Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini Ili Nijiamini Zaidi?

Nifanye Nini Ili Nijiamini Zaidi?

Vijana Huuliza

Nifanye Nini Ili Nijiamini Zaidi?

NDIYO | HAPANA

Unapojitazama kwenye kioo, je, unavutiwa na jinsi ulivyo?

Je, unaona kwamba una sifa zenye kuheshimika?

Je, unaweza kukabiliana na shinikizo kutoka kwa vijana wenzako?

Je, unaweza kuvumilia uchambuzi wa kweli?

Je, unaweza kustahimili unapoambiwa maneno yanayokuudhi?

Je, unahisi kuwa unapendwa?

Je, wewe hutunza afya yako?

Je, wewe hufurahi wengine wanapofanikiwa?

Je, wewe hujiona kuwa mtu mwenye mafanikio?

Ikiwa kuna maswali fulani kati ya haya ambayo umejibu hapana, huenda hujiamini hivi kwamba unashindwa kuona sifa zako nzuri. Habari hii itakusaidia kutambua sifa hizo nzuri!

VIJANA wengi wanakabiliwa na mahangaiko kuhusu sura yao, uwezo wao, na pia vile vijana wenzao wanavyowaona. Je, unahisi hivyo pia? Ikiwa unahisi hivyo, basi si wewe tu.

“Kutokamilika kwangu hunifanya nishuke moyo. Kwa kawaida, mimi hujichambua sana.”—Leticia. *

“Hata uwe mrembo kadiri gani, bado utakutana na wengine ambao ni warembo kuliko wewe.”—Haley.

“Mimi huhangaika sana ninapokuwa na wengine. Mimi huhofu kwamba watanidharau.”—Rachel.

Ikiwa wewe huhisi kama vijana waliotajwa hapo juu, usife moyo. Unaweza kupata msaada. Hebu tuchunguze njia tatu zinazoweza kukusaidia ujiamini zaidi na pia uwe na maoni yanayofaa kujihusu.

1. Tafuta Marafiki

Andiko la msingi. “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Linamaanisha nini. Rafiki wa kweli anaweza kutuimarisha sana wakati wa taabu. (1 Samweli 18:1; 19:2) Kujua tu kwamba mtu fulani anakujali kunaweza kukutia moyo. (1 Wakorintho 16:17, 18) Kwa hiyo, fanya urafiki na wale walio na uvutano mzuri kwako.

“Marafiki wa kweli watakutia moyo.”—Donnell.

“Nyakati nyingine jambo muhimu ni kujua kwamba mtu fulani anakujali kikweli. Hilo linaweza kufanya ujihisi ukiwa mwenye thamani.”—Heather.

Tahadhari: Hakikisha kwamba marafiki wako hakufanyi ufiche jinsi ulivyo ili tu ukubalike. (Methali 13:20; 18:24; 1 Wakorintho 15:33) Ukijihusisha katika matendo ya kipumbavu ili tu kuwapendeza wengine, utajivunjia heshima na utahisi umetumiwa vibaya.—Waroma 6:21

Andika maoni yako. Hapa chini, andika jina la rafiki anayeweza kukusaidia ujiamini zaidi.

․․․․․

Mbona usipange kutumia wakati pamoja na rafiki huyo uliyemtaja hapo juu? Taarifa: Si lazima rafiki huyo awe wa rika lako.

2. Jitoe kwa Wengine

Andiko la msingi. “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Linamaanisha nini. Unapowasaidia wengine, unafaidika pia. Jinsi gani? “Mtu mkarimu atafanikishwa,” inasema methali moja ya Biblia. “Amnyweshaye mwingine maji naye atanyweshwa.” (Methali 11:25, Biblia Habari Njema) Hiyo ni kweli kabisa—utakuwa na hali njema unapowasaidia wengine! *

“Mimi hufikiria jinsi ninavyoweza kuwasaidia wengine kutanikoni wanaohitaji msaada. Mimi huhisi vizuri zaidi ninapoonyesha wengine upendo na kuwafikiria.”—Breanna.

“Huduma ya Kikristo inathawabisha kwa kuwa inakufanya uache kujifikiria na uanze kuwafikiria wengine.”—Javon.

Tahadhari: Usiwasaidie wengine ukiwa na wazo la kupata thawabu. (Mathayo 6:2-4) Hutafaidika unapotoa ukiwa na nia mbaya. Kwa kweli, itakuwa wazi kwamba huo ni wonyesho tu wa nje!—1 Wathesalonike 2:5, 6.

Andika maoni yako. Fikiria kuhusu mtu uliyesaidia wakati fulani. Alikuwa nani, na ulimsaidia jinsi gani?

․․․․․

Baadaye ulihisi namna gani?

․․․․․

Fikiria kuhusu mtu mwingine unayeweza kusaidia, na uandike hapa chini jinsi unavyoweza kumsaidia.

․․․․․

3. Usife Moyo Unapofanya Makosa

Andiko la msingi. “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23.

Linamaanisha nini. Ni wazi kwamba hujakamilika. Hilo linamaanisha kwamba nyakati nyingine utasema au kutenda jambo lisilofaa. (Waroma 7:21-23; Yakobo 3:2) Ingawa huwezi kuepuka kufanya makosa, unaweza kudhibiti jinsi unavyoyashughulikia. Biblia inasema hivi: “Kwa maana huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.”—Methali 24:16.

“Nyakati nyingine mtu huhisi kwamba hajiheshimu anapolinganisha udhaifu wake na uwezo wa mtu mwingine.”—Kevin.

“Kila mtu ana sifa nzuri na sifa mbaya pia. Tunapaswa kujivunia sifa zetu nzuri na kujaribu sana kurekebisha zile mbaya.”—Lauren.

Tahadhari: Usitumie kutokamilika kwako kuwa kizingizio cha kutenda dhambi. (Wagalatia 5:13) Unapojihusisha katika dhambi kimakusudi, utakuwa unajitenga na mtu wa maana kuliko wote—Yehova Mungu!—Waroma 1:24, 28.

Andika maoni yako. Andika hapa chini sifa moja ambayo ungependa kufanyia kazi.

․․․․․

Andika tarehe ya leo kando ya sifa uliyoandika hapo juu. Fanya utafiti uone jinsi unavyoweza kuboresha sifa hiyo na ukague maendeleo yako baada ya mwezi mmoja.

Thamani Yako ya Kweli

Biblia inasema kwamba “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu.” (1 Yohana 3:20) Hilo linamaanisha kwamba Mungu anaweza kuona thamani yako, hata kuliko unavyojiona. Lakini je, kutokamilika kwako, kunabadili ukweli huo? Wazia kwamba una noti ya dola 100 iliyoraruka kidogo tu. Je, utaiona kuwa haina thamani yoyote na kuitupa kwa sababu tu imeraruka? La hasha! Iwe imeraruka au la bado ina thamani ya dola 100.

Hivyo ndivyo Mungu anavyokuthamini. Yeye hutambua na kuthamini jitihada zako za kumpendeza, hata ikiwa unaziona kuwa duni! Kwa kweli, Biblia inatuhakikishia kwamba “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Waebrania 6:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 30 Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, hebu wazia shangwe utakayopata unapoeleza wengine kuhusu ujumbe wa Ufalme.—Isaya 52:7.

MAMBO YA KUFIKIRIA

Utafanya nini unapohisi kuwa umeshuka moyo kwa sababu

● Marika wako wanakuchambua sana?

● Unahisi kwamba wenzako ni bora zaidi yako?

● Unaona udhaifu wako tu?

[Blabu katika ukurasa wa 27]

“Mtu anaweza kuwa mwenye sura nzuri na bado ahisi kwamba hapendezi. Au, mtu anaweza kuwa na sura isiyopendeza lakini bado ahisi kwamba yeye ni mrembo kuliko kila mtu. Yote yanategemea mtazamo wa mtu.”—Alyssa

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Hata jengo lenye nguvu zaidi linahitaji kuimarishwa, na nyakati nyingine, kufanyiwa ukarabati. Mara nyingi, nilitegemezwa sana na rafiki aliyeniambia maneno yenye upendo au hata alipotabasamu au kunikumbatia.”

“Badala ya kuwaonea wivu watu walio na sifa nzuri, tunaweza kunufaika zaidi kutokana na sifa zao nzuri kama vile wao pia wanavyoweza kunufaika kutokana na sifa zetu nzuri.”

[Picha]

Aubrey

Lauren

[Picha katika ukurasa wa 28]

Thamani ya pesa haipungui kwa sababu tu noti imeraruka. Vivyo hivyo, thamani yako machoni pa Mungu haipungui kwa sababu ya kutokamilika kwako