Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kinachotufanya Tuwe Wema au Waovu?

Ni Nini Kinachotufanya Tuwe Wema au Waovu?

Maoni ya Biblia

Ni Nini Kinachotufanya Tuwe Wema au Waovu?

HISTORIA imejaa chuki na umwagaji wa damu. Hata hivyo, mara nyingi kunapokuwa na matukio mabaya watu hutenda kwa fadhili na wanajidhabihu. Kwa nini mtu mmoja anakuwa mwuaji mkatili na mwingine anakuwa mfadhili mwenye upendo? Kwa nini nyakati nyingine wanadamu hutenda kama wanyama?

Kutokamilika na Dhamiri

Biblia inasema hivi waziwazi: “Mawazo ya moyo wa mutu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwanzo 8:21, Zaire Swahili Bible) Hivyo, watoto wana mwelekeo wa kuwa watundu. (Methali 22:15) Tangu tunapozaliwa, sisi sote tuna mwelekeo wa kutenda mabaya. (Zaburi 51:5) Lazima tutie jitihada nyingi sana ili tutende mema, kama tu kupiga makasia dhidi ya mkondo wa mto.

Hata hivyo, tumepewa pia dhamiri. Hisi hiyo tuliyozaliwa nayo ya kuamua mema na mabaya inatuchochea kutenda kwa njia ambayo watu wengi huona kuwa inafaa. Kwa sababu hiyo, hata watu ambao hawajafundishwa mambo ya kiadili wanaweza kutenda kwa njia nzuri. (Waroma 2:14, 15) Hata hivyo, kama ilivyotajwa juu, mwelekeo wetu wa kufanya makosa unaweza kusababisha pigano ndani yetu. Ni nini kingine kinachoweza kutuchochea tufanye mema au mabaya?

Mazingira Yaliyochafuliwa

Kinyonga hubadili-badili rangi ili afaane na mazingira yake. Vivyo hivyo, wale ambao hufanya urafiki na wahalifu wanaweza kuiga tabia zao kwa urahisi. Biblia inaonya hivi: “Usiufuate umati kwa ajili ya makusudio maovu.” (Kutoka 23:2) Kwa upande mwingine, kushirikiana kwa ukawaida na watu wanyoofu, wenye haki, na wenye maadili mazuri kunaweza kutuchochea kufanya mema.—Methali 13:20.

Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba hatuwezi kuathiriwa na uovu kwa sababu tu hatushirikiani moja kwa moja na watu wanaotenda maovu. Kwa sababu ya kutokamilika kwetu, uovu unaweza kujificha ndani ya akili zetu, ukisubiri wakati wa kujitokeza. (Mwanzo 4:7) Isitoshe, uovu unaweza kuingia nyumbani kupitia vyombo vya habari. Mara nyingi, michezo ya video, vipindi vya televisheni, na sinema hutukuza jeuri na matendo ya kulipiza kisasi. Hata kutazama na kusoma habari za ulimwengu au za eneo la kwenu zinaweza kukufanya uwe sugu kuhusiana na maovu ya kuteseka kwa wanadamu.

Ni nini mzizi wa mazingira haya yaliyochafuliwa? Biblia inajibu hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Huyo “mwovu,” yaani, Shetani Ibilisi, anafichuliwa katika Maandiko kuwa mwongo na muuaji. (Yohana 8:44) Anaendeleza uovu kupitia uvutano wa ulimwengu wake.

Kwa kuwa mitazamo na matendo yetu huathiriwa na mambo hayo yote, huenda watu fulani wakasema kwamba hawapaswi kulaumiwa wanapotenda maovu. Hata hivyo, ukweli ni nini? Kama tu usukani unavyoelekeza gari au meli, akili ndiyo huelekeza mwili.

Wema au Uovu—Chaguo Ni Lako

Kabla ya kufanya tendo jema au baya, lazima kwanza mtu aliwazie. Tukipanda mawazo mazuri na yanayofaa tutatenda mambo mema. Vivyo hivyo, mbegu za tamaa za kibinafsi zinaporuhusiwa kukua akilini, zitatokeza uovu chungu nzima. (Luka 6:43-45; Yakobo 1:14, 15) Hivyo, tunaweza kusema kwamba mtu huwa mwema au mwovu kwa kiwango anachochagua.

Kwa kupendeza, Biblia inaonyesha kwamba tunaweza kujifunza kutenda mema. (Isaya 1:16, 17) Upendo ndio unaotuchochea kutenda mema, kwa kuwa “upendo haumfanyii uovu jirani ya mtu.” (Waroma 13:10) Tunapowapenda watu, hatuwezi hata kufikiria kumtendea mtu yeyote kwa njia mbaya.

Hilo ndilo jambo ambalo Ray, kutoka Pennsylvania, Marekani, alijifunza. Kwa kuwa alijifunza kupigana alipokuwa mdogo, alibandikwa jina Punch (Ngumi). Pia alikuwa na tatizo la kukasirika upesi. Hata hivyo, alipotumia kanuni za Biblia alianza kufanya mabadiliko. Lakini haikuwa rahisi sikuzote. Nyakati nyingine, alihisi hivi kama Paulo, aliyeandika vitabu fulani vya Biblia: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” (Waroma 7:21) Sasa baada ya kujitahidi sana kwa miaka mingi, Ray amefaulu “kuushinda uovu kwa wema.”—Waroma 12:21.

Kwa nini inafaa kujitahidi “kutembea katika njia ya watu wema”? (Methali 2:20-22) Kwa sababu, mwishowe wema utashinda uovu. Biblia inasema: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali . . . bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena . . . Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:9-11) Mungu ataondoa uovu wote. Watu wanaojitahidi kufanya mema wanangojea wakati ujao mzuri kama nini!

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Ni nani anayetuamulia jinsi ambavyo tutatenda?—Yakobo 1:14.

● Je, tunaweza kubadili mwenendo wetu?—Isaya 1:16, 17.

● Je, uovu utawahi kwisha?—Zaburi 37:9, 10; Methali 2:20-22.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Mtu huwa mwema au mwovu kwa kiwango anachochagua