Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbinu 20 za Kutafuta Wakati Zaidi

Mbinu 20 za Kutafuta Wakati Zaidi

Kata na Uhifadhi

Mbinu 20 za Kutafuta Wakati Zaidi

“Endeleeni kutembea kwa hekima . . . , mkijinunulia wakati unaofaa.”—Wakolosai 4:5.

BAADA ya kutambua utendaji unaotaka kufanya, changamoto ni kutafuta mbinu ya kutimiza mambo hayo. Madokezo yafuatayo yanaweza kukusaidia kufanya hivyo.

1 KILA SIKU ANDIKA MAMBO UNAYOTAKA KUTIMIZA. Orodhesha mambo kulingana na yale unayotaka kutimiza kwanza. Tia alama mambo utakayohitaji kutumia wakati mwingi zaidi. Tia alama unapomaliza kuyafanya. Tia mambo unayoshindwa kumaliza kwenye orodha ya siku inayofuata.

2 HAKIKISHA KUWA KALENDA ZAKO ZINAPATANA. Usikose kufanya jambo muhimu kwa sababu hukuliandika katika kalenda zako zote. Ikiwa unatumia kalenda iliyo ndani ya kompyuta yako na nyingine katika kifaa cha elektroniki cha kubeba mkononi, hakikisha kwamba zote zinapatana.

3 ANDIKA “MIKAKATI” itakayotia ndani kila hatua ya jambo unalotaka kufanya, na uzipange katika mpangilio unaofaa.

4 PANGIA MAMBO MUHIMU KWANZA. Itakuwa rahisi kupata wakati wa kufanya mambo yasiyo muhimu.

5 JIWEKEE MIRADI AMBAYO UNAWEZA KUTIMIZA. Una uwezo wa kuboresha stadi zako za kazi, lakini huna uwezo wa kuamua ikiwa utakuwa msimamizi wa kampuni.

6 TAMBUA KWAMBA HUTAPATA WAKATI WA KUFANYA KILA KITU. Chagua kufanya mambo yatakayoleta matokeo bora. Vipi kuhusu mambo ambayo yanapaswa kushughulikiwa haraka au ambayo lazima yafanywe tu? Ikiwa hayawezi kuepukwa au kufanywa na mtu mwingine, jaribu kutumia muda mfupi iwezekanavyo kuyafanya. Mambo fulani yasiyo muhimu yanaweza kusubiri kwa miezi kadhaa ikiwezekana, au si lazima yafanywe. Tenga wakati mwingi iwezekanavyo ili ufanye mambo unayoona kuwa ni muhimu zaidi na yanayopatana na miradi yako.

7 ORODHESHA JINSI UNAVYOTUMIA WAKATI WAKO. Andika orodha ya mambo unayofanya kwa juma moja au mawili ili ujue jinsi unavyotumia wakati wako. Je, unapoteza wakati mwingi kwa kufanya mambo yasiyo muhimu? Je, kila wakati shughuli zako huvurugwa na mtu au watu walewale? Je, shughuli zako huvurugwa wakati fulani hususa katika siku au juma? Achana na mambo yanayopoteza wakati wako.

8 RATIBU MAMBO MACHACHE ZAIDI. Huenda ukahisi kwamba unaharakishwa na huenda usifurahie chochote ikiwa utapangia katika siku ileile kununua chakula, kurekebisha gari, kualika wageni, kuona sinema, na kusoma.

9 PUNGUZA MAMBO YANAYOVURUGA SHUGHULI ZAKO. Tenga wakati fulani kila siku ambao hutavurugwa isipokuwa iwe lazima kabisa. Ikiwezekana, zima simu yako wakati huo. Pia, zima programu zozote za kompyuta zinazotokeza habari ghafula kwenye kiwambo chako ikiwa zinavuruga kazi yako.

10 PANGIA KUFANYA KAZI NGUMU ZAIDI WAKATI AMBAPO UNAJUA UNA NGUVU ZAIDI NA UNAWEZA KUWA MAKINI.

11 FANYA KAZI ISIYOPENDEZA ZAIDI HARAKA IWEZEKANAVYO. Unapomaliza kazi hiyo, utajihisi una nguvu za kufanya kazi rahisi zaidi.

12 TENGA WAKATI KWA AJILI YA MAMBO YASIYOTAZAMIWA. Ukihisi unaweza kufika mahali fulani katika muda wa dakika 15, ahidi kwamba utafika baada ya dakika 25. Ukijua kwamba mkutano fulani utachukua saa zima, pangia kutumia saa moja na dakika 20. Tenga wakati fulani wa siku ambao hujapangia kufanya chochote.

13 FANYA JAMBO FULANI UNAPOSUBIRI. Sikiliza habari au rekodi fulani unaponyoa ndevu. Soma huku ukisubiri treni au unaposafiri. Bila shaka, unaweza kutumia wakati huo kupumzika. Lakini usiupoteze kisha baadaye ulalamike kwamba huna wakati.

14 RAHISISHA KAZI. Je, mambo 2 kati ya 10 ndiyo muhimu zaidi katika orodha yako? Ukifanya ile sehemu muhimu ya kazi fulani, je, utakuwa umeikamilisha kazi yote?

15 UNAPOHISI UMELEMEWA NA KAZI, andika kila kazi kwenye kadi ndogo. Kisha gawa kadi hizo katika vikundi hivi viwili: “Mambo ya Kufanya Leo” na “Mambo ya Kufanya Kesho.” Kesho inapofika fanya vivyo hivyo.

16 PUMZIKA MARA KWA MARA UPATE NGUVU TENA. Kurudi kazini ukiwa umetulia kiakili na kimwili kunaweza kunufaisha zaidi kuliko kufanya kazi ya ziada kwa saa nyingi.

17 ANDIKA MAWAZO YAKO. Andika tatizo, fafanua kwa nini linakutatiza, na uorodheshe njia zote za kulisuluhisha unazoweza kufikiria.

18 USITAZAMIE UKAMILIFU. Tambua wakati wa kuacha jambo fulani na kuanza lingine.

19 FANYA KAZI KAMA MTAALAMU. Usisubiri wakati unajihisi vizuri. Anza kufanya kazi mara moja.

20 BADILIKANA NA HALI. Haya ni mapendekezo, si sheria kali. Jaribu mbinu mbalimbali, tambua zile zinazokufaa, na ujaribu kuzitumia.