Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitayarishe kwa Ajili ya Magumu

Jitayarishe kwa Ajili ya Magumu

Jitayarishe kwa Ajili ya Magumu

“Niliamua kuacha kuvuta sigara ili nisidhuru afya ya mtoto wetu aliyekuwa tu amezaliwa. Kwa hiyo, ndani ya nyumba niliweka ishara inayosema ‘Usivute Sigara.’ Saa moja tu baada ya kufanya hivyo, nilishambuliwa kwa ghafula na hamu ya kutumia nikotini na nikawasha sigara.”—Yoshimitsu, Japani.

KAMA kisa cha Yoshimitsu kinavyoonyesha, kuna magumu ya kuacha kuvuta sigara. Isitoshe, uchunguzi unaonyesha kwamba karibu asilimia 90 ya wale wanaojikwaa hurudia zoea lao. Kwa hiyo, ikiwa unajaribu kuacha, huenda tu ukafaulu ukijitayarisha. Ni magumu gani ambayo hutokea kwa ukawaida?

Hamu ya kutumia nikotini: Kwa kawaida hamu hiyo huwa kubwa zaidi siku tatu baada ya kuacha kuvuta sigara na hupungua baada ya majuma mawili hivi. Katika kipindi hicho, “tamaa hiyo huja kama mawimbi; haiji kila wakati,” anasema mtu mmoja aliyeacha kuvuta sigara. Hata miaka inapopita, huenda ukashikwa na tamaa ya kuvuta sigara. Ikikushika, usivute sigara mara moja. Subiri kwa dakika tano hivi, tamaa hiyo itakwisha.

Dalili nyingine: Mwanzoni, ni vigumu kuwa macho au kukaza fikira na huenda mtu akaongeza uzito kwa urahisi. Huenda pia akapatwa na maumivu ya viungo, akatokwa na jasho, akahisi anataka kujikunakuna, kukohoa, na hisia zake zikabadilika-badilika kama vile kutokuwa na subira, kukasirika kwa urahisi, au hata kushuka moyo. Hata hivyo, dalili nyingi huisha baada ya majuma manne hadi sita.

Wakati huo, kuna mambo fulani yanayoweza kukusaidia. Kwa mfano:

● Lala kwa muda mrefu zaidi.

● Kunywa maji mengi au maji ya matunda. Kula chakula chenye lishe.

● Fanya mazoezi ya kadiri.

● Vuta pumzi kabisa, na uwazie hewa safi ikijaa ndani ya mapafu yako.

Vichochezi: Huu ni utendaji au hisia zinazoweza kuchochea hamu ya kuvuta sigara. Kwa mfano, huenda kwa kawaida ulivuta sigara ulipokuwa ukinywa kinywaji fulani. Kwa hiyo, unapojaribu kuacha kuvuta sigara, epuka kunywa kinywaji hicho polepole. Bila shaka, baada ya muda utafurahia kunywa kinywaji hicho kwa utaratibu.

Hata hivyo, huenda hisia fulani zisiishe hata baada ya mwili wako kupoteza uraibu wa nikotini. “Miaka kumi na tisa baada ya kuacha kuvuta sigara,” anasema Torben, aliyetajwa mapema, “bado ninashikwa na hamu ninapokunywa kahawa.” Hata hivyo, muda unapopita mtu huacha kuhusianisha kuvuta sigara na utendaji fulani hususa.

Hata hivyo, mambo ni tofauti kileo kinapohusika. Kwa kweli, unapojaribu kuacha kuvuta sigara, huenda ukahitaji kuacha kutumia kileo na kuepuka maeneo ambako kinapatikana kwa sababu idadi kubwa ya watu ambao hurudia zoea la kuvuta sigara hufanya hivyo wanapokunywa kileo. Kwa nini?

● Hata kiasi kidogo cha kileo humfanya mtu afurahie nikotini.

● Mara nyingi mahali ambapo watu hunywa pamoja wao pia huvuta sigara.

● Kileo hudhoofisha uwezo wa kuamua mambo na kumfanya mtu atende kwa njia isiyo ya kawaida. Biblia inasema hivi: ‘Divai ndiyo huondoa kusudi jema.’—Hosea 4:11.

Marafiki: Uwe mteuzi. Kwa mfano, epuka watu wanaovuta sigara au wanaoweza kukupa sigara. Pia, waepuke watu wanaojaribu kuvuruga jitihada zako za kuacha kuvuta sigara, labda kwa kukudhihaki.

Hisia: Katika uchunguzi mmoja karibu asilimia 66 ya wale walioanza tena kuvuta sigara walifanya hivyo baada tu ya kufadhaika au kupandwa na hasira. Ukipatwa na hisia fulani inayokuchochea kuvuta sigara, jikengeushe fikira labda kwa kunywa maji, kutafuna chingamu, au kutembea. Jaribu kufikiria mambo yanayofaa, labda kwa kusali kwa Mungu au kusoma kurasa kadhaa za Biblia.—Zaburi 19:14.

Visingizio Unavyopaswa Kuepuka

Nitavuta mara moja tu.

Ukweli: Kuvuta mara moja tu kunaweza kutosheleza asilimia 50 hivi ya vipokezi vya nikotini kwenye ubongo wako kwa saa tatu. Matokeo yatakuwa kwamba utaanza tena kuvuta sigara.

Kuvuta sigara hunisaidia kutuliza mfadhaiko.

Ukweli: Uchunguzi unaonyesha kwamba nikotini huongeza kiwango cha homoni zinazomfanya mtu afadhaike. Hisia zozote zinazokudanganya kuwa mfadhaiko wako unapungua unapovuta sigara zinaweza kuwa zinasababishwa tu na athari za kuacha kuvuta sigara.

Nimekuwa nikivuta sigara kwa muda mrefu sana siwezi kuacha.

Ukweli: Kukazia fikira mambo yasiyofaa huvunja moyo. Biblia inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Kwa hiyo, usifikirie huwezi kuacha kuvuta sigara. Mtu yeyote ambaye kwa kweli anataka kuacha kuvuta sigara na anayefuata kanuni zinazofaa, kama zile zilizotajwa katika gazeti hili, anaweza kufanikiwa.

Siwezi kukabiliana na athari zinazosababishwa na kuacha kuvuta sigara.

Ukweli: Ni kweli kwamba athari za kuacha kuvuta sigara zina nguvu, lakini zitapungua baada ya majuma machache tu. Kwa hiyo usife moyo! Ukishikwa na hamu ya kuvuta sigara baada ya miezi au miaka kadhaa, hiyo pia itakwisha, labda hata baada ya dakika chache, ikiwa hutavuta sigara.

Nina tatizo la akili.

Ukweli: Ikiwa unatibiwa tatizo la akili, kama vile mshuko wa moyo au schizophrenia, mwombe daktari akusaidie uache kuvuta sigara. Bila shaka, atajitahidi kukusaidia labda hata atabadili matibabu yako ili yasiongeze ugonjwa wako au kuathiri dawa unazotumia.

Ninapoanza tena kuvuta sigara mimi hujihisi bure.

Ukweli: Unapojikwaa na kuanza tena kuvuta sigara, kama watu wengi wanavyofanya wanapojaribu kuacha kuvuta, wewe si bure. Inuka na ujitahidi tena. Kuanguka hakumaanishi umeshindwa. Kukataa kuinuka ndiko kushindwa. Kwa hiyo, endelea kujitahidi. Mwishowe utafanikiwa.

Fikiria mfano wa Romualdo, aliyevuta sigara kwa miaka 26. Aliacha kuvuta sigara zaidi ya miaka 30 iliyopita. Anaandika hivi: “Niliacha kuhesabu mara ambazo nilijikwaa. Kila mara nilijihisi vibaya sana, kana kwamba singeweza kufaulu. Hata hivyo, nilipoazimia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu na kumwomba mara nyingi anisaidie, mwishowe nilifaulu kuacha kuvuta sigara kabisa.”

Katika habari ya mwisho ya mfululizo huu, tutachunguza mapendekezo mengine machache yanayofaa yanayoweza kukusaidia kuwa mwenye furaha unapoacha kuvuta sigara.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

HATARI HATA ITUMIWE JINSI GANI

Tumbaku inatumiwa katika njia nyingi tofauti-tofauti. Tumbaku fulani huuzwa katika maduka yanayouza dawa na bidhaa zenye vyakula vya kuboresha afya. Hata hivyo, “tumbaku ni hatari hata itumiwe kwa njia gani,” linasema Shirika la Afya Ulimwenguni. Mtu anaweza kufa kutokana na magonjwa yanayosababishwa na tumbaku kama vile, kansa na magonjwa ya moyo. Akina mama waja-wazito wanaovuta sigara wanaweza kuwadhuru watoto wao walio tumboni. Watu hutumia tumbaku za aina gani?

Bidis: Sigara hizo ndogo zilizotengenezwa kwa mkono hutumiwa sana katika nchi za Asia. Mtu anapovuta bidis anapata lami, nikotini, na kaboni monoksidi nyingi zaidi kuliko sigara za kawaida.

Biri: Tumbaku za aina hii husokotwa kwa majani ya tumbaku au karatasi iliyotengenezwa kwa tumbaku. Kwa kulinganisha na asidi ya tumbaku iliyo kwenye sigara, tumbaku iliyo kwenye biri hufanya nikotini iingie kupitia mdomo hata ikiwa biri haijawashwa.

Kreteks, au sigara za karafuu: Kwa kawaida zinakuwa na asilimia 60 hivi ya tumbaku na asilimia 40 ya karafuu. Mtu anapozivuta anapata lami, nikotini, na kaboni monoksidi nyingi zaidi kuliko sigara za kawaida.

Viko: Kuvuta kiko na kuvuta sigara kuna hatari zilezile, kwa kuwa mazoea yote mawili yanaweza kutokeza kansa zilezile na magonjwa mengine.

Tumbaku zisizokuwa na moshi: Hilo linatia ndani kutafuna na kunusa tumbaku, na gutkha inayotumiwa Kusini-Mashariki ya Asia. Nikotini huingia kwenye damu kupitia mdomo. Ni hatari kutumia tumbaku hizo zisizokuwa na moshi kama tu tumbaku nyingine.

Tumbaku inayovutwa kupitia maji: Moshi wa tumbaku inayovutwa kwa njia hiyo hupitishwa kwenye maji kabla ya kuvutwa. Hata hivyo, mbinu hiyo haipunguzi kiasi cha sumu, kutia ndani zile zinazosababisha kansa, ambazo huingia kwenye mapafu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

KUMSAIDIA MTU MWINGINE KUACHA

Usiwe mchambuzi. Kumsifu mtu na kumpongeza huwa na matokeo mazuri kuliko kulalamika na kumzomea. Kusema “Nafikiri utafaulu ukijaribu tena” ni afadhali kuliko kusema “Ona sasa umeshindwa tena!”

Uwe mwenye kusamehe. Jitahidi kutofunga kinyongo unapokasirikiwa na mtu anayejaribu kuacha kuvuta sigara. Tumia maneno yenye fadhili kama vile: “Najua ni vigumu, lakini pongezi kwa kujitahidi sana.” Usiseme: “Ulikuwa mtu mzuri zaidi ulipokuwa ukivuta sigara!”

Uwe rafiki wa kweli. Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Naam, “nyakati zote” jaribu kuwa na subira na kumwonyesha upendo mtu anayejaribu kuacha, hata iwe ni saa ngapi au mtu awe anakabili hisia gani.