Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

“Watu ambao hawavuti sigara, wanafanya mazoezi, wanakunywa kileo kwa kiasi, na wanakula matunda au mboga angalau mara tano kwa siku, wanaishi wastani wa miaka 14 zaidi ya watu wengine.” Mkataa huo ulifikiwa baada ya kuwafanyia watu 20,000 uchunguzi kwa miaka 11.—UC BERKELEY WELLNESS LETTER, MAREKANI.

“Kusoma ndiyo njia bora ya kustarehe. . . . Hata dakika sita tu zinatosha kupunguza mfadhaiko kwa asilimia 66.”—INDIA TODAY INTERNATIONAL, INDIA.

Watu Wanatupa Mashua Zao

“Hali mbaya ya kiuchumi inawafanya watu waache kutumia mashua zao,” linasema gazeti The New York Times likisimulia kuhusu hali nchini Marekani. Wanaomiliki mashua hizo wanafuta majina kutoka kwenye mashua zao, wanaondoa nambari za usajili, kisha wanaziacha baharini au kuzizamisha, nyakati nyingine wakitafuta kulipwa bima. Kwa nini wanafanya hivyo? “Wengine . . . wanakabili tatizo lilelile linalowakabili wenye nyumba: hawawezi kulipa mkopo huku thamani ya kitu wanachomiliki ikizidi kupungua na hivyo wanaamua kutoendelea kulipa,” linasema gazeti Times, ambalo linasema kuwa mashua hizo ni “vifaa vya kuchezea vya bei ghali na visivyopendeza tena.” Gazeti hilo linaeleza hivi: “Wanaozimiliki hawawezi kuziuza kwa kuwa soko limelemewa. Hawawezi kulipa mamia ya dola kila mwezi ili kupata mahali pa kuegesha mashua hizo na pia kuzitunza. Na hawana maelfu ya dola zinazohitajika ili wapate hati zinazoonyesha kuwa mashua hizo si mali yao tena.”

Watoto Wanaohangaishwa na Miili Yao

Watoto wadogo wenye umri wa miaka minne hivi “wanajaribu kubadili jinsi wanavyoonekana ili miili yao ifaane na maoni ya jamii,” linaripoti gazeti Sunday Telegraph la Sydney. Uchunguzi wa tabia za kula na kufanya mazoezi za wavulana na wasichana wenye umri huo ulionyesha kwamba wanahangaishwa na miili yao—wasichana wangependa kupunguza uzito na wavulana wangependa kujenga misuli. “Ilionekana kwamba watoto walikuwa na maoni ya mama zao [ambao] kwa kawaida hawavutiwi na miili yao wenyewe,” wakasema wachunguzi hao.

Watoto Wananunua Vitu Kwenye Intaneti

“Asilimia 20 ya watoto [nchini Uingereza] wananunua vitu kwenye Intaneti bila ruhusa ya wazazi wao na nusu kati yao wanatumia kadi za mkopo za wazazi wao,” linaripoti gazeti The Daily Telegraph la London. Watoto wengi kati yao wanajua Tovuti na maneno ya siri ambayo wazazi wao hutumia wanaponunua vitu kupitia Intaneti—jambo ambalo hufanya iwe rahisi kwao kupata namba ya kadi ya mkopo ya wazazi wao. Wazazi wengi wanadhani kwamba watoto wao hawawezi kununua vitu kwenye Intaneti bila ruhusa yao. Kuna “tofauti kubwa sana” kati ya kile wazazi wanafikiria watoto wao wanajua na kile ambacho kwa kweli watoto wanajua, inasema ripoti hiyo. Licha ya hayo, tabia hiyo inawafanya wazazi wakabili hatari ya kulaghaiwa. Wazazi wanaonunua vitu kwenye Intaneti wanashauriwa hivi: “Usiwe ukihifadhi habari kuhusu kadi zako za mkopo kwenye Intaneti,” tumia tu Tovuti zenye kuaminika, na “usiache Tovuti ikiwa wazi unapomaliza shughuli zako.”