Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunastaajabishwa na Ulimwengu!

Tunastaajabishwa na Ulimwengu!

Tunastaajabishwa na Ulimwengu!

UTAFITI wa wanasayansi umetuwezesha kufahamu mambo mengi kuhusu jinsi ulimwengu unavyofanya kazi. Sasa wanadamu wanaweza kuuelewa vizuri zaidi, kuanzia chembe zake ndogo sana hadi anga lake kubwa. Hata hivyo, bado kuna mambo mengi sana ambayo kufikia sasa hatujayaelewa.

Dunia yetu ni ndogo sana inapolinganishwa na ulimwengu wote. Hata hivyo, tunastaajabishwa na utata na umaridadi wa vitu vya asili vilivyo duniani kama vile ua lenye kupendeza, mandhari yenye kuvutia, manyoya ya ndege yenye rangi nzuri, mabawa ya kipepeo, machweo yenye rangi nyekundu, au tabasamu ya mtu tunayempenda.

Watu wengi wamepata uthibitisho wa kutosha katika ulimwengu unaowafanya waamini kwamba kuna mtu mwenye akili ambaye ndiye Mwanzilishi wa vitu vyote. Wanasema kwamba inaonekana ni kama sheria za fizikia zimepimwa kwa usahihi ili ziweze kutegemeza uhai. Ikiwa vipimo hivyo vingetofautiana hata kwa kiasi kidogo tu, hakungeweza kuwa na uhai. Lakini tumezungukwa na unamna-namna mwingi sana wa uhai ambao ni maridadi sana.

Mtaalamu wa anga, Paul Davies anaandika hivi: “Ulimwengu unaposonga na kubadilika ni kana kwamba unafuata mpangilio fulani . . . Ulimwengu haukutokezwa na matukio yaliyotokea bila mpango bali ulitokezwa na sheria za hisabati ambazo zinapatana kwa ustadi.” Wanasayansi fulani wanakubaliana na Davies. Wengine hawakubaliani naye.

Kwa mfano, mtaalamu wa fizikia aliye pia mshindi wa Tuzo la Nobeli Steven Weinberg, aliandika hivi: “Kadiri ulimwengu uonekanavyo kuwa wenye kueleweka zaidi, ndivyo inavyozidi kuonekana kuwa vigumu kuelewa ni kwa nini upo.” Ingawa hivyo, Weinberg pia alisema kwamba “nyakati nyingine ni kana kwamba vitu fulani katika ulimwengu vipo tu kwa sababu ya umaridadi na si kwamba ni lazima viwepo. . . . Tunalazimika kufikia mkataa kwamba umaridadi huo wote ulitokezwa kwa faida yetu.”

Una maoni gani? Ikiwa kuna vipimo sahihi, si bila shaka lazima kuwe pia na Mpimaji Mkuu—Mbuni, Muumba—aliye na kusudi? Je, kuna kusudi la kuwepo kwa uhai na ulimwengu wetu? Au je, tupo hapa kwa sababu ya matukio fulani yaliyotokea bila mpango au mwelekezo wowote? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.