Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Umuhimu wa Kuonyesha Upendo

Umuhimu wa Kuonyesha Upendo

Umuhimu wa Kuonyesha Upendo

PROFESA wa magonjwa ya akili ya watoto alimwambia hivi mama ambaye ilikuwa mara ya kwanza kujifungua na akapata watoto mapacha, “wakumbatie mara nyingi!” Mama huyo alikuwa amemwomba mashauri ya jinsi ya kuwalea watoto wake vizuri. Profesa huyo aliendelea kusema hivi: “Upendo unapaswa kuonyeshwa kwa njia nyingi, kama vile kukumbatia na kupiga busu, shauku, kujali, furaha, ukarimu, kusamehe, na kutoa nidhamu inapohitajika. Hatupaswi kuwazia tu kwamba watoto wetu wanajua tunawapenda.”

Tiffany Field, ambaye ni msimamizi wa taasisi ya Touch Research ya Chuo Kikuu cha Miami, Florida, Marekani, anakubaliana na jambo hilo. Anasema, “Kumgusa mtoto ni muhimu sana kwa ukuzi na hali njema yake kama vile tu chakula chenye lishe na mazoezi.”

Je, watu wazima pia wanahitaji kuguswa ili kuonyeshwa upendo? Bila shaka. Kutokana na utafiti wake, Claude Steiner, ambaye ni mtaalamu wa tabia alifikia mkataa kwamba hata tuwe na umri gani, ili tuwe na hali njema ya moyoni tunahitaji kuambiwa maneno yenye kutia moyo na kuguswa. Laura, ambaye ni muuguzi anayetunza kikundi kikubwa cha wazee, anasema: “Nimeona jinsi kuwatendea wazee kwa upendo kunavyowasaidia sana. Unapowatendea kwa wororo na kuwagusa, wanakuamini na kufuata kwa hiari maelekezo unayotoa. Isitoshe, kuwatendea kwa njia hiyo kunaonyesha kwamba unawaheshimu.”

Zaidi ya hayo, kuonyesha upendo kunamnufaisha anayetoa na anayepokea pia. Kama Yesu alivyosema, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Watu wenye wasiwasi, waliovunjika moyo, na ambao hawana amani ya akili wanafaidika sana wanapoonyeshwa upendo. Matukio mengi katika Biblia yanaonyesha jinsi watu kama hao walivyosaidiwa.

Wazia jinsi “mwanamume mwenye kujaa ukoma,” mtu aliyetengwa na jamii, alivyofarijika alipoguswa kwa wororo na Yesu Kristo mwenyewe!—Luka 5:12, 13; Mathayo 8:1-3.

Fikiria jinsi nabii mzee Danieli alivyojihisi akiwa na nguvu baada ya malaika wa Mungu kumtia moyo na kumgusa mara tatu. Kuguswa huko kwa upendo na maneno mazuri ya kutia moyo ndiyo mambo ambayo Danieli alihitaji ili ajihisi akiwa mwenye nguvu baada ya kuchoka kimwili na kiakili.—Danieli 10:9-11, 15, 16, 18, 19.

Pindi moja, rafiki wapendwa wa mtume Paulo walisafiri umbali wa kilomita 50 hivi kutoka Efeso hadi Mileto ili waonane naye. Wakiwa huko, Paulo aliwaambia kwamba huenda wasimwone tena. Wazia jinsi mtume huyo alivyotiwa moyo rafiki hao waaminifu ‘walipomwaga kwa kumkumbatia na kumbusu’!—Matendo 20:36, 37, Biblia Habari Njema.

Hivyo, Biblia na utafiti wa kisasa unatutia moyo tuonyeshane upendo. Kutendewa kwa njia hiyo kunawanufaisha watu kimwili na kihisia. Kwa kweli, sisi sote tunahitaji kuonyeshwa upendo, si watoto tu.