya watu wa jamii mbalimbali ilikuwa na nikaepuka kuivuka. Magenge hayo yaliogopwa kwa sababu ya vitendo vyao vya kihalifu na tabia nyingine za kijeuri.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilijiunga na genge fulani. Jina la genge letu lilikuwa Mafuvu. Mimi na rafiki zangu tulikuwa tukiingia kwenye treni za mizigo na kuiba makatoni yaliyokuwa na siagi ya karanga na vyakula vingine. Magenge yaliyokuwa na vijana wanaokaribia umri wa miaka 20 yalikuwa ndiyo hatari zaidi. Mara nyingi kulikuwa na mapigano makali ya kumwaga damu kati ya magenge ya aina hiyo. Pindi moja, rafiki yangu wa karibu alichomwa kisu hadi akafa mbele ya macho yangu.

Vita Vilinisisimua

Kushirikiana na genge hakukunifanya niwe na furaha. Baada ya muda fulani, nilitaka tu kuhama eneo hilo. Mjomba wangu anayeitwa Eddie, alikuwa ametoka kupigana Vita vya Korea, ambako alitumikia akiwa askari-jeshi wa kitengo cha Marine cha Jeshi la Majini la Marekani. Masimulizi ya mjomba Eddie kuhusu askari-jeshi wa kitengo hicho yalinisisimua sana. Niliambiwa kwamba kila askari-jeshi wa kitengo hicho hupewa mazoezi ya pekee kupigana kwenye nchi kavu, majini, na angani, naye ni kiongozi mwenye nidhamu na ni shujaa aliyefundishwa kutimiza wajibu wake vizuri. Maneno yanayowaongoza askari-jeshi hao ni, Semper fidelis, maneno ya Kilatini yanayomaanisha “uaminifu nyakati zote,” kuonyesha kuwa wanapaswa kuwa na ushikamanifu na ujitoaji wa hali ya juu. Kuanzia wakati huo, nilitamani sana kuwa askari-jeshi stadi wa kitengo hicho.

Novemba 8, 1961, siku ambayo nilifikia umri wa miaka 17, nilijiandikisha jeshini. Miezi minne baadaye, nilihitimu mafunzo ya msingi ya jeshi. Huo ulikuwa mwanzo wa miaka 11 ya kutumikia jeshini.

Nilijiunga na jeshi wakati ambapo hakukuwa na vita. Hata hivyo, mwanajeshi haachi kufanya mazoezi. Kwanza, nilitumwa Oahu, huko Hawaii, ambako kwa miaka miwili nilipata mafunzo makali ya askari-jeshi wa miguu na vita vya msituni. Nikawa mlenga-shabaha hodari, nikiwa na uwezo wa kulenga shabaha umbali wa mita 457. Nilifunzwa judo, kareti, kushughulikia mabomu, kusoma ramani, kubomoa vitu, na mawasiliano. Nilifurahia kila jambo.

Baada ya kutoka Hawaii, nilienda Japani kwa miezi sita kulinda silaha za chini ya maji kwenye Kituo cha Jeshi la Majini, huko Atsugi. Kisha, vita kati ya Marekani na Vietnam Kaskazini vikazidi, na nikatumwa nikiwa mmoja wa askari-jeshi kwenye meli inayobeba ndege za kivita ya USS Ranger. Ndege kutoka kwenye meli yetu iliyokuwa kwenye Ghuba ya Tonkin, ziliangusha mabomu huko Vietnam Kaskazini. Hatimaye nilikuwa katika vita halisi. Hata hivyo, niliona kwamba ninakosa ule msisimko wa kupigana vita ardhini kwa sababu nilikuwa ndani ya meli.

Uhalisi wa Vita

Mwaka wa 1966, nikiwa bado kwenye meli ya Ranger, niliruhusiwa kuondoka kwa heshima baada ya kutumikia jeshini kwa miaka minne. Askari-jeshi wengi wangefurahia kurudi nyumbani na hivyo kuepuka mapigano makali ambayo yalikuwa karibu kuanza. Hata hivyo, mimi nilikuwa nimejitoa kabisa kuwa askari-jeshi, shujaa kamili, na sikuwa na nia ya kuondoka. Nikaamua kujiandikisha tena.

Nilitaka kupigana. Hayo ndiyo mafunzo niliyokuwa nimepewa. Kwa hiyo, nikajitolea katika kikosi cha askari-jeshi wa miguu. Mradi tu nilikuwa katika kikosi cha Marine cha askari-jeshi wa miguu, sikujali nitatumwa wapi. Lengo langu lilikuwa kuwa askari-jeshi bora kabisa, na vita vikawa mungu wangu.

Mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1967, nilitumwa Vietnam. Nikiwa na msisimko na pia wasiwasi, nilipelekwa kwenye jimbo la Quang Tri ambako vita vilikuwa vimechacha kabisa. Kabla ya siku moja kwisha, nilijikuta katikati ya mapigano makubwa ya umwagaji damu. Watu walikuwa wakiuawa na kujeruhiwa kila mahali. Niliona vumbi likiruka kutokana na risasi za adui zilizokuwa zikipiga ardhini. Hakukuwa na mahali pa kujificha isipokuwa vichaka vichache tu. Nilianza tu kufyatua risasi. Halikuwa jambo lenye kupendeza. Nilifikiri kwamba nitakufa. Hatimaye vita vilikwisha. Nilipona lakini askari-jeshi wenzangu wengi waliuawa.

Kwa miezi 20 iliyofuata, nilishiriki kwenye mapigano makali zaidi ya Vita vya Vietnam. Kila siku kwa karibu saa 24, nilikuwa ama ninafyatua risasi ama ninajaribu kujikinga ili nisifyatuliwe, nilikuwa nikiweka mitego au nikiwekewa. Kwa karibu kipindi hicho chote, nilikuwa nikifyatuliana risasi na adui nikiwa kwenye mahandaki ambayo yaligeuka kuwa madimbwi yenye matope mvua iliponyesha. Nyakati nyingine kulikuwa na baridi na hali isiyovumilika. Nilikula na kulala ndani ya mahandaki hayohayo.

Mara kwa mara tulitumwa kwenye misitu yenye unyevunyevu kwa ajili ya kampeni ya kusaka na kuwaua maadui kukiwa na hatari ya kushambuliwa kutoka vichakani. Nyakati fulani mizinga ilikuwa ikianguka kando yangu kwa saa nyingi. Kwenye pigano fulani karibu na mji wa Khe Sanh, asilimia 75 hivi ya askari-jeshi kwenye kikosi changu walijeruhiwa au kuuawa—ni askari-jeshi 13 tu tuliosalimika.

Januari 30, 1968, nilikuwa kwenye kambi yetu, ambapo nililala kwenye hema kwa mara ya kwanza baada ya mwaka mmoja hivi. Utulivu huo ulivurugwa mapema asubuhi nilipoamshwa kwa kishindo cha mlipuko wa kombora. Nilijeruhiwa. Vipande kadhaa vya vyuma vilikwama kwenye bega na mgongoni mwangu. Asubuhi hiyo maadui walikuwa wameanza kampeni kubwa ya mashambulizi.

Majeraha hayo yalifanya nitunukiwe nishani ya jeshi la Marekani wanayopewa wanajeshi kwa kujeruhiwa vitani, lakini hayakunizuia kupigana. Madaktari waliondoa vyuma hivyo, na upesi nikaelekea kwenye mji wa Hue, ambako mapigano makali yalikuwa yakiendelea. Huko niliua watu kinyama. Halikuwa jambo kubwa kwangu kumpiga adui risasi. Kwa siku 32, nilitembea nyumba kwa nyumba nikiwasaka na kuwaua maadui.

Wakati huo niliona kwamba nina haki ya kufanya hivyo. Nilijiambia hivi, ‘Si maadui wanaua maelfu ya wanawake, wanaume, na watoto kwenye mji huo. Maiti za watu zimetapakaa mitaani. Mabomu yametegwa kila mahali, hata chini ya maiti. Mara nyingi maadui wanatushambulia kwa kuvizia.’ Yote hayo hayakunitisha. Akilini mwangu nilijiambia kwamba kumwua adui ni sawa kabisa.

Tamaa Isiyofaa ya Vita

Muda fulani baada ya pigano la Hue, nilikamilisha miezi 13 ya kuwa katika mgawo hususa jeshini. Hata hivyo, bado vita vilikuwa vikiendelea nami nilitaka kuendelea kushiriki. Kwa hiyo niliamua kujitolea kubaki tena Vietnam kwa kipindi kingine. Nilikuwa na cheo cha sajini mwandamizi wa jeshi na nilikuwa nimekabidhiwa mgawo fulani wa pekee. Mgawo huo ulitia ndani kuongoza askari-jeshi kwenye maeneo ya vijijini. Huko tulichangamana na wanavijiji, tukiwafundisha jinsi ya kulinda vijiji vyao. Kila mara tulikuwa chonjo kwa sababu mara nyingi maadui walijificha katikati ya raia. Tulitembea kimyakimya usiku tukisaka, kuwakamata, na kuwaua maadui. Licha ya hali hiyo yenye wasiwasi mwingi, hamu yangu ya kupigana vita ilizidi kuongezeka.

Muda wangu wa kuwa Vietnam ulimalizika haraka. Kwa mara nyingine tena nikaomba niongezewe muda wa kuwa kwenye uwanja wa vita. Pindi hii wakubwa wangu walikataa, labda kwa kuwa walitambua nilikuwa na tamaa isiyofaa ya vita. Hata hivyo, kazi yangu nikiwa askari-jeshi haikuishia hapo. Nilirudishwa nyumbani Marekani ili nikawafundishe askari-jeshi wapya. Kwa kipindi cha miaka mitatu na nusu, nilikazia uangalifu kazi yangu nikiwa mkufunzi. Niliwafundisha wanafunzi wangu mambo mengi, na nilijitahidi sana kuwafanya wafikie kiwango changu.

Nilipata Kusudi Bora Zaidi Maishani

Nilianzisha urafiki na mkufunzi mwenzangu. Mke wake alikuwa ametoka tu kumwacha. Dada yake, anayeitwa Christine Antisdel, alikuwa amebatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova muda mfupi kabla ya hapo, na alikuwa amekuja kumsaidia kuwalea watoto wake wawili wachanga. Hiyo ndiyo iliyokuwa mara yangu ya kwanza kusikia kuhusu Mashahidi wa Yehova.

Nililelewa nikiwa Mkatoliki na nilisoma katika shule ya Wakatoliki kwa miaka minane. Hata niliwahi kutumikia nikiwa mhudumu kanisani. Hata hivyo, kwa kweli sikujua chochote kuhusu Biblia. Christine alinisaidia kuelewa kweli za Biblia ambazo sikuwa nimewahi kusikia kabla ya hapo. Nilijifunza Biblia inafundisha nini hasa na kile ambacho haifundishi.

Kwa mfano, nilijifunza kwamba Biblia haifundishi kwamba baada ya watu kufa, Mungu anawaadhibu watu katika moto wa mateso. (Mhubiri 9:5, 10) Haifundishi kwamba Mungu ni sehemu ya Utatu. (Yohana 14:28) Hata hivyo, Biblia inafundisha kwamba Mungu ataondoa uovu, maumivu, na kifo na kwamba watu waadilifu wataishi milele katika paradiso duniani. (Zaburi 37:9-11; Ufunuo 21:3, 4) Pia, nilijifunza kweli kuhusu viwango vya maadili vya Mungu. (1 Wakorintho 6:9, 10) Nilijifunza kwamba Mungu ana jina, Yehova. (Zaburi 83:18) Mambo haya yote yalikuwa yenye kuvutia kama nini!

Mnamo Novemba 1972, nilipelekwa kwenye kambi nyingine, ili niwafundishe maofisa wa jeshi mbinu mbalimbali za kijeshi. Nikiwa huko nilianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Nilianza kuhudhuria mikutano yao na nilivutiwa sana na hali ya urafiki na undugu wa Mashahidi.

Lakini, kadiri nilivyojifunza Biblia, ndivyo dhamiri yangu ilivyonisumbua zaidi. Kweli ya Biblia ilipingana kabisa na jinsi nilivyokuwa nikiishi. Nilitoa maisha yangu nipigane kwa ajili ya taifa langu na kujihusisha katika jeuri, mambo ambayo Mungu anachukia.

Nilifikia mkataa kwamba siwezi kuwa askari-jeshi na wakati uleule nimwabudu Yehova Mungu. Hapo ndipo tamaa yangu kuelekea vita iliisha. Niliamua kuacha kazi hiyo. Miezi kadhaa ilipita nikishughulikia fomu za kuacha kazi, nikihojiwa, na kuchunguzwa akili yangu, na mwishowe niliruhusiwa kuondoka kwa heshima, kwa sababu ya dhamiri yangu. Hivyo ndivyo nilivyomaliza miaka 11 ya utumishi wangu wa kijeshi.

Sasa ningeweza kumwambia Yehova maneno ya Isaya 6:8: “Mimi hapa! Nitume mimi.” Ndiyo, nilikuwa tayari kwa shangwe kumtumikia Mungu wa kweli kwa nguvu zangu badala ya kutumikia nikiwa askari-jeshi wa Jeshi la Majini. Julai 27, 1973 (27/7/1973), nilibatizwa ili niwe Shahidi wa Yehova. Miezi mitano baadaye nilimwoa Christine Antisdel, Shahidi wa kwanza mimi kukutana naye.

Mimi na Christine tumetumia miaka 36 ya maisha yetu pamoja tukiwasaidia wengine kupata ujuzi wa Biblia ili waweze kumkaribia Mungu. Kwa miaka minane tulitumikia tukiwa wamishonari katika nchi ya Jamhuri ya Dominika. Kwa miaka 18 iliyopita, nimetumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri. Mimi na mke wangu tumetembelea mamia ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ya Kihispania kotekote nchini Marekani.

Hakuna maumivu yoyote ya kihisia au ya kiakili ninayopata kutokana na kupigana vita wakati uliopita. Sina mfadhaiko wa akili na pia sina tatizo la kuota ndoto zenye kushtua. Hata hivyo, baada ya kumkaribia Yehova Mungu, ninasikitika sana kwamba niliwaua wanadamu wenzangu wakati wa vita.

Nimefanya mabadiliko makubwa, lakini ninafurahi sana kwamba niliyafanya. Sasa ninahisi kwamba Mungu amenisamehe mambo yote niliyofanya zamani. Badala ya kuua watu, sasa kusudi langu ni kuwapa watu tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. Nilipokuwa askari-jeshi, nilifanya mambo kwa sababu ya kutojua nikichochewa na bidii ambayo haikuwa imeelekezwa vizuri. Kwa kuwa mimi ni Shahidi wa Yehova, na nimejifunza kile ambacho Biblia inafundisha, ninafanya mambo nikiwa na usadikisho imara kwamba kuna Mungu wa kweli na aliye hai, kwamba yeye ni Mungu mwenye upendo, na kwamba mwishowe, wale wanaompenda na kumtii watapata mambo mema.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kila siku kwa karibu saa 24, nilikuwa ama ninafyatua risasi ama ninajaribu kujikinga ili nisifyatuliwe

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Baada ya kumkaribia Yehova Mungu, ninasikitika sana kwamba niliwaua wanadamu wenzangu wakati wa vita

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa mkufunzi wa kijeshi (juu) na nikiwa askari-jeshi wa miguu huko Vietnam (kushoto)

[Picha katika ukurasa wa 25]

Majeraha yangu yalifanya nitunukiwe nishani hii ya jeshi la Marekani, lakini hayakunizuia kupigana

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mimi na Christine tumetumia miaka 36 ya maisha yetu pamoja tukiwasaidia wengine kupata ujuzi wa Biblia