Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ibada ya Nyoka—Nyakati za Kale na Sasa

Ibada ya Nyoka—Nyakati za Kale na Sasa

Ibada ya Nyoka—Nyakati za Kale na Sasa

WAMISRI wa kale waliabudu nyoka, kama tu Waminoa walioishi Krete nyakati za kale. Baadhi ya Waisraeli wa kale walitoa dhabihu kwa nyoka wa shaba. Wengine kutoka taifa hilohilo walianza pia kufukiza uvumba mbele ya “vitu vyenye kutambaa.”—Ezekieli 8:10-12; 2 Wafalme 18:4.

Zamani za kale ibada ya miungu yenye umbo la nyoka ilikuwa imekita mizizi nchini Mexico. Nyakati nyingine sanamu ya mungu mkuu wa Wamaya—Itzamná—ilikuwa ni nyoka. Quetzalcoatl, yaani, “nyoka mwenye manyoya,” alikuwa mungu wa masomo, utamaduni, na falsafa kwa Watolteki. Waazteki pia walimwona mungu huyo kuwa mungu wa masomo na pia muumba wa wanadamu. Gazeti Arqueología Mexicana (Gazeti la Uchimbuzi la Mexico) linasema hivi kuhusiana na mungu huyo mwenye majukumu mengi na vipawa: “Nyoka huyo mwenye manyoya alikuwa na maana nyingi mbalimbali, huenda hata kuliko mungu mwingine yeyote.”

Kwa karne nyingi, wakazi wa Mesoamerika waliabudu nyoka huyo mwenye manyoya. Leo, bado watu wa makabila ya Cora na Huichol huko Mexico wanamwabudu mungu huyo. Kwenye siku fulani za sherehe, waumini hucheza dansi wakiwa wamevalia manyoya na kusonga kama nyoka. Wakati wa sherehe za ibada ya uzazi, watu wa kabila la Quiche hucheza dansi kwa kutumia nyoka walio hai. Watu wa kabila la Chorti, ambacho ni kikundi cha Wamaya nchini Guatemala, huabudu nyoka fulani wa manyoya ambaye wao humhusianisha na watakatifu fulani Wakatoliki.

Swali ni hili, Muumba wa wanadamu na wanyama, kutia ndani nyoka, ana maoni gani kuhusu ibada ya miungu-nyoka?

Maoni ya Mungu Kuhusu Ibada ya Nyoka

Yehova Mungu alitoa amri hii kwa taifa la kale la Israeli: “Usijifanyie sanamu ya kuchongwa wala umbo lililo kama kitu chochote kilicho juu mbinguni wala kilicho chini duniani wala kilicho ndani ya maji chini ya dunia. Usiviinamie wala kushawishiwa kuvitumikia.”—Kutoka 20:4, 5.

Yehova aliwakataza watu wake wasiabudu mifano ya wanyama, kama vile nyoka. Kwa hiyo, je, hilo halionyeshi wazi kwamba wale wanaotaka kupata kibali chake wanapaswa kuepuka ibada ya nyoka? Kwa nini Mungu anapinga ibada ya sanamu, kutia ndani ibada ya nyoka? Jibu ni rahisi: Yeye ndiye amewapa wanadamu, nyoka, na viumbe wengine wote uhai. Yeye ndiye ameumba vitu vyote hivyo, kwa hiyo yeye ndiye anayepaswa kuabudiwa, si vitu alivyoviumba.

Kwa mfano: Tuseme kwamba mchoraji wa ramani za ujenzi alijenga nyumba na kuwapa watu wa familia mbalimbali nyumba hizo waishi na kufurahi. Namna gani ikiwa familia hizo zingeshukuru na kusifu nyumba hizo badala ya kumsifu mchoraji wa ramani? Huo ungekuwa upumbavu, na pia jambo hilo lingemuudhi mchoraji wa ramani. Vivyo hivyo, kuabudu wanyama badala ya Muumba wake ni jambo lenye kuchukiza kwa Mungu.

Kwa wazi, wale ambao wangependa kupata kibali cha Mungu wanapaswa kutii onyo lililotolewa na mtume Yohana: “Watoto wadogo, jilindeni na sanamu.”—1 Yohana 5:21.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

KUABUDU UKIWA UMESHIKA NYOKA

● Makanisa fulani kusini-mashariki mwa Marekani, huabudu wakiwa wameshika nyoka wenye sumu walio hai. Watu fulani huzungusha nyoka mwenye sumu juu ya mabega yao huku wengine wakiwabeba nyoka kadhaa kwa wakati mmoja. Kuwainua na kuwasogeza nyoka kunaweza kuwafanya washtuke na kumwuma mtu. Kwa miaka mingi, watu fulani wamekufa kwa sababu ya kuumwa na nyoka walipokuwa wakiabudu.

Watu wanaotumia nyoka kwa njia hiyo katika ibada wanataja Marko 16:17-18 kuwa msingi wa kufanya hivyo. Mistari hiyo inatia ndani maneno haya: “Watainua nyoka kwa mikono yao.” Tafsiri ya Biblia ya King James Version na tafsiri nyingine huonyesha kuwa mistari hiyo ilikuwa sehemu ya maandishi ya awali. Hata hivyo, tafsiri za New Revised Standard Version, New American Standard Bible, na The New King James Version zinaonyesha kwamba mistari hiyo haipatikani katika hati za zamani za Injili ya Marko.

Mafundisho ya Biblia hayaungi mkono wazo la kwamba kushika nyoka ni sehemu inayokubalika ya ibada ya kweli. Biblia inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Huenda utakubali kwamba Muumba wetu mwenye upendo hawezi kuwatazamia waabudu wake wa kweli wafuate desturi fulani hatari ili wampendeze. Mwana wake, Yesu, alitoa mwaliko huu: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi.” (Mathayo 11:28, 29) Kwa kweli, kushika nyoka na kupatwa na maumivu, ugonjwa, na hata kifo kinachosababishwa na kuumwa na nyoka si jambo ambalo Yehova na Yesu anataka kiwapate wafuasi wao!

[Hisani]

REUTERS/Tami Chappell

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kichwa cha nyoka mwenye manyoya kwenye ukuta wa hekalu la Waazteki

[Picha katika ukurasa wa 22]

Sanamu ya Quezalcoatl, nyoka mwenye manyoya mungu wa Watolteki

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]

Top: REUTERS/Tami Chappell; bottom: © Leonardo Díaz Romero/age fotostock