Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Bado Sehemu Zote za Biblia Zina Manufaa?

Je, Bado Sehemu Zote za Biblia Zina Manufaa?

Maoni ya Biblia

Je, Bado Sehemu Zote za Biblia Zina Manufaa?

“Biblia haina thamani kubwa kwa wanadamu leo, mbali na kujua tu mambo yatakayowasaidia kujibu maswali katika michezo mbalimbali.”

“Maandiko ya Biblia yanayohusu ukoo, ubikira, na kumwogopa Mungu yalikuwa na faida katika nyakati za Biblia, lakini hayana thamani kubwa katika Karne ya 21.”

“Biblia ilikuwa imepitwa na wakati hata kabla ya kuchapishwa kwa mara ya kwanza.”

MANENO hayo yalitolewa hivi karibuni katika Tovuti ya Intaneti iliyokuwa na kichwa “Je, Biblia imepitwa na wakati?” Una maoni gani kuhusu maneno hayo? Je, unakubaliana nayo?

Huenda ukapinga maneno kama hayo, lakini bado ukajiuliza ikiwa kila kitu katika Biblia kina manufaa. Isitoshe, Biblia zinazotumiwa katika makanisa mengi zimegawanywa katika sehemu mbili, Agano la Kale na Agano Jipya na hilo linatoa wazo la kwamba asilimia 75 ya Biblia imepitwa na wakati.

Hakuna mtu anayetoa dhabihu za wanyama zilizotajwa katika Sheria ya Musa. Kwa hiyo, kuna faida gani ya kuhifadhi habari zote kuhusu dhabihu zilizo katika kitabu cha Mambo ya Walawi? (Mambo ya Walawi 1:1–7:38) Namna gani kuhusu sura za kwanza za 1 Mambo ya Nyakati, ambazo huzungumzia orodha ya majina ya watu wa ukoo? (1 Mambo ya Nyakati 1:1–9:44) Orodha hizo zina manufaa gani ikiwa hakuna mtu yeyote leo anayeweza kufuatia ukoo wake kwa kuzitumia?

Hebu wazia ukichuma tunda la tofaa kutoka katika mtofaa. Ukiwa na tunda hilo mkononi, je, inamaanisha kwamba mti huo hauna manufaa tena? Sivyo, ikiwa utahitaji matunda tena! Kwa njia fulani Biblia ni kama mtofaa huo. Huenda ikawa sehemu fulani za Biblia, kama vile Zaburi au Mahubiri ya Mlimani zikawa rahisi kusoma na zenye kuvutia. Kwa kuwa tunavutiwa na sehemu hizo za Biblia kama tu tunavyopendezwa na tunda fulani, je, tupuuze sehemu zile nyingine za Biblia? Biblia yenyewe ina maoni gani kuhusu jambo hilo?

Katika mwaka wa 65 W.K. hivi, mtume Paulo aliandika barua yake ya pili kwa Timotheo akimkumbusha hivi: “Tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” Kisha Paulo akaendelea kumwambia: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:15, 16) Paulo alipoandika kwamba “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida,” je, alikuwa akizungumza tu kuhusu maandiko ya Agano Jipya?

Ona kwamba Paulo anamkumbusha Timotheo kuwa alijifunza “maandishi matakatifu” tangu “utoto mchanga.” Ikiwa kama watu fulani wanavyoamini kuwa Timotheo alikuwa na umri wa miaka 30 hivi wakati barua hii ilipoandikwa, basi alikuwa mtoto mchanga wakati wa kifo cha Yesu. Hiyo ilikuwa kabla ya sehemu yoyote ya Agano Jipya, au Maandiko ya Kigiriki kuandikwa. Mama ya Timotheo alikuwa Myahudi, basi ni wazi kuwa alimfundisha Agano la Kale, au Maandiko ya Kiebrania. (Matendo 16:1) Paulo aliposema “kila Andiko” ni wazi kwamba alitia ndani maandiko yote ya Agano la Kale, yaliyotia ndani sheria kuhusu kutoa dhabihu na orodha ya majina ya watu wa ukoo.

Miaka 1,900 hivi baadaye, bado tunafaidika kwa njia mbalimbali tunaposoma sehemu hizo zote za Biblia. Kwanza kabisa, hatungekuwa na Biblia iwapo Mungu hangeongoza kuandikwa na kuhifadhiwa kwake na wanadamu ambao aliwachagua. (Waroma 3:1, 2) Katika Israeli la kale, Sheria ya Musa haikuwa tu kitu kitakatifu cha kuhifadhiwa kwa ajili ya vizazi vya wakati ujao, lakini ilikuwa katiba ya taifa hilo. Mambo katika Sheria hiyo ambayo huenda yakaonekana si ya lazima kwetu leo, yalikuwa ya maana kwa hali njema ya taifa la Israeli. Isitoshe, rekodi za orodha za watu wa ukoo katika Biblia zilikuwa muhimu kumtambulisha Masihi, ambaye ilitabiriwa angekuwa mzao wa Mfalme Daudi.—2 Samweli 7:12, 13; Luka 1:32; 3:23-31.

Ingawa Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, wanapaswa kuwa na imani katika Masihi aliyetabiriwa, Yesu Kristo. Orodha za kale za watu wa ukoo zilizohifadhiwa katika Biblia zinathibitisha kwamba kwa kweli Yesu alikuwa “mwana wa Daudi” aliyeahidiwa. Na habari kuhusu dhabihu zilizotolewa zinaongeza uthamini wetu kwa dhabihu muhimu zaidi ambayo Yesu alitoa, na hivyo kutufanya tuwe na imani yenye nguvu kuielekea.—Waebrania 9:11, 12.

Paulo aliandikia hivi kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza la Roma: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Andiko hilo linatukumbusha kwamba Biblia haikuandikwa kwa faida yetu tu bali pia kwa faida ya watu wengine. Kwa zaidi ya miaka 3,500, maneno yake yaliyoongozwa kwa roho yamewaelekeza, yakawafundisha, na kuwasahihisha watu wa Mungu katika nyika ya Sinai, katika Nchi ya Ahadi, katika uhamisho wa Babiloni, katika Milki ya Roma, na sasa ulimwenguni pote. Hakuna kitabu kingine ambacho kinaweza kusema kimetimiza jambo hilo. Kama vile huwezi kuona mizizi ya mtofaa, inaweza kuwa vigumu kuona thamani ya sehemu fulani za Biblia. Huenda ukahitaji kuchimba zaidi ili uone thamani yake, lakini utathawabishwa sana unapofanya hivyo!

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Timotheo aliyajua “maandishi matakatifu” kwa muda gani?—2 Timotheo 3:15.

● Ni sehemu gani za Biblia zenye manufaa na zilizoongozwa na roho ya Mungu?—2 Timotheo 3:16.

● Tunaweza kunufaika jinsi gani kutokana na “mambo yote yaliyoandikwa zamani”?—Waroma 15:4.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Habari zilizo katika Biblia zinaweza kuongeza uthamini wetu kwa dhabihu ya Yesu