Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Acheni Kuhangaika”

“Acheni Kuhangaika”

“Acheni Kuhangaika”

“Pesa zote katika akaunti yetu ya benki zilikwisha kutia ndani zile tulizokuwa tumewawekea watoto wetu akiba. Kwa miezi mingi sana hatukuwa tukipata pesa zozote.”

● Nilisimamia shule moja katika eneo la vijijini la India na ilikuwa ikiendelea vizuri. Wakati mmoja kulikuwa na wanafunzi 500 hivi. Kisha, shule moja ya kifahari ya jijini ikaanza kutuma mabasi katika eneo letu, na ikarahisisha mambo ili wanafunzi waweze kujiunga na shule hiyo. Wanafunzi wengi kutoka katika shule yangu walihamia shule hiyo ya jijini. Idadi ya wanafunzi katika shule yangu ilipungua kutoka 500 hivi hadi 60 hivi. Isitoshe, karibu na kipindi hichohicho mtu fulani aliyekuwa na deni langu la kifedha alishindwa kunilipa. Kwa kuwa kulikuwa na wafanyakazi wengi katika shule yangu ambao ilikuwa lazima niwalipe mshahara, nilikabili tatizo kubwa la kifedha.

Tuliketi chini tukiwa familia na kuzungumzia hali hiyo. Sote tulionyesha roho ya kujidhabihu kwa kujitahidi kufuata himizo la Yesu la kuwa na ‘jicho rahisi’ kuhusiana na pesa, yaani, kutonunua vitu vingi kuliko uwezo wetu. (Mathayo 6:22, 25) Kwa muda fulani, tulilazimika kuacha kutumia gari letu kwa sababu ya gharama za mafuta na za kulidumisha. Tulipunguza gharama za chakula kwa kununua vitu jioni sana, wakati ambapo bei ya chakula ilikuwa imepunguzwa. Pia tulipunguza idadi ya vyakula tulivyokula kila mlo.

Sisi ni Mashahidi wa Yehova, na kwa sababu hiyo tunaona kwamba ni muhimu kukusanyika pamoja na waumini wenzetu katika mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:25) Ingawa hali yetu ya kifedha ilikuwa ngumu, tuliazimia kwamba hatutakosa mikutano na makusanyiko—hata ikiwa hilo lilimaanisha kusafiri mbali sana. Huduma yetu—ambayo inahusisha kuwafundisha watu Biblia—inatia ndani kwenda kwenye maeneo ya mbali. Tulitumia pikipiki ndogo aina ya skuta badala ya gari ili kufanya kazi hiyo. Bila shaka, ni watu wawili tu wanaoweza kutumia skuta kwa wakati mmoja.

Lakini hilo halikumaanisha eti tulitumia muda mfupi zaidi katika huduma. Badala ya hivyo, mke wangu na binti yetu walianza kutumia wakati mwingi zaidi kuzungumza na wengine kuhusu Biblia. Nyakati nyingine walitembea kilomita sita hadi nane kwenda na kurudi ili kujifunza Biblia na watu waliopendezwa. Pia, mimi na mwanangu tulijitahidi kutumia wakati mwingi zaidi kuwafundisha watu kuhusu Biblia.

Sasa hali yetu ya kifedha ni afadhali zaidi. Hata hivyo, hali yetu imetufundisha tusitegemee sana vitu vya kimwili. Pia tumejifunza kutohangaikia kupita kiasi mambo ambayo hatuwezi kubadili. Andiko la Zaburi 55:22 limetutia moyo sana. Linasema hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” Maneno hayo yalithibitika kuwa ya kweli kabisa tulipokuwa na matatizo ya kifedha!—Tumetumiwa makala hii.