Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kutosheleza Uhitaji Wako wa Kiroho

Unaweza Kutosheleza Uhitaji Wako wa Kiroho

Maoni ya Biblia

Unaweza Kutosheleza Uhitaji Wako wa Kiroho

WANADAMU wanahitaji mambo ya kiroho kama tu wanavyohitaji chakula. Hata hivyo, wanaweza kupata vyakula vingi vyenye lishe vinavyoweza kutegemeza uhai. Vipi kuhusu uhitaji wetu wa kiroho? Kuna mazoea mengi sana ya kitamaduni na ya kidini yanayosemekana kuwa yanaweza kututosheleza.

Watu wengi wasema kwamba maadamu unafanya jambo la kiroho, basi kile unachoamini na jinsi unavyoabudu si muhimu sana. Wewe una maoni gani? Je, ni jambo la maana kufikiria jinsi unavyotosheleza uhitaji wako wa kiroho? Biblia inasema nini?

Hali ya Kiroho ya Kweli Inahusisha Nini?

Biblia inafunua kwa nini tuna uhitaji huu wa kiroho kwenye Mwanzo 1:27: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Kwa kuwa Yehova Mungu ni roho, maneno hayo hayamaanishi kwamba tunafanana naye kimwili, bali kwamba tuna sifa kama zake. Kama Muumba wake, mwanadamu wa kwanza, Adamu, angeweza kuthamini na kuonyesha sifa kama vile upendo usio na ubinafsi, fadhili, huruma, haki, na kujizuia. Pia alipewa dhamiri, yaani, uwezo wa ndani wa kutambua yaliyo sawa na yasiyo sawa, ambao ungemwongoza atumie uhuru wake wa kuchagua kupatana na sheria za Mungu. Sifa hizo zilimfanya awe tofauti na wanyama akiwa na uwezo wa kufanya mapenzi ya Muumba wake kwa njia ya pekee.—Mwanzo 1:28; Waroma 2:14.

Biblia inaeleza kuhusu kitu fulani ambacho ni muhimu ili tutosheleze uhitaji wetu wa kiroho. Kwenye 1 Wakorintho 2:12-15, inamfafanua mtu wa kiroho kuwa yule anayepokea roho ya Mungu. Roho hiyo ni nguvu za utendaji za Mungu, na ni lazima roho hiyo itende ndani ya mtu ili aweze kujua mambo ya kiroho. Kwa sababu hiyo, mtu anayeongozwa na roho hiyo anaweza kuchunguza na kuelewa mambo kupatana na maoni ya Mungu. Kwa kutofautisha, mtu ambaye hana roho ya Mungu anaitwa mtu wa kimwili, ambaye anayaona mambo ya kiroho kuwa upumbavu. Kwa sababu hiyo, anafanya maamuzi kwa kutegemea hekima ya wanadamu tu.

Hivyo, kwa kuwa tuna uwezo wa kufikiri na kutenda kama Mungu kwa sababu tumeumbwa kwa mfano wake, hatuwezi kuwa na hali nzuri ya kiroho kupitia hekima ya wanadamu, mafanikio ya kibinafsi, au kwa kujua utu na uwezo wa kibinafsi. Tunahitaji roho ya Mungu. Hiyo ndiyo sababu wale wanaopinga utendaji wa roho ya Mungu, na badala yake wanachagua kufuata tamaa zao wenyewe na mambo yasiyompendeza Mungu, wanafafanuliwa kuwa watu wasio na hali ya kiroho. Wanaongozwa na tamaa na mapendezi ya kimwili tu.—1 Wakorintho 2:14; Yuda 18, 19.

Kutosheleza Uhitaji wa Kiroho

Ili kuwa na hali nzuri ya kiroho, lazima mtu kwanza amkubali Yehova kuwa Muumba na kutambua kwamba tuko hai kwa sababu yake. (Ufunuo 4:11) Kwa hiyo, tunatambua kwamba maisha yetu yanakuwa na kusudi wakati tu tunapofanya mapenzi yake. (Zaburi 115:1) Kufanya mapenzi ya Mungu kunatupa kusudi maishani, uhitaji wa kiroho ambao ni muhimu kama chakula cha kimwili. Ndiyo sababu Yesu, mtu aliyejulikana sana kwa sababu ya hali yake nzuri ya kiroho angeweza kusema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma.” (Yohana 4:34) Kufanya mapenzi ya Mungu kulimtia nguvu, kukamburudisha, na kumletea uradhi.

Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, ili kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho tunapaswa pia kupatanisha utu wetu na utu wake. (Wakolosai 3:10) Kwa kufanya hivyo, tunaepuka mwenendo unaotuvunjia heshima au unaoharibu uhusiano wetu na wengine. (Waefeso 4:24-32) Kuchagua kuishi kupatana na viwango vya Yehova kunaboresha maisha yetu na kutuletea amani ya kweli ya akili, kwa kuwa tunaepuka kuhukumiwa na dhamiri yetu.—Waroma 2:15.

Yesu alifunua kweli nyingine ya msingi kuhusu kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho aliposema: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Tunahitaji kuhangaikia hali yetu ya kiroho nyakati zote. Kupitia Biblia, Yehova anajibu maswali kuhusu maisha yetu, maswali ambayo kila mtu hujiuliza.—2 Timotheo 3:16, 17.

Chanzo cha Furaha ya Kweli

Mtu anaweza kutosheleza njaa yake kwa kula vyakula vitamu lakini visivyokuwa na lishe. Vivyo hivyo, huenda ikaonekana kwamba umetosheleza uhitaji wako wa kiroho kwa “kujijaza” mambo au falsafa za kibinadamu. Lakini kama vile tu kula chakula kisicho na lishe nzuri kunavyoweza kutokeza utapiamlo, magonjwa, au hatari nyingine kubwa, tusipotosheleza uhitaji wetu wa kiroho kwa njia inayofaa tutapatwa na madhara.

Hata hivyo, tukisitawisha uhusiano wa karibu na Yehova Mungu, tukichagua kufanya mapenzi yake, na tukifuata mwongozo wake, tutaona ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Kwa nini wanadamu wana uhitaji wa kiroho?—Mwanzo 1:27.

▪ Je, tunaweza kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho bila msaada wowote?—1 Wakorintho 2:12-15.

▪ Tunapaswa kufanya nini ili tutosheleze uhitaji wetu wa kiroho?—Mathayo 4:4; Yohana 4:34; Wakolosai 3:10.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Tusipotosheleza uhitaji wetu wa kiroho kwa njia inayofaa tutapatwa na madhara