Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nyota ya Aina Gani Iliyowaongoza Wale “Mamajusi” kwa Yesu?

Ni Nyota ya Aina Gani Iliyowaongoza Wale “Mamajusi” kwa Yesu?

Ni Nyota ya Aina Gani Iliyowaongoza Wale “Mamajusi” kwa Yesu?

Hadithi za Krismasi zinazojulikana sana husema kwamba nyota hiyo ilikuwa ishara kutoka mbinguni. Je, hilo ni kweli?

▪ Nyota isiyo ya kawaida iliwavutia “mamajusi” kutoka Mashariki, na mwishowe iliwaongoza kwa mtoto mchanga Yesu, anaeleza mwandikaji wa Biblia, Mathayo. (Mathayo 2:1-12, Union Version) Hadithi za Krismasi zinazojulikana sana husema kwamba nyota hiyo ilikuwa ishara kutoka mbinguni. Kitabu kimoja kinasema kwamba nyota hiyo ilikuwa sehemu ya “mpango wa Mungu ili kuonyesha . . . kwamba Baba alimheshimu na kumkubali mtoto Yesu kuwa Mwana wake mpendwa.” Hata nyimbo za Krismasi huitukuza nyota hiyo. Nyota hiyo ilikuwa nini?

Watu fulani wamesema kwamba ilikuwa nyota ya kawaida. Wasomi wengi wamependekeza kwamba ni sayari mbalimbali zilizokuwa zikipishana karibu-karibu. Hata hivyo, kitabu The New Bible Dictionary kinasema kwamba “tukio hilo la kawaida haliwezi kutajwa kuwa ‘nyota.’” Sayari mbalimbali zinazopishana karibu-karibu haziwezi kuonekana kama nyota moja kwa kuwa kila sayari hutoa mwanga wake. Wengine wamedai kwamba nyota hiyo ilikuwa nyota-mkia au mlipuko wa nyota. Hata hivyo, hakuna yoyote kati ya vitu hivyo ambayo ingeweza kusafiri angani kwa njia ambayo ingewaongoza wanaume hao kwenye jiji hususa na kisha kutua juu ya nyumba fulani hususa.

Je, nyota hiyo ilikuwa tukio la kawaida au iliongozwa na Mungu? Fikiria mambo haya hakika: Wale “mamajusi” hawakuwa wasomi; wala hawakuwa wafalme. Tafsiri mbalimbali za kisasa zinasema walikuwa “wanajimu.” Walijihusisha na mazoea ambayo yameshutumiwa katika Maandiko Matakatifu. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Ona kwamba ni wanajimu hao tu wanaosemekana kuwa ‘waliiona’ hiyo nyota. Ikiwa nyota hiyo ingekuwa nyota ya kawaida, ingeonekana na kila mtu kama vile tu nuru nyangavu inavyoonekana na watu wote. Lakini hata Mfalme Herode alilazimika kuwauliza kuhusu nyota hiyo. Kwanza iliwaongoza wanajimu hao hadi Yerusalemu kwa Herode ambaye alikuwa adui wa mtoto Yesu ambaye angekuja kuwa Masihi. Herode alinuia kumwua Yesu. Kisha, nyota hiyo iligeuza mwelekeo na kuwaongoza wanajimu hao upande wa kusini hadi Bethlehemu ambako Yesu alikuwa, na hivyo kuhatarisha uhai wa Yesu.

Mambo hayo yanathibitisha kwamba nyota hiyo ilitoka kwa mtu mwovu, yaelekea Shetani Ibilisi. Biblia inasema kwamba yeye hutumia “ishara za uwongo na mambo ya ajabu.” (2 Wathesalonike 2:9) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli hawashangai kwamba Shetani anaweza kuwafanya wanajimu waone kitu kinachofanana na nyota na kisha kutumia kitu hicho kuwaongoza kwa Mwana wa Mungu, ambaye Shetani mwenyewe alitaka kumwangamiza. Bila shaka, hakuna mtu anayeweza kumshinda Yehova Mungu. Kwa hiyo, haishangazi kwamba njama ya Ibilisi ya kumwua Yesu akiwa mtoto haikufanikiwa.

Hata hivyo, ni jambo lenye kupendeza kwamba Mungu alitangaza kwa njia ya kimuujiza kuzaliwa kwa Yesu. Usiku ambao Yesu alizaliwa, malaika aliwatokea wachungaji na kutangaza kuzaliwa kwa “mwokozi.” Pia malaika huyo aliwapa mwelekezo ili wachungaji hao waweze kumtembelea Yesu. Kisha umati wa malaika ukatokea na kuanza kumsifu Mungu. (Luka 2:8-14) Mungu aliwatumia malaika hao na si nyota kuwajulisha watu kuhusu kuzaliwa kwa Yesu.