Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Tatizo la Maji—Linashughulikiwa Jinsi Gani? (Januari 2009) Sikufurahishwa na umalizio wa habari hiyo. Badala ya kuwatia moyo wasomaji wawasaidie watu kwa kuchimba visima, kuunga mkono miradi ya kuhifadhi maji, au hata kushughulikia tatizo hilo kwa njia nyingine, habari hiyo inasema hivi: “Suluhisho halisi kwa tatizo la maji linaweza kupatikana tu kutoka kwa Mungu na si mwanadamu” na kwamba “‘atafanya vitu vyote kuwa vipya.’ (Ufunuo 21:5)” Ingawa hilo ni jambo lenye kutia moyo, je, haingefaa kujitahidi kusaidia kwa njia fulani tukisubiri wakati huo? Kuna matatizo mengi sana katika ulimwengu huu. Ingawa kwa kweli Mungu amepangia jinsi ya kusuluhisha mambo, hatuwezi kusubiri tu bila kufanya chochote huku Ibilisi akifanya anachotaka.

S. S., Marekani

“Amkeni!” lajibu: Kusudi la habari iliyotajwa halikuwa kuonyesha kwamba watu hawapaswi kujitahidi kuboresha mambo sasa. Kama vile habari hiyo ilivyosema, “Mungu aliwapa wanadamu jukumu la kutunza sayari hii.” Hivyo, tumechapisha habari nyingi katika magazeti yetu inayowatia moyo wasomaji wajitahidi kuhifadhi mali za asili za dunia pamoja na mazingira. Hata hivyo, kwa kusikitisha mara nyingi jitihada za wanadamu za kutunza mali za asili za dunia huzuiwa na sheria zinazopendelea ukuzi wa kiuchumi badala ya kutunza mazingira na pia zimezuiwa na pupa na ubinafsi ambao wanadamu wasio wakamilifu wamerithi. Hiyo ndiyo sababu inayotufanya tuseme kwamba “suluhisho halisi kwa tatizo la maji linaweza kupatikana tu kutoka kwa Mungu.”

Dunia Imekusudiwa Itegemeze Uhai (Februari 2009) Kwa kuwa vyombo vya habari vinatufanya tuwe na wasiwasi kwa kuandika tu kuhusu kuongezeka kwa joto duniani, kusoma habari hizo kulinifanya niwe na amani ya akili. Nilitiwa moyo pia kujua kwamba wakati ujao wa dunia si mbaya kwani dunia itakuwa paradiso kimwili na kiroho na wanadamu wataishi kwa amani. Asanteni sana.

M. H., Japani

Dyslexia Haijanizuia Kufikia Miradi Yangu (Februari 2009) Mimi pia nina tatizo la dyslexia, na kwa kusikitisha sikujua tatizo langu ni baya kwa kadiri gani hadi mimi na mke wangu tulipopewa mgawo wa umishonari na nikajaribu kujifunza lugha nyingine. Habari hiyo ilinitia moyo sana, hasa sanduku kwenye ukurasa wa 22, ambalo lilinisaidia kuelewa tatizo langu. Nilitiwa moyo niliposoma jinsi Michael Henborg alivyojitahidi kujifunza lugha mbalimbali. Asanteni sana.

M. M., Tanzania

Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kusoma Biblia? (Aprili 2009) Nina tatizo la kuona na mimi hutumia vitabu vyenye maandishi ya vipofu shuleni. Ninathamini sana vichapo vyenu ambavyo vimenisaidia kukabiliana na matatizo yangu mengi. Mimi husikiliza kaseti na CD zenu kabla ya kulala. Hilo hunisaidia kulala nikiwa na mawazo yanayofaa akilini. Nilisikiliza habari hiyo angalau mara tano na nikaona mambo ninayoweza kutumia kuboresha funzo langu la kibinafsi.

S. H., Ufaransa